Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tunapaswa ‘Kuendelea Kukesha’?

Kwa Nini Tunapaswa ‘Kuendelea Kukesha’?

“Hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.”​—MT. 24:42.

NYIMBO: 136, 129

1. Toa mfano unaoonyesha kwa nini ni muhimu kutambua wakati na mambo yanayotukia. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

KUSANYIKO lilikuwa karibu kuanza. Mwenyekiti alienda jukwaani na kuwakaribisha watu wote. Muziki ulipoanza, wasikilizaji walijua kwamba ulikuwa wakati wa kuketi. Walitaka kusikiliza muziki mtamu na walitazamia kwa hamu hotuba ambazo zingetolewa. Hata hivyo, huenda kuna wengine ambao hawakumkazia fikira mwenyekiti au hawakutambua kwamba kipindi cha muziki kilikuwa kikiendelea. Hawakutambua kwamba kusanyiko lilikuwa limeanza, hivyo, bado walikuwa wakitembea-tembea au kuzungumza na marafiki wao. Hali hiyo inaonyesha jambo linaloweza kutokea tusipotambua wakati au mambo yanayotukia. Tunajifunza somo muhimu sana kutokana na kisa hiki kwa kuwa tutakabili tukio kubwa hata zaidi hivi karibuni, nasi tunapaswa kujitayarisha. Ni tukio gani hilo?

2. Kwa nini Yesu aliwaambia wanafunzi wake ‘waendelee kukesha’?

2 Yesu Kristo alipokuwa akizungumzia “umalizio wa mfumo wa mambo,” aliwahimiza hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kutazama, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.” Baada ya hapo, Yesu aliwahimiza hivi mara kadhaa: “Endeleeni kukesha.” (Mt. 24:3 soma Marko 13:32-37.) Pia, simulizi la Mathayo linalozungumzia habari hiyo linafunua kwamba Yesu aliwaonya wafuasi wake waendelee kukesha: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja. . . . Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” Pia alisema: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—Mt. 24:42-44; 25:13.

3. Kwa nini tunazingatia onyo la Yesu?

3 Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunachukua kwa uzito onyo la Yesu. Tunajua kwamba tunaishi katika kipindi cha mwisho kabisa cha “wakati wa mwisho” na “dhiki kuu” itaanza hivi karibuni! (Dan. 12:4; Mt. 24:21) Ulimwenguni pote tunaona vita, kuongezeka kwa ukosefu wa maadili na uasi-sheria, vurugu za kidini, upungufu wa chakula, magonjwa na matetemeko ya nchi. Tunajua kwamba kazi kubwa sana ya kuhubiri Ufalme inafanywa na watu wa Yehova kotekote. (Mt. 24:7, 11, 12, 14; Luka 21:11) Tunatazamia kwa hamu kuja kwa Yesu na kutimizwa kwa kusudi la Baba yake.—Marko 13:26, 27.

SIKU HIYO INAKARIBIA SANA

4. (a) Kwa nini tunaweza kuamini kwamba Yesu anajua wakati ambapo Har–Magedoni itatukia? (b) Ingawa hatujui dhiki kuu itaanza lini, tunaweza kuwa na uhakika gani?

4 Tunajua kwamba kila kusanyiko huwa na wakati hususa wa kuanza. Lakini hata tujitahidi kadiri gani, hatuwezi kujua mwaka hususa, siku, wala saa ambayo dhiki kuu itaanza. Yesu alisema hivi alipokuwa duniani: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mt. 24:36) Lakini Kristo amepewa mamlaka huko mbinguni ya kupiga vita dhidi ya ulimwengu wa Shetani. (Ufu. 19:11-16) Hivyo, tunaweza kufikia mkataa kwamba sasa Yesu anajua wakati ambapo Har–Magedoni itatukia. Lakini sisi hatujui. Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kuwa macho hadi wakati wa dhiki kuu. Hata hivyo, sikuzote Yehova amejua siku hiyo. Ameamua wakati hususa ambao mwisho utatokea. Kila siku inapopita wakati huo unaendelea kukaribia zaidi. ‘Haitachelewa!’ (Soma Habakuki 2:1-3.) Tunawezaje kuwa na uhakika huo?

5. Toa mfano unaoonyesha kwamba sikuzote unabii wa Yehova hutimizwa kwa wakati.

5 Sikuzote unabii mbalimbali ambao Yehova ametoa unatimia kwa wakati barabara! Fikiria wakati hususa alipowakomboa Waisraeli kutoka Misri. Musa alisema hivi kuhusu Nisani 14, 1513 K.W.K: “Mwishoni mwa ile miaka 430, naam, ikawa kwamba siku hiyo hiyo majeshi yote ya Yehova yakatoka katika nchi ya Misri.” (Kut. 12:40-42) Ile “miaka 430” ilianza Yehova alipofanya agano na Abrahamu mwaka wa 1943 K.W.K. (Gal. 3:17, 18) Muda fulani baadaye, Yehova alimwambia Abrahamu hivi: “Ujue hakika kwamba uzao wako utakuwa mkaaji mgeni katika nchi isiyokuwa yao, nao watawatumikia watu wale, nao watawatesa kwa miaka mia nne.” (Mwa. 15:13; Mdo. 7:6) Yaelekea ile “miaka 400” ya mateso ilianza 1913 K.W.K. Ishmaeli alipomdhihaki Isaka wakati alipoachishwa kunyonya, na ikaisha Waisraeli walipotoka Misri mwaka wa 1513 K.W.K. (Mwa. 21:8-10; Gal. 4:22-29) Naam, karne nne mapema, Yehova alikuwa ameamua wakati hususa wa kuwakomboa watu wake!

6. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawaokoa watu wake?

6 Yoshua, ambaye alikuwa kati ya wale waliokombolewa kutoka Misri, aliwakumbusha hivi Waisraeli wote: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.” (Yos. 23:2, 14) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba ahadi ya Yehova ya kutukomboa katika dhiki kuu itatimia pia. Hata hivyo, ili tuokoke uharibifu wa mfumo huu, tunapaswa kuendelea kukesha.

ENDELEA KUKESHA ILI UOKOKE

7, 8. (a) Katika nyakati za kale, mlinzi alikuwa na wajibu gani, na tunajifunza nini kutokana na hilo? (b) Toa mfano wa jambo linaloweza kutukia mlinzi anapolala akiwa kazini.

7 Tunaweza kujifunza somo kutokana na wakati uliopita kuhusu umuhimu wa kuendelea kuwa macho. Nyakati hizo, majiji makubwa kama Yerusalemu yalizungukwa na kuta kubwa. Kuta hizo ziliandaa ulinzi dhidi ya wavamizi na pia zilikuwa na minara mirefu ambapo walinzi wangeweza kuangalia maeneo yaliyozunguka. Walinzi walikuwa kwenye malango na kuta usiku na mchana. Ikiwa wangeona hatari yoyote, walipaswa kuwajulisha wakazi wa jiji. (Isa. 62:6) Walijua umuhimu wa kuwa macho na kuwa makini ili kutambua mambo yaliyotendeka karibu nao. Iwapo hawangefanya hivyo, watu wengi wangeweza kufa.—Eze. 33:6.

8 Mwanahistoria Myahudi Yosefo, anasema kwamba katika mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yaliweza kutwaa Mnara wa Antonia, uliokuwa karibu na ukuta wa jiji la Yerusalemu kwa sababu walinzi waliokuwa kwenye malango walikuwa wamelala! Kwa sababu hiyo, Waroma waliingia hekaluni na kuliteketeza, na huo ukawa mwisho wa dhiki kuu zaidi iliyowahi kukabili jiji la Yerusalemu na taifa la Wayahudi.

9. Watu wengi leo wanakosa kutambua nini?

9 Leo, nchi nyingi zinalinda mipaka yao kwa kutumia wanajeshi na mifumo ya usalama ya hali ya juu. Walinzi hao huchunguza maeneo yao kuhakikisha kwamba watu hawaingii bila kibali na maadui hawahatarishi usalama wa nchi. Hata hivyo, walinzi hao wanaweza kuona tu hatari zinazotoka kwa serikali za kibinadamu au wanadamu. Hawatambui kwamba Ufalme wa Mungu umesimamishwa mbinguni na unafanya kazi mikononi mwa Kristo. Pia hawatambui kwamba Ufalme huo una jukumu la kuhukumu mataifa yote hivi karibuni. (Isa. 9:6, 7; 56:10; Dan. 2:44) Kwa upande mwingine, tukiwa macho na kuendelea kukesha kiroho, tutakuwa tayari siku hiyo ya hukumu itakapofika.—Zab. 130:6.

USIKENGEUSHWE

10, 11. (a) Tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu nini, na kwa nini? (b) Ni nini kinachokusadikisha kwamba Ibilisi amewafanya watu wapuuze unabii wa Biblia?

10 Wazia mlinzi ambaye anahitaji kuwa macho usiku kucha. Kwa kawaida, yeye huchoka na kuhisi usingizi muda mfupi tu kabla ya zamu yake kwisha. Vivyo hivyo, kadiri tunavyokaribia mwisho wa mfumo huu wa mambo, ndivyo inavyokuwa vigumu kuendelea kukesha. Ingesikitisha sana iwapo tungeshindwa kuendelea kukesha! Acheni tuzungumzie mambo matatu yanayoweza kufanya tusiendelee kukesha.

11 Ibilisi anapofusha watu ili wasipendezwe na mambo ya kiroho. Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaonya wanafunzi wake mara tatu kuhusu “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yoh. 12:31; 14:30; 16:11) Yesu alijua kwamba Ibilisi angewafanya watu wabaki gizani kiakili ili wasiwe na hisi ya uharaka inayozungumziwa mara nyingi katika unabii kutoka kwa Mungu kuhusu wakati ujao. (Sef. 1:14) Shetani anapofusha akili za watu kupitia milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. Umegundua nini unapozungumza na watu wengine? Je, si kweli kwamba tayari Ibilisi “amezipofusha akili za wasioamini” kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo na kwamba Kristo anatawala sasa katika Ufalme wa Mungu? (2 Kor. 4:3-6) Tunasikia mara nyingi watu wakisema, “Sipendezwi.” Wengi wao hawajali tunapowaambia kuhusu jambo litakaloupata ulimwengu huu.

12. Kwa nini hatupaswi kumruhusu Ibilisi atudanganye?

12 Usiruhusu hali ya kutojali ya wengine ikuvunje moyo au kukufanya usiendelee kukesha. Tunajua ni kwa nini tunapaswa kuendelea kufanya hivyo. Paulo aliwaandikia hivi waamini wenzake: “Ninyi wenyewe mnajua vema kabisa kwamba siku ya Yehova inakuja,” kisha akaongeza, “sawasawa kabisa kama mwizi usiku.” (Soma 1 Wathesalonike 5:1-6.) Yesu alituonya hivi: “Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyoitazamia.” (Luka 12:39, 40) Hivi karibuni, Shetani atawadanganya watu wengi wahisi kwamba kuna “amani na usalama.” Atawapotosha na kuwafanya wafikiri kwamba mambo yote yako sawa. Namna gani sisi? Siku hiyo ya hukumu haipaswi “[kutufikia] kama vile ambavyo ingewafikia wezi,” maadamu ‘tutakaa macho na kutunza akili zetu.’ Hiyo ndiyo sababu tunapaswa kusoma na kutafakari Neno la Mungu kila siku ili tujue kile ambacho Yehova anatuambia.

13. Roho ya ulimwengu inaathirije watu, na tunaweza kuepukaje hatari hiyo?

13 Roho ya ulimwengu inafanya watu wasinzie kiroho. Watu wengi wanajishughulisha sana na mambo ya kawaida maishani hivi kwamba hawatambui “uhitaji wao wa kiroho.” (Mt. 5:3) Wamezama kwa kuvutiwa na vitu vya ulimwengu vinavyochochea “tamaa ya mwili na tamaa ya macho.” (1 Yoh. 2:16) Pia, leo kuliko wakati mwingine wowote, kuna burudani nyingi ambazo zinawavutia na kuwachochea watu “[wapende] raha” na kutosheleza tamaa yoyote waliyo nayo. (2 Tim. 3:4) Hiyo ndiyo sababu Paulo aliwaandikia Wakristo kwamba hawapaswi “[kupanga] kimbele kwa ajili ya tamaa za mwili,” ambazo huwafanya watu walale kiroho.—Rom. 13:11-14.

14. Tunapata onyo gani katika andiko la Luka 21:34, 35?

14 Badala ya kuongozwa na roho ya ulimwengu, tunakubali kuongozwa na roho takatifu ambayo Yehova anatumia kutusaidia tuelewe waziwazi matukio ya wakati ujao. [1] (1 Kor. 2:12) Hata hivyo, tunahitaji kuwa waangalifu. Hata mambo ya kawaida maishani yanaweza kutukengeusha tusimtumikie Yehova. (Soma Luka 21:34, 35.) Huenda wengine wakatudhihaki kwa sababu ya kuendelea kukesha, lakini hiyo si sababu ya kupoteza hisi yetu ya uharaka. (2 Pet. 3:3-7) Badala yake, tunapaswa kushirikiana kwa ukawaida na Wakristo wenzetu katika mikutano ya kutaniko, mahali ambapo tunapata roho ya Mungu.

Je, unafanya yote uwezayo kubaki macho kiroho? (Tazama fungu la 11 hadi 16)

15. Ni nini kilichowapata Petro, Yakobo, na Yohana, na tunaweza kupatwa na jambo hilo jinsi gani?

15 Udhaifu wetu wa kimwili unaweza kudhoofisha azimio letu la kubaki macho. Yesu alijua kwamba wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kushindwa na udhaifu wa kimwili. Fikiria mambo yaliyotokea usiku uliotangulia kifo cha Yesu. Ili adumishe utimilifu wake, alihitaji kumwomba Baba yake wa mbinguni ampe nguvu. Yesu aliwaambia Petro, Yakobo, na Yohana “[waendelee] kukesha” alipokuwa akisali. Hata hivyo, hawakutambua uzito wa mambo ambayo yangetukia. Walikuwa wamechoka, nao wakalala. Yesu pia alikuwa amechoka lakini alikesha na kusali kwa Baba yake. Mitume wake walipaswa kufanya hivyo.—Marko 14:32-41.

16. Kulingana na Luka 21:36, Yesu alituagiza ‘tuendelee kukesha’ jinsi gani?

16 ‘Kuendelea kukesha’ kiroho hakumaanishi kuwa na nia nzuri tu ya kufanya yaliyo sawa. Siku chache kabla ya mambo yaliyotukia katika bustani ya Gethsemane, Yesu aliwaambia wanafunzi haohao waombe dua kwa Yehova. (Soma Luka 21:36.) Kwa hiyo, ili tuendelee kukesha kiroho, sisi pia tunahitaji kukesha kuhusiana na sala.—1 Pet. 4:7.

ENDELEENI KUKESHA

17. Tunaweza kuhakikishaje kwamba tuko tayari kwa mambo yatakayotukia hivi karibuni?

17 Kwa kuwa Yesu alisema kwamba mwisho utakuja ‘katika saa tusiyofikiria,’ huu si wakati wa kusinzia kiroho, wala wakati wa kufuatilia mambo yasiyo halisi ya Shetani na ulimwengu wake au ambayo mwili wetu unatamani. (Mt. 24:44) Kupitia Biblia, Mungu na Kristo wanatueleza mambo ambayo watafanya hivi karibuni na jinsi tunavyoweza kuendelea kukesha. Tunapaswa kukazia fikira hali yetu ya kiroho, uhusiano wetu na Yehova, na kutanguliza Ufalme. Lazima tutambue wakati na mambo yanayotukia ili tuwe tayari kwa ajili ya mambo yajayo. (Ufu. 22:20) Uhai wetu upo hatarini!

^ [1] (fungu la 14) Tazama sura ya 21 ya kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala!