Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Weka Mipaka Iliyo Wazi

Weka Mipaka Iliyo Wazi

“Kulea watoto ukiwa peke yako si jambo rahisi​—hasa wanapofikia umri wa kubalehe na kutaka kuasi wazazi wao kama vijana wengine wengi.”​—DULCE, AFRIKA KUSINI.

Tatizo.

Biblia ilitabiri kwamba “katika siku za mwisho,” watoto kwa ujumla wangekuwa “wasiotii wazazi.”​—2 Timotheo 3:1, 2.

Mapendekezo.

Tambua kwamba “ili wakue vizuri, watoto wanahitaji kujua sheria na matarajio ya wazazi.” (The Single Parent Resource, cha Brook Noel) Barry G. Ginsberg ambaye ni mwanasaikolojia wa watoto na familia anasema hivi: “Mahusiano huwa mazuri na yasiyo na mkazo kunapokuwa na mipaka iliyo wazi.” Aliongezea hivi: “Mipaka hiyo inapokuwa ya wazi na inapoeleweka vizuri, inakuwa rahisi kufanya familia iwe na furaha.” Unaweza kuwekaje mipaka iliyo wazi?

Uwe thabiti. Uchunguzi mmoja uliofanywa nchini Australia ulionyesha kwamba watoto huwa watundu wazazi wao wanaposhindwa kuwakataza jambo fulani na wanapowaruhusu wafanye watakavyo. Kama Biblia inavyosema: “Mvulana [au msichana] aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.”​—Methali 29:15.

Usiache hisia za hatia kuhusu hali yako ukiwa mzazi mmoja zikufanye uwaendekeze watoto wako. Yasmin, aliyenukuliwa hapo awali anasema: “Nyakati nyingine, mimi huanza kuwahurumia wana wangu wawili kwa sababu wanalelewa na mzazi mmoja.” Lakini kama tutakavyoona, hakuruhusu hisia hizo, ambazo hazikuwa na ubaya wowote, zimfanye abatilishe uamuzi wake.

Usibadili-badili sheria, na usiwe kigeugeu. (Mathayo 5:37) “Watoto wanapojua kwamba bila shaka watatiwa nidhamu kwa sababu ya tabia fulani isiyofaa, hilo litawazuia wasiwe na matatizo ya kihisia na tabia zisizofaa,” linasema jarida American Journal of Orthopsychiatry. Yasmin anasema: “Niliketi pamoja na wavulana wangu na tukazungumza kuhusu nidhamu. Wakifanya makosa, ninajaribu kutoa nidhamu bila kubadilika-badilika. Hata hivyo, nimejifunza kwanza kuwasikiliza na kisha kuwaeleza kwa utulivu jinsi ambavyo jambo walilofanya limeathiri familia yetu. Baada ya kufanya hivyo, mimi hutoa nidhamu kama nilivyosema.”

Uwe na usawaziko; usitoe nidhamu ukiwa na hasira. Ingawa unahitaji kuwa thabiti kwa lililo sawa, unahitaji pia kubadilikana kulingana na hali inapohitajika. “Hekima inayotoka juu”​—yaani, kutoka kwa Mungu—​ni “yenye usawaziko,” linasema andiko la Yakobo 3:17. Watu wenye usawaziko hawafanyi mambo bila kufikiri au kwa hasira. Wala hawashikilii sheria kupita kiasi. Badala yake, wao hufikiri kwanza, huenda hata wakasali kuhusu jambo hilo, kisha wanaweza kutenda kwa utulivu na kwa njia inayofaa.

Kutobadili-badili sheria, kuwa thabiti, na kuwa na usawaziko, pamoja na kuweka mfano mzuri, kutakusaidia kuweka mipaka ambayo itafanya nyumba yako iwe kimbilio la kweli kwa ajili ya watoto wako.