Hamia kwenye habari

Dhambi Isiyoweza Kusamehewa Ni Nini?

Dhambi Isiyoweza Kusamehewa Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Dhambi isiyoweza kusamehewa ni matendo yanayoambatana na mtazamo unaomzuia mtenda-dhambi kusamehewa na Mungu. Mtazamo huo huanzaje?

 Mungu huwasamehe wale wanaotubu dhambi zao, wanaofuata viwango vyake maishani, na kumwamini Yesu Kristo. (Matendo 3:​19, 20) Hata hivyo, mtu anaweza kukita mizizi katika kutenda dhambi hivi kwamba asibadili kamwe mtazamo au mwenendo wake mbaya. Katika Biblia mtu wa aina hiyo hurejelewa kuwa na “moyo mwovu” uliofanywa “kuwa mgumu kwa nguvu za udanganyifu za dhambi.” (Waebrania 3:​12, 13) Kama udongo uliopitishwa katika tanuru usivyoweza kufinyangwa tena, ndivyo moyo wa mtu huyo unavyodumu katika ukaidi wake dhidi ya Mungu. (Isaya 45:9) Hivyo, kwa kuwa hakuwezi kuwa na msingi wowote wa mtu huyo kusamehewa, anakuwa amefanya dhambi isiyoweza kusamehewa.​—Waebrania 10:26, 27.

 Yesu alipokuwa duniani, baadhi ya viongozi wa dini ya Kiyahudi walitenda dhambi isiyoweza kusamehewa. Ingawa walifahamu kwamba Yesu alifanya miujiza kwa nguvu za roho takatifu ya Mungu, walimshutumu kuwa nguvu zake zilitoka kwa Shetani Ibilisi.​—Marko 3:​22, 28-​30.

Mifano ya dhambi zinazosamehewa

  •  Kukufuru kwa sababu ya kukosa ujuzi. Mtume Paulo ambaye awali alikuwa mkufuru, alisema hivi: “Nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilikosa ujuzi nami nilitenda kwa ukosefu wa imani.”​—1 Timotheo 1:​13.

  •  Uzinzi. Biblia inawataja wale ambao wakati mmoja walifanya uzinzi lakini walibadili mwenendo wao na kusamehewa na Mungu.​—1 Wakorintho 6:​9-​11.

“Je, nimetenda dhambi isiyoweza kusamehewa?”

 Ikiwa unajutia kikweli dhambi ulizofanya zamani na unataka kubadili mwenendo wako, ni wazi kwamba hujatenda dhambi isiyoweza kusamehewa. Mungu anaweza kukusamehe hata ikiwa umerudia dhambi ileile mara kadhaa, maadamu hujaufanya moyo wako kuwa mgumu dhidi yake.​—Methali 24:16.

 Watu fulani wanahisi kwamba wamefanya dhambi isiyoweza kusamehewa kwa sababu wanasumbuliwa na hatia. Hata hivyo, Biblia inatufundisha kwamba hisia zetu zinaweza kutudanganya. (Yeremia 17:9) Mungu hajatupa mamlaka ya kumhukumu mtu yeyote​—kutia ndani sisi wenyewe. (Waroma 14:​4, 12) Yeye anaweza kutusamehe hata ikiwa mioyo yetu inatuhukumu.​—1 Yohana 3:​19, 20.

Je, Yuda Iskariote alifanya dhambi isiyoweza kusamehewa?

 Ndiyo. Akichochewa na pupa, aliiba pesa zilizotolewa kwa ajili ya utumishi mtakatifu. Yuda alijifanya anawahangaikia maskini wakati nia yake ilikuwa kukusanya pesa nyingi zaidi za kuiba. (Yohana 12:​4-8) Moyo wa Yuda ulipotia mizizi katika dhambi, alimsaliti Yesu kwa vipande 30 vya fedha. Yesu alijua kwamba Yuda hangetubu kikweli kwa kosa lake, na hivyo alimwita “mwana wa maangamizi.” (Yohana 17:12) Hilo lilimaanisha kwamba Yuda hangekuwa na tumaini la kufufuliwa baada ya kifo, angeangamia moja kwa moja.​—Marko 14:21.

 Yuda hakutubu kikweli dhambi yake. Aliungama dhambi yake kwa viongozi wa kidini alioshirikiana nao, lakini si kwa Mungu.​—Mathayo 27:​3-5; 2 Wakorintho 7:​10.