Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Mhubiri 3:11—“Amefanya Kila Kitu Kipendeze kwa Wakati Wake”

Mhubiri 3:11—“Amefanya Kila Kitu Kipendeze kwa Wakati Wake”

 “Amefanya kila kitu kipendeze kwa wakati wake. Hata ameweka umilele katika moyo wao; lakini bado wanadamu hawatajua kamwe kazi ambayo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”​—Mhubiri 3:11. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya tangu mwanzo hata mwisho.”​—Mhubiri 3:11, Union Version.

Maana ya Mhubiri 3:11

 “Amefanya kila kitu kipendeze kwa wakati wake.” Neno la Kiebrania lililotafsiriwa kuwa ‘pendeza’ halimaanishi tu uzuri wa nje au kitu kinachovutia. Linaweza pia kutafsiriwa ‘kuwa na mpangilio mzuri’ au ‘kufaa.’ (Mhubiri 3:11, maelezo ya chini) Kazi za Mungu zinazopendeza zinatia ndani uumbaji wake na pia mambo yote anayofanya ili kutimiza mapenzi yake.​—Danieli 2:21; 2 Petro 3:8; Ufunuo 4:11.

 “Hata ameweka umilele katika moyo wao.” Mungu aliwaumba wanadamu ili waishi milele. (Zaburi 37:29) Kwa sababu hiyo, aliwapa pia tamaa ya kuishi milele. Hata hivyo, wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa walikataa kumtii Mungu na wakajiletea kifo wao wenyewe na pia wazao wao. (Mwanzo 3:17-19; Waroma 5:12) Licha ya hayo, Mungu anaahidi “kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai” kutia ndani tamaa ya mwanadamu ya kuishi milele. (Zaburi 145:16) Biblia inafunua hatua ambazo Yehova a amechukua ili kuwapa tena wanadamu tumaini la kuishi milele.​—Waroma 6:23.

 “Wanadamu hawatajua kamwe kazi ambayo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” Hekima ya Mungu ni nyingi sana na yenye kina hivi kwamba Biblia inasema ‘haitafutiki.’ (Waroma 11:33) Hata hivyo, Mungu yuko tayari kufunua makusudi yake kwa wale wanaotaka kumpendeza.​—Amosi 3:7.

Muktadha wa Mhubiri 3:11

 Kitabu cha Mhubiri kiliandikwa na Mfalme Sulemani wa Israeli la kale, mwanamume aliyekuwa maarufu kwa sababu ya hekima ambayo Mungu alikuwa amempa. Kitabu hicho kina ushauri mzuri kuhusu mambo ambayo kwa kweli ni muhimu maishani na mambo yasiyo na thamani. (Mhubiri 1:2, 3; 2:1, 17; 7:1; 12:1, 13) Katika Sura ya 3, Sulemani anazungumzia baadhi ya mambo ambayo yanatukia maishani mwa mwanadamu tena na tena. Anataja kazi na utendaji mbalimbali. (Mhubiri 3:1-8, 10) Mungu amewapa wanadamu uhuru wa kuchagua utendaji ambao wangependa kufanya na wakati ambapo wangependa kuufanya. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Yoshua 24:15) Sulemani anafafanua kwamba wanadamu wanaposhirikiana na kusudi la Mungu na kuheshimu “wakati uliowekwa” na Mungu—ratiba ya Mungu—ndipo tu wanapoweza kufurahia kikweli matokeo ya kazi yao ngumu. Sulemani anaiita furaha hiyo “zawadi kutoka kwa Mungu.”​—Mhubiri 3:1, 12, 13.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Mhubiri.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?”