Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Wana Hasira Sana?

Kwa Nini Watu Wana Hasira Sana?

Kwa Nini Watu Wana Hasira Sana?

NI VIGUMU kueleza ni nini kinachosababisha hasira. Hata wanasayansi wanakubali kwamba hawaelewi visababishi vya hasira. Hata hivyo, wataalamu wa akili wanakubali kwamba kuna mambo fulani ambayo huchochea hasira.

Huenda jambo linaloudhi au kutamausha likachochea hasira. Kwa kawaida, mtu huudhika au kutamauka anapotendewa isivyo haki. Kutukanwa au kukosewa heshima kunaweza pia kumwudhi mtu. Pia, mtu anaweza kuwa na hasira anapoona jambo fulani kuwa tisho kwa mamlaka au sifa yake.

Bila shaka, watu hukasirishwa na mambo tofauti ikitegemea umri, jinsia, na hata utamaduni wao. Isitoshe, watu hutenda kwa njia tofauti-tofauti wanapopandwa na hasira. Watu fulani hawakasiriki upesi, nao husahau haraka wanapokosewa, lakini wengine hukasirika haraka na huenda wakaendelea kuwa na hasira kwa siku nyingi, majuma, miezi, au muda mrefu hata zaidi.

Tumezungukwa na mambo yanayoweza kuchochea hasira. Zaidi ya hilo, siku hizi watu wanachokozeka kwa urahisi zaidi. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kuna mtazamo wa ubinafsi wa “mimi kwanza” ambao umeenea katika siku zetu. Biblia inaeleza hivi: “Katika siku za mwisho . . . watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, . . . wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:1-5) Je, andiko hilo halifafanui kwa usahihi mtazamo wa watu wengi leo?

Kwa kweli, watu wenye ubinafsi wasipopata kile wanachotaka, mara nyingi wao hukasirika. Kuna sababu nyingine nyingi kwa nini mwelekeo wa watu kulipuka kwa hasira unaongezeka. Fikiria baadhi ya sababu hizo.

Kielelezo cha Wazazi

Wazazi wana uvutano mkubwa katika utu wa mtoto tangu utotoni hadi anapobalehe. Mwanasaikolojia Harry L. Mills anaeleza: “Tangu utotoni, watu hujifunza kuonyesha hasira kwa kuiga tabia ya kukasirika ya watu wanaowazunguka.”

Ikiwa mtoto analelewa katika mazingira yenye uhasama, yaani, mahali ambapo mambo madogo huwafanya watu walipuke kwa hasira, mtoto huyo anajifunza kwamba anapokabili matatizo maishani anapaswa kutenda kwa hasira. Unaweza kumfananisha mtoto huyo na mmea unaotiwa maji machafu. Huenda mmea huo ukakua, lakini ukakosa kukomaa inavyofaa, na unaweza kupata madhara ya kudumu. Vivyo hivyo, hasira ni kama maji machafu, na watoto waliolelewa katika mazingira yenye hasira wana mwelekeo wa kuwa na hasira wanapokuwa watu wazima.

Majiji Yaliyosongamana Watu

Katika mwaka wa 1800, asilimia 3 hivi ya watu ulimwenguni walikuwa wakiishi katika majiji. Katika mwaka wa 2008, idadi hiyo iliongezeka na kuwa asilimia 50, na kufikia mwaka wa 2050, idadi hiyo inatarajiwa kufikia asilimia 70. Kadiri watu wanavyozidi kufurika katika majiji yaliyosongamana, ndivyo inavyotazamiwa kwamba viwango vya hasira na kukata tamaa vitaongezeka. Kwa mfano, Mexico City ni moja kati ya majiji makubwa zaidi na yaliyo na watu wengi zaidi duniani. Msongamano wa magari ni kisababishi kikubwa cha mahangaiko. Mexico City lililo na watu milioni 18 hivi na magari milioni sita, “linaweza kusemwa kuwa ndilo jiji kuu lenye watu waliofadhaika zaidi ulimwenguni,” anasema mwandishi mmoja wa habari. “Kuna msongamano mkubwa wa magari, na hilo hufanya watu wachemke kwa hasira.”

Katika majiji yaliyosongamana watu kuna mambo mengine yanayosababisha mfadhaiko, kama vile uchafuzi wa hewa, kelele nyingi, ukosefu wa makazi, tofauti za kitamaduni, na kuongezeka kwa uhalifu. Kadiri visababishi hivyo vya mfadhaiko vinavyozidi kuongezeka, ndivyo na watu wanavyozidi kukata tamaa, kukasirika, na kukosa subira.

Kutamaushwa na Uchumi

Kuzorota kwa uchumi ulimwenguni pote kumefanya watu wafadhaike na washikwe na wasiwasi. Ripoti moja ya 2010 iliyotolewa na Shirika la Fedha Duniani (IMF) pamoja na Shirika la Umoja wa Mataifa la Wafanyakazi Ulimwenguni (ILO) inasema: “Inakadiriwa kwamba watu zaidi ya milioni 210 ulimwenguni pote hawana ajira.” Kwa kusikitisha, wengi wa walioachishwa kazi hawana pesa walizoweka akiba au njia nyingine ya kujikimu.

Wale walioajiriwa wana wasiwasi pia. Shirika la ILO linasema kwamba mfadhaiko unaotokana na kazi “ni tatizo lililoenea ulimwenguni pote.” Lorne Curtis, mshauri kuhusu mambo ya usimamizi huko Ontario, Kanada anasema, “Watu wana wasiwasi kuhusu kazi zao na hutarajia mabaya,” kisha anaendelea kusema kwamba kwa sababu hiyo, “wanajitetea na wana mwelekeo wa kubishana na wasimamizi wao au wafanyakazi wengine.”

Ubaguzi na Ukosefu wa Haki

Hebu wazia jinsi ambavyo ungehisi ikiwa ungeingia katika shindano la kukimbia na ugundue kwamba ni wewe tu unayekimbia ukiwa umefungwa minyororo miguuni. Mamilioni ya watu wanahisi hivyo wanapobaguliwa kwa sababu ya rangi yao au kwa sababu nyingine. Watu hukasirika wanapopata vizuizi vinavyowazuia wasipate kazi, elimu, makao, na mambo mengine ya lazima.

Ukosefu mwingine wa haki unaweza kumponda mtu roho na kusababisha maumivu makubwa ya kihisia. Kwa kusikitisha, sisi sote tumetendewa isivyo haki wakati mmoja. Zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Tazama! machozi ya wale wanaokandamizwa, lakini hawakuwa na mtu wa kuwafariji.” (Mhubiri 4:1) Mtu anaweza kupandwa na hasira kunapokuwa na ukosefu mwingi wa haki na hakuna faraja.

Ulimwengu wa Burudani

Utafiti mwingi sana umefanywa ili kuchunguza jinsi jeuri katika televisheni na vyombo vingine vya habari inavyowaathiri watoto. James P. Steyer, mwanzilishi wa shirika la Common Sense Media, ambalo hutoa habari kuhusu vyombo vya habari, anasema hivi: “Kizazi ambacho kimekua kikiona jeuri nyingi inayoonekana kuwa halisi hakishtuki watu wanapotenda kwa jeuri, ukatili, na bila huruma.”

Ni kweli kwamba vijana wengi ambao wamezoea kuona jeuri kwenye televisheni hawageuki na kuwa wahalifu sugu. Hata hivyo, mara nyingi ulimwengu wa burudani huonyesha kwamba hasira inayoonyeshwa kwa jeuri ni njia inayofaa ya kukabiliana na matatizo, na hilo hutokeza kizazi ambacho hakina hisia zozote kuhusu jeuri.

Uvutano wa Roho Waovu

Biblia inafunua kwamba nguvu fulani isiyoonekana ndiyo chanzo cha hasira ambayo watu wanaonyesha leo. Jinsi gani? Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, kiumbe fulani wa roho alimwasi Mungu Mweza-Yote. Kiumbe huyo mwovu wa roho anaitwa Shetani, jina ambalo linamaanisha “Mpinzani,” au “Adui” katika Kiebrania. (Mwanzo 3:1-13) Baadaye, Shetani aliwachochea malaika wengine wajiunge naye katika uasi.

Malaika hao waasi ambao wanajulikana kama roho waovu wametupwa chini kwenye ujirani wa dunia. (Ufunuo 12:9, 10, 12) Isitoshe, wana “hasira kali,” kwa kuwa wanajua kwamba wana kipindi kifupi cha wakati. Kwa hiyo, hata ikiwa hatuwezi kuwaona roho hao waovu, tunaona matokeo ya utendaji wao. Jinsi gani?

Shetani na roho wake waovu wanatumia mwelekeo wetu wa kutenda dhambi ili kutushawishi tuwe na “uadui, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, magomvi, migawanyiko, . . . karamu za kupindukia, na mambo kama hayo.”—Wagalatia 5:19-21.

Pinga Kishawishi

Kwa kweli, tunapofikiria matatizo hayo yote, mikazo, na mahangaiko, tunaelewa kwa nini watu hukasirika wanapojaribu kutimiza majukumu yao ya kila siku.

Ni vigumu sana kwa mtu kujizuia asichemke kwa hasira! Makala inayofuata itatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kudhibiti hasira.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

UNA TATIZO KUBWA IKIWA . . .

▶ Wewe hukasirika unapolazimika kusubiri kwenye foleni dukani.

▶ Wewe hubishana mara nyingi na wafanyakazi wenzako.

▶ Mara kwa mara wewe hukesha ukifikiria mambo yaliyokukasirisha mchana.

▶ Ni vigumu kwako kusamehe waliokukosea.

▶ Mara nyingi huwezi kudhibiti hisia zako.

▶ Baada ya kulipuka kwa hasira mara nyingi unahisi aibu au unajuta. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 36 Habari zimetolewa katika Tovuti ya MentalHelp.net.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

TAKWIMU KUHUSU HASIRA

Shirika la Afya ya Akili la London, Uingereza, lilichapisha ripoti iliyokuwa na kichwa Boiling Point—Problem Anger and What We Can Do About It (Kuchemka kwa HasiraTatizo la Hasira na Jinsi Tunavyoweza Kukabiliana Nalo). Takwimu zifuatazo ni kati ya mambo makuu yaliyotokezwa na ripoti hiyo:

Asilimia 84 wanahisi wamefadhaika kazini kuliko ilivyokuwa miaka mitano iliyopita.

Asilimia 65 wamefoka kwa hasira kazini au wamewaona wengine wakifoka.

Asilimia 45 ya wafanyakazi hulipuka kwa hasira mara kwa mara kazini.

Asilimia 60 hivi hukosa kwenda kazini kwa sababu ya mfadhaiko.

Asilimia 33 ya Waingereza wamewakasirikia jirani zao hivi kwamba hawazungumzi nao.

Asilimia 64 wanakubali kwamba watu kwa ujumla wamekuwa wenye hasira sana.

Asilimia 32 wanasema kwamba wana rafiki wa karibu au mtu wa familia ambaye hushindwa kudhibiti hasira.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Milipuko yako ya hasira inaweza kuwaathirije watoto wako?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, ulimwengu wa burudani unaathiri maoni yako kuhusu hasira na jeuri?