Hamia kwenye habari

Mnyama-Mwitu Mwenye Rangi Nyekundu wa Ufunuo Sura ya 17 Ni Nini?

Mnyama-Mwitu Mwenye Rangi Nyekundu wa Ufunuo Sura ya 17 Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu anayetajwa katika Ufunuo sura ya 17, ni ishara ya shirika ambalo kusudi lake ni kuunganisha na kuwakilisha mataifa ya ulimwengu huu. Mwanzoni lilitambuliwa kama Ushirika wa Mataifa na sasa linajulikana kama Umoja wa Mataifa.

Mambo yanayomtambulisha mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu

  1.   Shirika la kisiasa. Mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu ana “vichwa saba” vinavyowakilisha “milima saba” na “wafalme saba,” au mamlaka zinazotawala. (Ufunuo 17:​9, 10) Milima na wanyama-mwitu wanatumiwa katika Biblia kuwakilisha serikali.​—Yeremia 51:24, 25; Danieli 2:​44, 45; 7:​17, 23.

  2.   Mfano wa mfumo wa kisiasa wa ulimwenguni pote. Mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu anafanana na mnyama-mwitu mwenye vichwa saba anayetajwa kwenye Ufunuo sura ya 13, ambaye anawakilisha mfumo wa kisiasa wa ulimwenguni pote. Wanyama-mwitu hao wawili wana vichwa saba, pembe kumi, na majina yenye makufuru. (Ufunuo 13:1; 17:3) Kufanana huko ni muhimu. Mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu ni sanamu, au mfano, wa mfumo wa kisiasa wa ulimwenguni pote.​—Ufunuo 13:15.

  3.   Mamlaka kutoka kwa falme nyingine. Mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu “anatokana na,” au chanzo chake ni, falme nyingine zinazotawala.​—Ufunuo 17:11, 17.

  4.   Uhusiano na dini. Babiloni Mkubwa, yaani, dini zote za uwongo duniani, ameketi juu ya mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu, kuonyesha kwamba mnyama-mwitu huyo anaathiriwa na dini.​—Ufunuo 17:​3-5.

  5.   Anamvunjia Mungu heshima. Mnyama-mwitu ‘amejaa majina ya makufuru.’​—Ufunuo 17:3.

  6.   Angeacha kutenda kwa muda. Mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu angetiwa katika “abiso,” a au angeacha kutenda, kwa muda lakini angeinuka tena.​—Ufunuo 17:8.

Unabii wa Biblia watimia

 Ona jinsi ambavyo mashirika ya Umoja wa Mataifa na Ushirika wa Mataifa yametimiza unabii wa Biblia kumhusu mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu.

  1.   Shirika la kisiasa. Shirika la Umoja wa Mataifa linategemeza mfumo wa kisiasa kwa kudumisha “usawa kati ya Wanachama wake wote.” b

  2.   Mfano wa mfumo wa kisiasa wa ulimwenguni pote. Katika mwaka wa 2011, nchi ya 193 ilijiunga na shirika la Umoja wa Mataifa. Hivyo, shirika hilo linadai kuwa linawakilisha mataifa na watu wengi zaidi ulimwenguni.

  3.   Mamlaka kutoka kwa falme nyingine. Shirika la Umoja wa Mataifa haliwezi kuwepo bila maitafa yanayoifanyiza, na mamlaka yake inategemea mataifa hayo.

  4.   Kuhusianishwa na dini. Mashirika ya Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa yamekuwa yakitegemezwa na dini za ulimwengu huu. c

  5.   Kumvunjia Mungu heshima. Shirika la Umoja wa Mataifa lilianzishwa ili “kudumisha amani na usalama ulimwenguni pote.” d Ingawa huenda lengo hilo likaonekana kuwa lenye kusifika, shirika hilo linamvunjia Mungu heshima kwa kudai kufanya jambo ambalo ni Ufalme wake tu una uwezo wa kutimiza.​—Zaburi 46:9; Danieli 2:​44.

  6.   Kuacha kutenda kwa muda. Ushirika wa Mataifa, shirika ambalo lilifanyizwa muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu ili kudumisha amani, lilishindwa kuzuia uhasama kati ya mataifa. Shirika hilo liliacha kutenda Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza katika mwaka wa 1939. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokwisha katika mwaka wa 1945, shirika la Umoja wa Mataifa lilifanyizwa. Kusudi, mbinu, na muundo wake unafanana sana na ule wa Ushirika wa Mataifa.

a Kulingana na kitabu Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “abiso” linamaanisha “kina kisichoweza kupimwa.” Tafsiri ya King James Version inatumia neno “shimo lisilo na mwisho.” Katika Biblia, neno hilo linamaanisha mahali au hali ya kufungiwa bila utendaji wowote.

b Ona Kitengo cha 2 cha Mkataba wa Umoja wa Mataifa.

c Kwa mfano, baraza linalowakilisha dini nyingi za Kiprotestanti nchini Marekani lilitangaza katika mwaka wa 1918 kwamba Ushirika wa Mataifa ungekuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Mnamo 1965, wawakilishi wa Ubudha, Ukatoliki, Kanisa la Othodoksi la Mashariki, Uhindu, Uislamu, Uyahudi, na Uprotestanti walikusanyika kule San Francisco kutegemeza na kusali kwa ajili ya Umoja wa Mataifa. Na katika mwaka wa 1979, Papa John Paul wa Pili alieleza tumaini lake kwamba Umoja wa Mataifa “litaendelea daima kuwa baraza kuu zaidi la amani na haki.”

d Ona Kitengo cha 1 cha Mkataba wa Umoja wa Mataifa.