Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mamilioni ya nakala za chapisho linalosaidia kujifunza kusoma na kuandika lenye kichwa Jitahidi Kusoma na Kuandika zimechapishwa katika lugha zaidi ya 100

Elimu ya Biblia Husaidia Watu Kujua Kusoma na Kuandika

Elimu ya Biblia Husaidia Watu Kujua Kusoma na Kuandika

“Mwanadamu ana haki ya kujua kusoma na kuandika, hilo ni muhimu kwa maendeleo yake na ya jamii.”—UNESCO. *

RIPOTI zinaonyesha kwamba ulimwenguni pote watu zaidi ya milioni 700 walio na umri wa miaka 15 na zaidi hawajui kusoma na kuandika. Hivyo, hawawezi kujifunza mambo mengi kama vile mwenendo unaofaa na mafundisho ya kiroho yaliyo katika Biblia ‘yaliyoandikwa ili kutufundisha sisi.’ (Waroma 15:4) Hivyo, katika nchi nyingi Mashahidi wa Yehova wanawafundisha watu kusoma na kuandika kupitia programu yao ya kufundisha Biblia—bila malipo yoyote. Je, programu hiyo imekuwa na mafanikio?

Fikiria kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico, ambako lugha yao ya taifa ni Kihispania. Tangu mwaka wa 1946, Mashahidi wamewafundisha watu zaidi ya 152,000 kusoma na kuandika, na baadaye wanafunzi hao walikuwa walimu. Kwa kutambua mchango wa kazi yao, Mashahidi wamepokea barua nyingi kutoka serikalini. Barua moja inasema hivi: “Bodi Kuu ya Elimu inatambua na kuwapongeza kwa ushirikiano wenu mnaoonyesha katika kuendeleza Programu ya Elimu ya Watu Wazima.”

Vijana kwa wazee wamenufaika kutokana na programu ya kujifunza kusoma na kuandika. Kwa mfano, Josefina alikuwa na umri wa miaka 101 alipojiunga na programu hiyo na alifanikiwa kumaliza masomo yake baada ya miaka miwili!

Ijapokuwa lugha ya taifa nchini Mexico ni Kihispania, madarasa ya kusoma na kuandika hayafanywi katika lugha hiyo peke yake. Katika mwaka wa 2013, vikundi nane vya watu wanaozungumza lugha zao za asili, walijifunza kusoma na kuandika katika lugha hizo.

Kujua kusoma na kuandika kunaweza kukusaidia kujifunza mambo mengi. Zaidi ya yote, ujuzi huo huwawezesha watu wa namna zote kuisoma Biblia—kitabu kilichoongozwa na roho ya Mungu kinachoweza kuwaweka watu huru kutokana na utumwa wa ushirikina, mafundisho ya kidini yasiyo ya kweli, na mwenendo usiofaa.—Yohana 8:32.

^ fu. 2 Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni.