Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Je, Unaweza Kuamini Ripoti za Habari?

Je, Unaweza Kuamini Ripoti za Habari?

WATU wengi hutilia shaka kile wanachosoma na kusikia katika vyombo vya habari. Kwa mfano, katika mwaka wa 2012 watu nchini Marekani waliulizwa ikiwa wanaweza “kuamini na kuwa na uhakika” kwamba habari zilizo kwenye magazeti, televisheni, na redio ni sahihi, kamili, na hazina ubaguzi. Watu 6 kati ya 10 walisema kwamba ama “hawaziamini sana” au “hawaziamini hata kidogo.” Je, shaka zao zina msingi?

Waandishi wengi wa habari na mashirika yaliyowaajiri wanasema kwamba wajibu wao ni kutoa ripoti sahihi. Hata hivyo, kuna sababu nzuri za kuhangaikia jambo hilo. Hebu fikiria mambo yafuatayo:

  • WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI. Mashirika machache lakini yenye uvutano mkubwa ndiyo yanayomiliki vyombo vya habari. Mashirika hayo ndiyo yanayoamua ni habari gani zitakazotolewa, jinsi zitakavyotolewa, na zitapewa umuhimu gani. Kwa sababu mashirika mengi yanataka tu kujipatia faida, huenda vyombo vya habari vikafanya maamuzi kwa kutegemea faida za kifedha. Ikiwa habari fulani itafanya wamiliki wa vyombo vya habari wakose faida, huenda isiripotiwe.

  • SERIKALI. Habari nyingi tunazosikia kwenye vyombo vya habari zinahusu wanasiasa na serikali. Serikali inataka kuwashawishi watu waunge mkono sera zao na maofisa wao. Na kwa sababu vyombo vya habari hupata habari kutoka kwa serikali, nyakati nyingine waandishi wa habari na maofisa wa serikali hushirikiana.

  •  MATANGAZO YA BIASHARA. Katika nchi nyingi, mashirika ya habari huhitaji pesa za kuendeleza biashara yao, na mara nyingi mapato hayo hutoka kwa matangazo ya biashara. Nchini Marekani, magazeti hupata mapato ya kati ya asilimia 50 na 60 kutoka kwa matangazo ya biashara, magazeti ya habari hupata asilimia 80, na vituo vya kibinafsi vya televisheni na redio hupata mapato yake yote kutoka kwa matangazo ya biashara. Kwa sababu hiyo, inaeleweka ni kwa nini mashirika ya matangazo ya biashara hayataki kudhamini programu ambazo zitafanya watu wawe na maoni mabaya kuhusu bidhaa zao au kuhusu shirika lao. Ikiwa hawafurahii habari zinazotolewa na shirika fulani la habari, basi watatumia shirika lingine la habari kutangaza bidhaa zao. Jambo hilo linaweza kuwafanya wahariri wa habari wazuie kutolewa kwa habari ambazo zinaonyesha mambo yasiyofaa kuhusu wadhamini wao.

  • UKOSEFU WA UNYOOFU. Waandishi fulani wa habari si wanyoofu. Wengine hutunga habari. Kwa mfano, miaka michache iliyopita, ripota mmoja nchini Japani alitaka kuandika kuhusu jinsi wapiga-mbizi walivyokuwa wakiharibu matumbawe huko Okinawa. Kwa kuwa hakupata tumbawe lolote lililoharibiwa, aliharibu matumbawe fulani kisha akayapiga picha. Pia, huenda picha zikabadilishwa ili kuwadanganya watu. Teknolojia ya kubadili picha imekuwa ya hali ya juu hivi kwamba ni vigumu kujua ikiwa picha fulani imebadilishwa.

  • MAPENDEZI YA MWANDISHI WA HABARI. Hata ikiwa mwandishi wa habari ana mambo yote hakika, anaweza kuripoti kulingana na mapendezi yake. Ni mambo gani yanayopaswa kuripotiwa, na ni gani hayapaswi? Kwa mfano, huenda timu ya kandanda ikashindwa kwa mabao mawili. Hilo ni jambo hakika. Lakini mwandishi wa habari anaweza kutoa sababu nyingi sana kwa nini timu hiyo ilishindwa.

  • KUTOANDIKA HABARI FULANI. Wanapopanga mambo hakika ili kutokeza habari yenye kuchochea, mara nyingi waandishi hawataji habari ambazo hazitaeleweka kwa urahisi au ambazo hazijakamilika. Jambo hilo hufanya habari fulani zitiliwe chumvi na nyingine zipunguzwe uzito. Kwa kuwa huenda watangazaji wa televisheni na maripota wakawa na dakika moja hivi ya kusimulia habari muhimu sana, huenda wasitaje mambo fulani muhimu.

  •  MASHINDANO. Katika miaka ya hivi karibuni, idadi ya vituo vya televisheni imeongezeka na muda ambao watazamaji wanatumia kutazama kituo kimoja tu umepungua sana. Ili kuwavutia watazamaji, vituo vya televisheni vimelazimika kutoa habari za pekee au zile zitakazowafurahisha watazamaji. Kitabu Media Bias (Ubaguzi wa Vyombo vya Habari) kinasema hivi kuhusu jambo hilo: “Habari [kwenye televisheni] sasa zimejaa tu picha, nyingine zenye kushtua na nyingine zenye kusisimua, na habari zimefupishwa ili kuwafaa watazamaji ambao hawawezi kukaza fikira kwa muda mrefu.”

  • MAKOSA. Kwa sababu waandishi wa habari si wakamilifu, wao hufanya makosa bila kukusudia. Maana ya sentensi inaweza kupotoshwa kwa kukosea herufi moja, kuweka alama ya mkato mahali pasipofaa, au kosa la kisarufi. Huenda mambo hakika yakakosa kuchunguzwa kwa makini. Pia huenda mwandishi wa habari ambaye anaharakisha kumaliza kazi kabla ya muda fulani akakosea anapoandika nambari, kwa mfano huenda akaandika 10,000 badala ya 100,000.

  • MADAI YASIYO YA KWELI. Si rahisi kuripoti habari kwa usahihi. Jambo ambalo linaonekana kuwa kweli leo, huenda kesho likathibitishwa kuwa si kweli. Kwa mfano, zamani watu waliamini kwamba dunia iko katikati ya mfumo wetu wa jua. Lakini sasa tunajua kwamba dunia hulizunguka jua.

 Usawaziko Unahitajika

Ingawa ni jambo la hekima kutoamini kila jambo tunalosoma katika vyombo vya habari, hilo halimaanishi kwamba tutilie shaka habari zote. Tunahitaji kujihadhari huku tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu vyombo vya habari.

Biblia inasema hivi: “Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?” (Ayubu 12:11) Yafuatayo ni madokezo yatakayotusaidia kupima maneno tunayosikia na kusoma:

  • CHANZO: Je, habari hiyo inatoka kwa mtu au shirika linaoaminika? Je, programu hiyo au chapisho hilo linajulikana kwa kutoa habari zinazoaminika au zinazosisimua tu? Shirika hilo linadhaminiwa na nani?

  • UTAFITI: Je, habari hiyo imefanyiwa utafiti wa kutosha? Je, inategemea chanzo kimoja tu? Je, vyanzo vya utafiti vinategemeka, vinatoa habari bila ubaguzi, na vinachunguza mambo kwa akili pana? Je, vina maoni yaliyosawazika au vinatoa maoni ya upande mmoja tu?

  • KUSUDI: Jiulize: ‘Je, habari hii imekusudiwa inielimishe au inifurahishe tu? Je, mwandishi anajaribu kuuza kitu fulani au kuunga mkono jambo fulani?’

  • HISIA: Habari inapoonyesha hisia za hasira, dharau, au kuchambua, hilo linaonyesha kwamba imekusudiwa kushambulia na si kutoa hoja zinazopatana na akili.

  • UPATANO: Je, habari hiyo inapatana na habari zilizo katika ripoti au makala nyingine? Ikiwa habari zinapingana, basi jihadhari!

  • IMEPITWA NA WAKATI: Je, habari hiyo ni ya karibuni? Jambo ambalo lilidhaniwa kuwa sahihi miaka 20 iliyopita huenda lisiwe sahihi leo. Kwa upande mwingine, ikiwa habari hiyo inahusu jambo lililotokea karibuni sana, huenda isitie ndani mambo yote hakika.

Kwa hiyo, je, unaweza kuamini ripoti za habari? Shauri linalofaa linapatikana katika maneno yenye hekima ya Sulemani ambaye aliandika hivi: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.