Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Watoto na Simu za Mkononi​—Sehemu ya 1: Je, Mtoto Wangu Anastahili Kuwa na Simu ya Mkononi?

Watoto na Simu za Mkononi​—Sehemu ya 1: Je, Mtoto Wangu Anastahili Kuwa na Simu ya Mkononi?

 Watoto wengi wana simu za mkononi, a na wengi wao hutumia simu hizo kuingia kwenye Intaneti wakiwa peke yao chumbani. Kuna hatari gani ikiwa utamruhusu mtoto wako awe na simu ya mkononi? Kuna manufaa gani? Mtoto wako anapaswa kutumia simu kwa kipindi gani cha wakati?

 Unachopaswa kujua

 Manufaa

  •   Ni ulinzi kwa watoto, na amani ya akili kwa wazazi. Bethany, mama ya vijana wawili anasema hivi: “Tunaishi katika ulimwengu hatari, ni muhimu kwa watoto kuweza kuwasiliana na wazazi wao.”

     Mama anayeitwa Catherine anaongezea kwa kusema hivi: “Kwa kutumia programu fulani, unaweza kuunganisha simu yako na ya mtoto wako ili uweze kujua yuko wapi. Ikiwa anaendesha gari, unaweza kujua ikiwa anaendesha kwa mwendo gani.”

  •   Inasaidia kufanya kazi za shule. Mama anayeitwa Marie anasema hivi: “Watoto hutumiwa kazi za shule kupitia barua-pepe au ujumbe mfupi, na wanaweza pia kuwasiliana na walimu wao kwa njia hiyo.”

 Hatari

  •   Kutumia simu kupita kiasi. Ni kawaida kwa vijana kutumia simu zao kwa saa kadhaa kila siku. Kwa kweli, muda ambao wazazi pia hutumia vifaa vyao vya kielektroni unalingana na muda wanaotumia pamoja na watoto wao. Mshauri mmoja alisema baadhi ya nyumba zimekuwa kama “mkutano unaofanywa kila siku na watu wasiofahamiana ambao macho yao yamekazwa kwenye mashine.” b

  •   Ponografia. Kulingana na kadirio moja, kila mwezi zaidi ya nusu ya vijana wote hutafuta ponografia. Jambo hilo halishangazi kwa kuwa ni rahisi sana kuipata kupitia simu za mkononi. William, baba ya vijana wawili anasema hivi: “Wazazi wanapomruhusu mtoto kuwa na simu ya mkononi, huenda wakawa wanamfungulia mlango wa duka la ponografia ambalo mtoto wanaweza kuingia akiwa popote pale.”

  •   Kuitegemea. Watu wengi wanapenda sana simu zao. Ikipotea kwa muda mfupi tu, wengi wao husema kwamba wanashikwa na hofu, wanakuwa na wasiwasi, na hata wanajihisi wagonjwa. Wazazi fulani wanasema kwamba watoto wao hukosa adabu wanapotumia simu zao. Carmen anasema hivi: “Wakati mwingine ninapotaka kuzungumza na mtoto wangu, yeye huzungusha macho kwa dharau au husema neno lenye kukosa heshima kwa kuwa hataki kusumbuliwa.”

  •   Hatari za ziada. Simu ya mkononi inaweza kuwa chanzo cha kunyanyaswa mtandaoni na kutumiwa jumbe chafu, pia inaweza kusababisha matatizo mengi ya afya yanayotokana na kuketi vibaya na kutolala vizuri. Vijana fulani hutumia programu zinazoficha programu nyingine (ghost)—ambazo huenda zikaonekana kuwa hazina madhara, kama vile kikokotoo—ili kuficha habari ambazo hawataki wazazi wao wazijue.

     Daniel, baba ya msichana tineja, anasema hivi: “Simu ya mkononi hufungua dirisha na kumruhusu mtu kutazama chochote katika Intaneti—iwe ni kizuri ama kibaya.”

 Unachopaswa kuuliza

  •   ‘Je, mtoto wangu anahitaji simu ya mkononi?’

     Biblia inasema hivi: “Mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Ukiwa na hilo akilini, jiulize:

     ‘Je, ni jambo la hekima kumpa mtoto wangu simu ya mkononi kwa sababu tu ya ulinzi au mambo mengine? Je, nimechanganua manufaa na hatari zinazohusika? Je, ninaweza kutumia njia nyingine badala ya kumpa simu ya mkononi?’

     Baba anayeitwa Todd anasema hivi: “Simu za kawaida bado zinapatikana na mtoto wako anaweza kuwasiliana nawe kwa kupiga simu au kutuma ujumbe mfupi. Pia utaokoa pesa nyingi.”

  •   ‘Je, mtoto wangu ni mkomavu vya kutosha?’

     Biblia inasema hivi: “Moyo wa mwenye hekima humwongoza katika njia inayofaa.” (Mhubiri 10:2) Ukiwa na hilo akilini, jiulize hivi:

     ‘Ni jambo gani linalonisadikisha kwamba ninaweza kumwamini mtoto wangu? Je, sisi tuna mawasiliano mazuri tayari? Je, mtoto wangu ana tatizo la kusema uwongo, huenda hata kunificha nisiwafahamu rafiki zake? Je, tayari anajua jinsi ya kudhibiti matumizi ya vifaa vingine kama vile televisheni, tablet, au kompyuta?’ Mama anayeitwa Serena anasema hivi: “Simu ya mkononi ni kifaa bora na chenye nguvu sana. Fikiria jukumu unalomkabidhi mtoto wako ambaye bado hana uzoefu mwingi.”

  •   ‘Je, mimi niko tayari kushughulikia jukumu hilo?’

     Biblia inasema hivi: ‘Mzoeze mtoto njia anayopaswa kuifuata.’ (Methali 22:6; maelezo ya chini) Ukiwa na hilo akilini, jiulize hivi:

     ‘Je, ninajua habari za kutosha kuhusu simu kiasi cha kuweza kumsaidia mtoto wangu kuelewa na kuepuka hatari ambazo huenda zikatokea? Je, ninajua jinsi ya kuweka vizuizi vya mzazi katika simu ya mtoto wangu? Ninaweza kumsaidiaje mtoto wangu kutumia simu yake vizuri?’ Daniel, baba aliyetajwa mwanzoni anasema: “Nimeona wazazi wengi wakiwapa tu watoto wao simu ya mkononi bila kuchunguza jinsi wanavyoitumia.”

 Jambo kuu: Watoto wanahitaji kuzoezwa kutumia simu za mkononi kwa hekima. Kitabu Indistractable kinasema hivi: “Ni jambo lisilopatana na akili kutarajia kwamba watoto wetu hawatashawishika kutumia kupita kiasi vifaa vya kielektroni hasa wakati ambapo wazazi hawawaandalii usimamizi wowote.”

a Katika makala hii, neno “simu ya mkononi” linatumiwa kumaanisha simu iliyo na uwezo wa kuingia kwenye Intaneti.

b Kutoka kitabu Disconnected, cha Thomas Kersting.