Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 5

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 5

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 5

Ugiriki na Historia ya Biblia

Hii ni habari ya tano katika mfululizo wenye habari saba katika matoleo ya “Amkeni!” yenye kufuatana yanayozungumzia serikali saba kuu za ulimwengu zinazotajwa katika historia ya Biblia. Kusudi lake ni kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na ujumbe wake unatoa tumaini kwamba mateso yanayosababishwa na utawala mkatili wa wanadamu yatakwisha.

KATIKA karne ya nne K.W.K., kijana Mmakedonia anayeitwa Aleksanda alifanya Ugiriki * kuwa sehemu muhimu ya historia ya ulimwengu. Kwa kweli, alifanya Ugiriki iwe serikali ya tano kuu ya ulimwengu katika historia ya Biblia na hivyo akaja kuitwa Aleksanda Mkuu. Milki zilizotangulia zilikuwa Misri, Ashuru, Babiloni, na Muungano wa Umedi na Uajemi.

Baada ya kifo cha Aleksanda, milki yake iligawanyika na kuacha kuwa yenye nguvu. Hata hivyo, utamaduni, lugha, dini, na falsafa za Ugiriki ziliendelea kuwa na uvutano muda mrefu baada ya milki hiyo ya kisiasa kukoma.

Historia Inayotegemeka

Biblia haitaji manabii wowote wa Mungu waliotabiri wakati wa utawala wa Ugiriki, wala hakuna vitabu vyovyote vya Biblia vilivyoongozwa kwa roho ya Mungu vilivyoandikwa wakati huo. Hata hivyo, Ugiriki inatajwa katika unabii wa Biblia. Kwa kuongezea, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanayojulikana kama Agano Jipya, mara nyingi yanataja uvutano wa Ugiriki. Hasa katika Israeli, kulikuwa na majiji kumi ya Kigiriki yaliyoitwa Dekapoli, kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “majiji kumi.” (Mathayo 4:25; Marko 5:20; 7:31) Biblia inataja eneo hilo mara kadhaa, na vitabu vya historia na magofu ya majumba ya maonyesho, viwanja vya michezo, mahekalu, na mabafu zinathibitisha kwamba eneo hilo lilikuwepo.

Biblia pia inataja utamaduni na dini ya Kigiriki, hasa katika kitabu cha Matendo, ambacho kiliandikwa na daktari Luka. Ona mifano michache ifuatayo:

Ikieleza matukio yaliyotukia wakati wa ziara ya mtume Paulo huko Athene katika mwaka wa 50 W.K., Biblia inasema kwamba jiji hilo lilikuwa “limejaa sanamu.” (Matendo 17:16) Historia inathibitisha kwamba Athene na viunga vyake vilikuwa vimejaa sanamu na vihekalu vya kidini.

Matendo 17:21 inasema kwamba “Waathene wote na wageni waliokuwa wakikaa huko kwa muda hawakuwa wakitumia wakati wao wa starehe wakifanya chochote ila kuambiana jambo au kusikiliza jambo jipya.” Maandishi ya Thucydides na Demosthenes yanathibitisha kwamba Waathene walipenda kujihusisha katika mazungumzo na mabishano.

Biblia inasema waziwazi kwamba “Waepikurea na wanafalsafa Wastoa pia wakawa wanaongea [na Paulo] kwa mabishano,” na hata wakampeleka kwenye Areopago ili wasikilize zaidi mambo aliyokuwa akisema. (Matendo 17:18, 19) Jiji la Athene lilijulikana kuwa na wanafalsafa wengi, kutia ndani Waepikurea na Wastoa.

Paulo anataja madhabahu ya Athene iliyokuwa imeandikwa “Kwa Mungu Asiyejulikana.” (Matendo 17:23) Huenda madhabahu yaliyokuwa yamewekwa wakfu kwa mungu asiyejulikana yalijengwa na Epimenide wa Krete.

Alipokuwa akiwahutubia Waathene, Paulo alitaja maneno, “kwa maana sisi pia ni uzao wake,” akisema kwamba maneno hayo si ya mshairi mmoja, bali ni ya “watu fulani ambao ni washairi kati yenu.” (Matendo 17:28) Washairi hao Wagiriki walikuwa Arato na Kleanthe.

Maneno hayo ya Paulo yalimfanya msomi mmoja afikie mkataa huu: “Kwa maoni yangu, simulizi la ziara ya Paulo huko Athene limeandikwa na mtu aliyekuwako huko na kujionea mwenyewe mambo yaliyoandikwa.” Mkataa huo unaweza pia kufikiwa kuhusu yale ambayo Biblia inasema yalimpata Paulo huko Efeso ya Asia Ndogo. Katika karne ya kwanza W.K., jiji hilo bado lilishikilia sana dini ya kipagani ya Kigiriki, hasa ibada ya mungu wa kike Artemi.

Hekalu la Artemi ambalo ni mojawapo ya maajabu saba ya ulimwengu wa kale, linatajwa mara kadhaa katika kitabu cha Matendo. Kwa mfano, tunaambiwa kwamba huduma ya Paulo huko Efeso ilimkasirisha mtu fulani anayeitwa Demetrio, fundi wa fedha, aliyekuwa na biashara ya kutengeneza vihekalu vya fedha vya Artemi iliyomletea pesa nyingi. “Paulo huyu,” akasema Demetrio kwa hasira, “ameshawishi umati mkubwa na kuwageuza kwenye kauli nyingine, akisema kwamba wale waliofanywa kwa mikono si miungu.” (Matendo 19:23-28) Kisha Demetrio akachochea umati wenye hasira ambao ulianza kupaaza sauti na kusema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”

Leo unaweza kutembelea magofu ya Efeso na mahali ambapo hekalu la Artemi lilikuwa. Isitoshe, maandishi ya kale kutoka Efeso yanathibitisha kwamba sanamu zilitengenezwa ili kumtukuza mungu huyo wa kike na kwamba kulikuwa na kikundi cha mafundi wa fedha katika jiji hilo.

Unabii Unaotegemeka

Miaka 200 hivi kabla ya wakati wa Aleksanda Mkuu, Danieli, nabii wa Yehova Mungu aliandika kuhusu utawala huo wa ulimwengu: “Tazama! kulikuwa na mbuzi-dume akija kutoka upande wa magharibi akiwa juu ya uso wa dunia yote, naye hakuwa akigusa nchi. Huyo mbuzi-dume alikuwa na pembe yenye kuonekana wazi kati ya macho yake. Akaja mpaka akamfikia yule kondoo-dume mwenye zile pembe mbili, . . . akaja akikimbia kumwelekea akiwa na ghadhabu yake yenye nguvu. Naye . . . akampiga na kumwangusha yule kondoo-dume, akazivunja zile pembe zake mbili, na huyo kondoo-dume hakuwa na nguvu za kusimama mbele yake. Basi akamwangusha katika nchi na kumkanyagia chini . . . Ndipo yule mbuzi-dume akajivuna mno; lakini mara alipokuwa na nguvu, ile pembe kubwa ikavunjwa, na badala yake kukatokea pembe nne zenye kuonekana wazi, kuelekea zile pepo nne za mbingu.”—Danieli 8:5-8.

Maneno hayo yalimhusu nani? Danieli mwenyewe anajibu: “Yule kondoo-dume uliyemwona mwenye pembe mbili anawakilisha wafalme wa Umedi na Uajemi. Na yule mbuzi-dume mwenye manyoya anawakilisha mfalme wa Ugiriki; na ile pembe kubwa iliyokuwa kati ya macho yake, inawakilisha mfalme wa kwanza.”—Danieli 8:20-22.

Hebu fikiria kuhusu jambo hilo! Babiloni ilipokuwa bado ndiyo serikali kuu ya ulimwengu, Biblia ilitabiri kwamba serikali kuu ambazo zingefuata zingekuwa Muungano wa Umedi na Uajemi na Ugiriki. Isitoshe, kama ilivyotajwa awali, Biblia ilisema waziwazi kwamba “mara alipokuwa na nguvu, ile pembe kubwa”—Aleksanda—‘ingevunjwa’ na mahali pake pangetokea pembe nyingine nne, na kuongezea kwamba hakuna hata moja ya pembe hizo ambayo ingekuwa uzao wa Aleksanda.—Danieli 11:4.

Habari zote katika unabii huo zilitimia. Aleksanda alikuwa mfalme katika mwaka wa 336 K.W.K., na katika muda wa miaka saba alimshinda Mfalme Dario wa Tatu, mtawala mwenye nguvu wa Uajemi. Baada ya hapo, Aleksanda aliendelea kupanua milki yake hadi alipokufa kifo cha mapema katika mwaka wa 323 K.W.K., akiwa na umri wa miaka 32. Hakuna mtawala mmoja hususa aliyechukua mahali pa Aleksanda, wala wazao wake hawakumrithi. Badala yake, majenerali wake wakuu wanne—Lisimako, Kasanda, Seleuko, na Ptolemy—“walijiweka kuwa wafalme” na kutawala milki hiyo, kinasema kitabu The Hellenistic Age.

Alipokuwa akipanua milki yake, Aleksanda pia alitimiza unabii mwingine wa Biblia. Kwa mfano, nabii Ezekieli na Zekaria, walioishi katika karne ya saba na ya sita K.W.K., walitabiri kuharibiwa kwa jiji la Tiro. (Ezekieli 26:3-5, 12; 27:32-36; Zekaria 9:3, 4) Ezekieli hata aliandika kwamba mawe yake na mavumbi yake yatawekwa “katikati ya maji.” Je, maneno hayo yalitimia?

Hebu fikiria kile ambacho majeshi ya Aleksanda yalifanya wakati yalipozingira Tiro mwaka wa 332 K.W.K. Walikwangua magofu ya jiji la bara la Tiro na kuyatupa baharini ili kutengeneza njia hadi kwenye jiji la kisiwani la Tiro. Mbinu hiyo ilifanikiwa, na Tiro likaanguka. “Unabii kuhusu Tiro, kutia ndani mambo madogo sana, ulitimizwa,” akasema mvumbuzi wa karne ya 19 wa eneo hilo. *

Tumaini Linalotegemeka

Ushindi wa Aleksanda haukuleta amani na usalama ulimwenguni. Baada ya kuchunguza kipindi cha utawala wa Ugiriki, msomi mmoja alisema hivi: “Hali za watu wa kawaida . . . hazikubadilika sana.” Hali zimekuwa hivyo katika historia yote, na jambo hilo linathibitisha tena maneno ya Biblia kwamba “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.

Hata hivyo, utawala mbaya hautaendelea milele, kwa kuwa Mungu amesimamisha serikali bora kuliko serikali yoyote ya kibinadamu. Serikali hiyo inayoitwa Ufalme wa Mungu, itachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu, na raia wake watafurahia amani na usalama wa kweli utakaodumu milele.—Isaya 25:6; 65:21, 22; Danieli 2:35, 44; Ufunuo 11:15.

Mfalme wa Ufalme wa Mungu si mwingine ila Yesu Kristo. Tofauti na watawala wa kibinadamu ambao wana pupa ya mamlaka na hawawajali watu wa kawaida, Yesu anachochewa na upendo wake kwa Mungu na wanadamu. Mtunga-zaburi alitabiri hivi kumhusu: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.”—Zaburi 72:12-14.

Je, ungependa Mtawala kama huyo? Ikiwa ndivyo, lingekuwa jambo la hekima ukichunguza serikali kuu ya sita ya ulimwengu katika historia ya Biblia—Roma. Kwa kweli, Mwokozi aliyetabiriwa alizaliwa wakati wa utawala wa Roma na aliacha kumbukumbu isiyoweza kufutika katika historia ya wanadamu. Tafadhali soma habari ya sita ya mfululizo huu itakayokuwa katika toleo linalofuata la gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mambo yanayotajwa katika habari hii kuhusu Ugiriki yanarejelea Ugiriki ya kale kabla ya karne ya kwanza na hayahusiani na mipaka ya kisasa ya kitaifa.

^ fu. 23 Kama ilivyotabiriwa na Ezekieli, Tiro lilishindwa kwa mara ya kwanza na Mfalme Nebukadreza wa Babiloni. (Ezekieli 26:7) Baadaye, jiji hilo lilijengwa upya. Jiji hilo lililojengwa upya ndilo lililoharibiwa na Aleksanda, na hivyo kutimiza maneno yote yaliyotabiriwa na manabii.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Biblia ilitabiri kwa usahihi ushindi wa Aleksanda Mkuu na kuvunjika kwa milki yake

[Ramani]

MILKI YA UGIRIKI

UGIRIKI

MISRI

UMEDI

UAJEMI

INDIA

[Ramani katika ukurasa wa 20]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Aleksanda alitimiza unabii wa Biblia alipotumia magofu ya jiji la zamani la bara la Tiro kujenga njia ya mawe hadi kwenye jiji la kisiwani

BARA

Njia ya mawe iliyojengwa na Aleksanda

TIRO

TIRO YA LEO

Eneo lililojazwa magofu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Miaka 200 hivi mapema, unabii wa Biblia ulitabiri kuhusu Aleksanda Mkuu

[Picha katika ukurasa wa 19]

Sanamu ya Artemi, mungu wa kike wa Efeso

[Picha katika ukurasa wa 19]

Madhabahu iliyowekwa wakfu kwa mungu asiyejulikana

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 17]

Top, time line: Egyptian wall relief and bust of Nero: Photograph taken by courtesy of the British Museum; Persian wall relief: Musée du Louvre, Paris; bottom, bust of Alexander the Great: Musée du Louvre, Paris