Hamia kwenye habari

FEBRUARI 22, 2023
NIGERIA

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Pijini (ya Afrika Magharibi) na Lugha ya Urhobo

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo Yatolewa Katika Lugha ya Pijini (ya Afrika Magharibi) na Lugha ya Urhobo

Februari 12, 2023, Ndugu Jeffrey Winder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Pijini (ya Afrika Magharibi) na katika lugha ya Urhobo. Programu hiyo ilipeperushwa kwa makutaniko nchini Nigeria na kwa ujumla ilitazamwa na watu 559,326 nchini humo. Mara tu baada ya Biblia hiyo kutolewa, ilipatikana kwenye tovuti na watu wangeweza kuipakua. Nakala zilizochapishwa zitapatikana baadaye mwaka huu.

Kutaniko la kwanza la lugha ya Pijini (ya Afrika Magharibi) lilianzishwa mwaka wa 2015. Sasa, kuna zaidi ya makutaniko 1,100 ya lugha ya Pijini (ya Afrika Magharibi) nchini Nigeria na pia kuna makutaniko mengi katika nchi nyingine kama vile Uingereza na Marekani. Hapo awali, makutaniko hayo yalitumia toleo la Kiingereza la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Ndugu mmoja alisema hivi: “Hapo awali, tulihubiri katika lugha ya Pijini na kisha tukasoma andiko kwenye Biblia ya Kiingereza, na haikuwa rahisi. Wakati mwingine, mwenye nyumba hakuelewa jambo kuu baada ya kumsomea andiko. Lakini sasa, tutahubiri katika lugha ya Pijini na tutawasomea Biblia ya Pijini. Kwa kuwa tutasoma Biblia inayotumia lugha ya asili ya mwenye nyumba, ataelewa vizuri zaidi ujumbe wetu.”

Kuishi Katika Tumaini la Taratibu Mpya Yenye Haki, kijitabu cha kwanza kutafsiriwa katika lugha ya Urhobo

Kutaniko la kwanza la lugha ya Urhobo lilianzishwa mwaka wa 1933. Mwaka wa 1968, ndugu zetu walitafsiri kijitabu kilichoitwa Kuishi Katika Tumaini la Taratibu Mpya Yenye Haki. Hicho kilikuwa kijitabu cha kwanza kutafsiriwa katika lugha ya Urhobo. Tangu wakati huo, idadi ya makutaniko ya Urhobo imeongezeka kufikia makutaniko 103. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo iliyotolewa katika lugha ya Urhobo itakuwa baraka kubwa kwa makutaniko hayo kwa sababu Biblia hiyo inatumia lugha rahisi na inayoeleweka.

Tunasali kwamba tafsiri hizi ziwasaidie watu wengine wengi “[wajazwe] ujuzi sahihi” wa Mungu.​—Wakolosai 1:9.