Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Mathayo 11:28-30​—“Njoni Kwangu, . . . Nami Nitawapumzisha”

Mathayo 11:28-30​—“Njoni Kwangu, . . . Nami Nitawapumzisha”

 “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu. Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”​—Mathayo 11:28-30, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya

 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”​—Mathayo 11:28-30, Biblia Habari Njema

Maana ya Mathayo 11:28-30

 Kwa uchangamfu Yesu aliwakaribisha wasikilizaji wake waje kwake. Aliwahakikishia kwamba, kwa kujifunza kutoka kwake, wangepata burudisho na kitulizo.

 “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo.” Wale ambao walipewa mwaliko huo na Yesu walikuwa ‘wamelemewa na mizigo’ ya sheria na tamaduni za kibinadamu ambazo viongozi wao wa kidini waliwalazimisha kufuata. (Mathayo 23:4; Marko 7:7) Watu wengi walikuwa na mahangaiko mengi na walitaabika kwa sababu walilazimika kufanya kazi ngumu kwa muda mrefu ili kupata riziki.

 “Nami nitawaburudisha.” Yesu aliahidi kuwapa kitulizo, au pumziko, wale ambao wangekubali mwaliko wake wenye upendo. Aliwaburudisha kwa kuwasaidia waelewe kile ambacho Mungu alitarajia wafanye. (Mathayo 7:24, 25) Kujua mambo hayo kungewaweka huru kutokana na utumwa wa mawazo ya uwongo na tamaduni za kidini zenye kukandamiza. (Yohana 8:31, 32) Hata ingawa kujifunza na kutenda kulingana na mafundisho ya Yesu kulihitaji jitihada, kufanya hivyo kuliburudisha.

 “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu.” Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida wafanyakazi walitumia nira—​ubao uliowekwa mabegani​—ili kubeba mizigo mizito. Basi, neno “nira” likawa na maana ya kuwa chini ya mamlaka au mwongozo wa mtu mwingine. (Mambo ya Walawi 26:13; Isaya 14:25; Yeremia 28:4) Maneno “mjifunze kutoka kwangu” yanaweza pia kumaanisha “kuwa wanafunzi wangu (wafuasi).” Kwa hiyo, Yesu aliwatia moyo wasikilizaji wake wawe wanafunzi wake kwa kumfuata na kuiga mfano wake.​—Yohana 13:13-15; 1 Petro 2:21.

 “Nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.” Yesu hakuahidi kwamba matatizo yote yangeisha mara moja. Hata hivyo, aliwasaidia wasikilizaji wake kupata faraja na tumaini. (Mathayo 6:25-32; 10:29-31) Wale ambao walikubali mafundisho yake na kuwa wanafunzi wake walitambua kwamba kumtumikia Mungu si mzigo, bali kufanya hivyo kuliwaletea uradhi wa kweli.​—1 Yohana 5:3.

 “Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” Tofauti na viongozi wa kidini wa siku zake, Yesu alikuwa mpole na mnyenyekevu. (Yohana 7:47-49) Hakuwa mkali na hakuwakandamiza watu. Badala yake, alikuwa mwenye fadhili na mwenye kufikika kwa urahisi. Alikuwa mwenye usawaziko na ufikirio na hakutarajia wafuasi wake wafanye zaidi ya uwezo wao. (Mathayo 7:12; Marko 6:34; Luka 9:11) Aliwaonyesha wafuasi wake jinsi ambavyo wangeweza kufaidika kutokana na rehema ya Mungu na kufurahia burudisho linalotokana na kuwa na dhamiri safi. (Mathayo 5:23, 24; 6:14) Yesu alikuwa na sifa nzuri ambazo ziliwavuta watu kwake na pia kuwachochea kukubali nira yake yenye fadhili na kuwa wanafunzi wake.

Muktadha wa Mathayo 11:28-30

 Yesu alisema maneno yaliyorekodiwa kwenye Mathayo 11:28-30 alipokuwa kwenye kampeni ya kuhubiri kule Galilaya katika mwaka wa 31 W.K. Mtume Mathayo ndiye mwandikaji pekee wa Injili aliyeandika kuhusu mwaliko wa Yesu wenye fadhili. Mathayo, Myahudi ambaye hapo awali alikuwa mkusanya-kodi, alikuwa amejionea jinsi watu wa kawaida walivyokandamizwa na kodi za Waroma na pia mfumo wa kidini wa Kiyahudi uliokuwa umepotoka. Basi, bila shaka alitiwa moyo alipoona Yesu akitumia mamlaka aliyopewa na Yehova a, Baba yake, kuwaalika wanyenyekevu na waliokandamizwa waje kwake.​—Mathayo 11:25-27.

 Injili ya Mathayo inaonyesha sifa zenye kutokeza ambazo Yesu alionyesha akiwa Masihi aliyeahidiwa na mtawala wa wakati ujao wa Ufalme wa Mungu.​—Mathayo 1:20-23; Isaya 11:1-5.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha Mathayo.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?