Hamia kwenye habari

Ni Nini Maana ya “Jicho kwa Jicho”?

Ni Nini Maana ya “Jicho kwa Jicho”?

Jibu la Biblia

 Sheria ya “jicho kwa jicho” ilikuwa sehemu ya Sheria ya Mungu ambayo alilipatia taifa la kale la Israeli kupitia Musa na Yesu alinukuu maneno hayo kwenye Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 5:​38; Kutoka 21:24, 25; Kumbukumbu la Torati 19:21) Maneno hayo yalimaanisha kwamba hukumu inapotolewa dhidi ya watenda mabaya, adhabu inapaswa kulingana na uhalifu uliotendwa. a

 Sheria hiyo ilitumiwa kuonya dhidi ya matendo ya kimakusudi ya kumdhuru mtu mwingine. Sheria ya Musa ilisema hivi kuhusu mtu aliyemdhuru mwenzake kimakusudi: “Mfupa uliovunjika kwa mfupa uliovunjika, jicho kwa jicho, jino kwa jino, atajeruhiwa kama alivyomjeruhi mwenzake.”​—Mambo ya Walawi 24:20.

 Kusudi la sheria ya “jicho kwa jicho” lilikuwa nini?

 Kuwepo kwa sheria ya “jicho kwa jicho” hakukumaanisha kwamba watu wanaruhusiwa kuchukua sheria mikononi. Badala yake, iliwasaidia mahakimu waliowekwa rasmi kutoa adhabu iliyofaa, wasiwe wakatili sana, wala wasitoe adhabu ndogo sana.

 Sheria hiyo pia iliwazuia watu wowote ambao wangefikiria kuwadhuru wengine kimakusudi au ambao wangepanga njama ya kufanya hivyo. Sheria ilieleza hivi: “Wale wanaobaki [ambao wangeona haki ya Mungu ikitekelezwa] watasikia na kuogopa, nao hawatatenda tena kamwe uovu kama huo miongoni mwenu.”​—Kumbukumbu la Torati 19:20.

 Je, sheria ya “jicho kwa jicho” inawahusu Wakristo?

 Hapana, sheria hiyo haiwahusu Wakristo. Ilikuwa sehemu ya Sheria ya Musa, ambayo ilifutwa na kifo cha kidhabihu cha Yesu.​—Waroma 10:4.

 Hata hivyo, sheria hiyo inatusaidia kuelewa njia ya Mungu ya kufikiri. Kwa mfano, inaonyesha kwamba Mungu anathamini haki. (Zaburi 89:14) Pia inafunua kiwango chake cha haki​—yaani, kwamba wanaotenda maovu wanapaswa kutiwa nidhamu “kwa kiwango kinachofaa.”​—Yeremia 30:11.

 Maoni yasiyo sahihi kuhusu sheria ya “jicho kwa jicho”

 Maoni yasiyo sahihi: Sheria ya “jicho kwa jicho” ilikuwa yenye ukatili kupita kiasi.

 Ukweli: Sheria hiyo haikuidhinisha kutoa hukumu zinazokandamiza na zenye ukatili. Badala yake, ilipotumiwa kwa njia nzuri, iliwaruhusu mahakimu waliostahili kutoa adhabu ya kosa baada tu ya kuchunguza hali zilizohusika na ni kwa kadiri gani kosa hilo lilikuwa la kimakusudi. (Kutoka 21:28-​30; Hesabu 35:22-​25) Hivyo, sheria ya “jicho kwa jicho” ilitenda kama kizuizi dhidi ya kutolewa kwa adhabu zinazopita kiasi.

 Maoni yasiyo sahihi: Sheria ya “jicho kwa jicho” iliidhinisha watu kuendeleza matendo ya kulipiza kisasi.

 Ukweli: Sheria ya Musa ilisema hivi: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo dhidi ya wana wa watu wako.” (Mambo ya Walawi 19:18) Badala ya kuwachochea watu kulipiza kisasi, Sheria iliwatia moyo watu kumtegemea Mungu na mfumo wa sheria ambao alikuwa ameukabidhi mamlaka ya kurekebisha makosa yote.​—Kumbukumbu la Torati 32:35.

a Kanuni hiyo ya kisheria, ambayo nyakati nyingine ilijulikana kwa maneno ya Kilatini lex talionis, ilitumiwa pia katika mifumo ya kisheria ya jamii nyingine za kale.