Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Visababishi vya Ukosefu wa Haki

Visababishi vya Ukosefu wa Haki

Visababishi vya Ukosefu wa Haki

KARIBU miaka elfu mbili iliyopita, Biblia ilifafanua kwa usahihi tabia ya watu katika siku zetu. Ilisema: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, . . . wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-4.

Watu wengi watakubali kwamba mambo hayo yasiyofaa yameenea sana katika siku zetu. Yanaonekana kupitia njia mbalimbali kama vile, pupa, ubaguzi, mielekeo ya uhasama dhidi ya jamii, ufisadi, na ukosefu mkubwa sana wa usawa wa kiuchumi. Hebu tuzungumzie kila moja ya mambo hayo.

PUPA. Imesemekana kwamba “Pupa ina faida” na “Pupa ni nzuri.” Lakini maneno hayo si kweli. Pupa huumiza! Kwa mfano, mara nyingi pupa ndiyo huchochea ulaghai, miradi ya kuwekeza yenye udanganyifu, na kukopa au kukopesha pesa bila kuwajibika. Matokeo kama vile kuporomoka kwa uchumi yamewaumiza watu wengi. Ni kweli kwamba baadhi ya watu wanaopatwa na matokeo hayo mabaya mara nyingi wana pupa. Hata hivyo, baadhi ya waathiriwa ni watu wa kawaida wanaofanya kazi kwa bidii ili kujiruzuku na wamepoteza nyumba zao na malipo yao ya uzeeni.

UBAGUZI. Watu wenye ubaguzi huwahukumu wengine isivyo haki na hata kuwabagua kwa sababu ya kabila, rangi, jinsia, hali yao ya kiuchumi, au hata dini yao. Kwa mfano, kamati moja ya Umoja wa Mataifa iligundua kwamba katika nchi moja huko Amerika Kusini, mwanamke mmoja mja-mzito alikufa katika hospitali kwa kuwa alikuwa amebaguliwa katika kituo kingine cha afya kwa sababu ya kabila lake na pia alikuwa maskini. Ubaguzi umesababisha matendo mabaya ya ukosefu mkubwa sana wa haki kama vile kuangamizwa kwa makabila na jamii nzimanzima.

MIELEKEO YA UHASAMA DHIDI YA JAMII. Muhtasari wa kitabu Handbook of Antisocial Behavior unasema hivi: “Kila mwaka makumi ya maelfu ya familia hutenganishwa, maisha ya mamia ya maelfu ya watu huharibiwa, na mali yenye thamani ya mamilioni ya dola huharibiwa kwa sababu ya mwelekeo wa uhasama dhidi ya jamii. Jeuri na chuki zimeenea sana katika jamii yetu hivi kwamba huenda wanahistoria wa wakati ujao hawatafafanua siku zetu kuwa ‘Enzi ya Uvumbuzi wa Mambo ya Angani’ au ‘Enzi ya Usambazaji wa Habari’ bali wataifafanua kuwa ‘Enzi ya Uhasama Dhidi ya Jamii’—wakati ambapo jamii ilijipiga vita yenyewe.” Tangu kitabu hicho kichapishwe katika mwaka wa 1997, watu hawajabadili mielekeo na tabia zao.

UFISADI. Ripoti moja kuhusu ufisadi huko Afrika Kusini ilisema kwamba katika kipindi cha miaka saba, zaidi ya asilimia 81 ya randi 25.2 (dola bilioni 4 za Marekani) wakati huo, ambazo zilikuwa zimepewa idara ya afya ya mkoa mmoja zilitumiwa vibaya. Pesa “ambazo zilipaswa kutumiwa kudumisha hospitali, kliniki, na vituo vya afya katika mkoa huo,” hazikuwa zimetumiwa, linasema jarida The Public Manager.

UKOSEFU MKUBWA SANA WA USAWA WA KIUCHUMI. Ripoti moja katika gazeti Time inasema kwamba katika mwaka wa 2005, “ni asilimia 5 tu ya watu wanaopata mapato ya juu zaidi” waliofaidika kutokana na asilimia 30 hivi ya mapato ya mwaka mzima ya Uingereza. Na huko Marekani, “ni asilimia 5 tu ya watu wanaopata mapato ya juu zaidi wanaofaidika kutokana na zaidi ya asilimia 33 ya mapato ya Marekani,” linasema gazeti Time. Ulimwenguni pote, karibu watu bilioni 1.4 wanapata dola 1.25 (za Marekani) au chini kwa siku, na watoto 25,000 hufa kila siku kwa sababu ya umaskini.

Je, Kuna Suluhisho kwa Ukosefu wa Haki?

Mnamo 1987, aliyekuwa waziri mkuu wa Australia wakati huo aliweka lengo kwamba kufikia mwaka wa 1990 hakuna mtoto nchini Australia atakayeishi chini ya hali za umaskini. Lengo hilo halikuwahi kufikiwa. Kwa kweli, waziri huyo mkuu baadaye alijuta kwamba alikuwa ameweka lengo hilo.

Hata mtu awe na mamlaka, utajiri, au uvutano wa aina gani, yeye bado ni mwanadamu na hawezi kuondoa ukosefu wa haki. Kwa kweli, hata watu wenye mamlaka hupatwa na ukosefu wa haki, huzeeka, na kufa. Mambo hayo halisi hutukumbusha maandiko haya mawili ya Biblia:

“Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”Yeremia 10:23.

‘Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, ambao hawana wokovu wowote.’Zaburi 146:3.

Tukitambua ukweli wa maneno hayo, hatutakatishwa tamaa jitihada za wanadamu zinapokosa kufanikiwa. Kwa hiyo, je, hilo linamaanisha kuwa tunapaswa kukata tamaa kwamba hakuna suluhisho la ukosefu wa haki? La! Kama tutakavyoona katika makala ya mwisho ya mfululizo huu, ulimwengu ulio na haki ya kweli uko karibu sana. Kwa sasa, tunaweza kufanya jambo fulani. Tunaweza kuchunguza mawazo na matendo yetu. Jiulize: ‘Je, ninaweza kuwatendea wengine kwa haki zaidi? Je, kuna sehemu ninazopaswa kufanyia maendeleo?’ Maswali hayo yanajibiwa katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

A. Polisi nchini China wakimkamata mtu aliyehusika katika jeuri dhidi ya watu wa jamii nyingine

B. Uporaji na uharibifu wa mali huko London, Uingereza

C. Umaskini mbaya sana katika kambi moja ya wakimbizi huko Rwanda

[Hisani]

Top left: © Adam Dean/Panos Pictures; top center: © Matthew Aslett/Demotix/CORBIS; top right: © David Turnley/CORBIS