Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA HISTORIA

Aristoto

Aristoto

ZAIDI ya miaka 2,300 iliyopita, Aristoto alichangia sehemu kubwa sana katika elimu ya sayansi na falsafa. Mawazo na ugunduzi wake umewachochea watu na maandishi yake yametafsiriwa na kusomwa na watu wengi sana. Profesa wa historia James MacLachlan aliandika hivi: “Maoni ya Aristoto kuhusu ulimwengu wa asili yalitawala katika fikira za watu wa Ulaya kwa miaka 2,000 hivi.” Baadhi ya maoni ya Aristoto yaliathiri mafundisho ya Wakatoliki, Waprotestanti na vilevile Waislamu.

Alipenda Mambo Mengi

Aristoto aliandika kuhusu sanaa, nyota, biolojia, maadili, lugha, sheria, hoja muhimu, nguvu za uvutano, metafizikia, mwendo, starehe, ushairi, siasa, saikolojia, ufasaha wa kusema, na uhai, ambao aliamini kwamba unaweza kufa. Hata hivyo, amekuwa mashuhuri katika nyanja ya biolojia na hoja muhimu.

Wasomi wa kale Wagiriki walitegemea uwezo wao wa kuona, mkataa, na hoja za msingi ili kufafanua ulimwengu wa asili. Kwanza, walifikiria mambo ambayo kwa wazi ni kweli, waliamini kwamba ikiwa watatafakari kwa kina kweli hizo, wataweza kufikia mikataa iliyo sahihi.

Kwa kutegemea falsafa hiyo, walifikia mikataa mingi iliyo sahihi, mkataa mmoja ni kwamba kuna sheria za msingi katika ulimwengu. Hata hivyo, tatizo kubwa ni kwamba kulikuwa na mipaka ya vitu ambavyo wangeweza kuona kwa macho, hilo lilifanya watu wengi mashuhuri kutia ndani Aristoto kukosea. Kwa mfano, waliamini kwamba nyota na sayari ziliizunguka dunia. Wakati huo, hilo lilionekana kuwa kweli. Kitabu The Closing of the Western Mind kinaeleza hivi: “Hoja na mambo waliyojionea yaliunga mkono maoni ya Wagiriki kwamba dunia ni kitovu cha ulimwengu.”

Imani ya kwamba dunia ni kitovu cha ulimwengu ilikuwa na madhara makubwa katika historia, kwa sababu Kanisa Katoliki liliunga mkono fundisho hilo.

Wakatoliki Wakubali Maoni ya Aristoto

Zamani “Wakristo” huko Ulaya, walifuata baadhi ya mafundisho ya Aristoto, yaani, waliyakubali kuwa mafundisho ya kweli. Mwanatheolojia mashuhuri wa Roma Katoliki, Thomas Aquinas (c. 1224-1274) alitumia maandishi ya Aristoto katika theolojia. Hivyo, maoni ya Aristoto kwamba dunia ni kitovu cha ulimwengu yakatiwa ndani ya imani ya kanisa Katoliki. Fundisho hilo lilikubaliwa pia na viongozi wa kanisa la Protestanti, kama vile Calvin na Luther, ambao walidai kwamba hilo ni fundisho la Biblia.—Ona sanduku “ Hawakuelewa Vizuri Biblia.”

Baadhi ya mafundisho ya Aristoto yalikubaliwa kuwa kweli

Mwandishi Charles Freeman alisema hivi “Katika maeneo fulani [mafundisho ya Aristoto] na Mafundisho ya Katoliki hayangeweza kutofautishwa.” Hivyo, ilisemwa kwamba Aquinas “alimbatiza” Aristoto katika imani ya Katoliki. Freeman aliongezea kwamba kihalisi, “Aquinas ndiye alikuwa mfuasi wa mafundisho ya Aristoto.” Na kwa kiasi fulani, tunaweza kuongezea kwamba kanisa lilifuata mafundisho hayo. Matokeo ni kwamba, Galileo, mtaalamu wa nyota na hisabati wa Italia, ambaye alitoa ushahidi kwamba dunia ndiyo inayozunguka jua, alihitajiwa kwenda katika mahakama ya wazushi na alilazimishwa kuacha maoni yake. * Kwa wazi, Aristoto alitambua kwamba elimu ya sayansi inasonga, na mambo yanaweza kueleweka upya. Laiti kama kanisa lingekuwa na mtazamo huo pia!

^ fu. 11 Ili kupata habari zaidi kuhusu Galileo soma makala ya Amkeni! la Aprili 22, 2003 yenye kichwa “Mgogoro Kati ya Galileo na Kanisa,”