Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kumhusu Danieli?

Biblia Inasema Nini Kumhusu Danieli?

Jibu la Biblia

 Danieli alikuwa nabii Myahudi aliyeishi katika karne ya saba na ya sita K.W.K. Mungu alimwezesha kueleza maana ya ndoto, pia alimpa maono kuhusu matukio ya wakati ujao, na alimwongoza kwa roho kuandika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake, yaani, kitabu cha Danieli.​—Danieli 1:17; 2:19.

Danieli Alikuwa Nani?

 Danieli alilelewa katika ufalme wa Yuda. Jiji la Yerusalemu na hekalu la Wayahudi lilikuwa sehemu ya ufalme huo. Mwaka wa 617 K.W.K., mfalme Nebukadneza wa Babiloni, alivamia Yerusalemu na kuwateka “viongozi wa nchi” akawapeleka uhamishoni Babiloni. (2 Wafalme 24:15; Danieli 1:1) Danieli, ambaye huenda wakati huo alikuwa tineja, alitekwa pia.

 Daneli na vijana wengine (kutia ndani Shadraki, Meshaki na Abednego) walipelekwa kwenye makao ya mfalme wa Babiloni ili kupata mafunzo ya pekee kwa ajili ya kumtumikia mfalme. Ingawa walishinikizwa kukana imani yao, Danieli na rafiki zake watatu walibaki washikamanifu kwa Mungu wao, Yehova. (Danieli 1:3-8) Baada ya kupata mafunzo kwa miaka mitatu, Mfalme Nebukadneza aliwasifu kwa sababu ya hekima na ujuzi wao, na akasema kwamba “walikuwa bora mara kumi kuliko makuhani wote wachawi na watu waliofanya mazingaombwe katika milki yake yote.” Alimchagua Danieli na rafiki zake kutumikia katika makao ya mfalme.​—Danieli 1:18-20.

 Miongo mingi baadaye, Danieli alipokuwa na umri wa miaka 90 hivi, aliitwa kwenye makao ya mfalme. Mwanamume aliyeitwa Belshaza, ambaye alikuwa akitawala Babiloni wakati huo, alimwomba Danieli amweleze maana ya maandishi yaliyokuwa yametokea ghafula ukutani. Kwa mwongozo wa Mungu, Danieli alieleza kwamba milki ya Babiloni ingeshindwa na milki ya Wamedi na Waajemi. Jiji la Babiloni lilitekwa usiku huohuo.​—Danieli 5:1, 13-31.

 Chini ya utawala wa Wamedi na Waajemi, Danieli aliteuliwa kuwa ofisa mkuu na Mfalme Dario alitaka kumuongezea madaraka zaidi. (Danieli 6:1-3) Maofisa wenye wivu walipanga njama ili Danieli auawe kwa kutupwa ndani ya shimo la simba. (Danieli 6:4-23) Danieli alipokaribia mwisho wa maisha yake, malaika alimtokea na mara mbili alimwita Danieli “mtu mwenye thamani sana.”​—Danieli 10:11, 19.

 Jionee matukio hayo katika drama ya Biblia iliyo na sehemu mbili yenye kichwa, Danieli Alionyesha Imani Maisha Yake Yote.