Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Waroma wangeruhusu mtu kama vile Yesu ambaye walikuwa wamemtundika mtini, azikwe kwa njia ya kawaida?

WATU wengi wanalijua simulizi la Yesu kuhusu kutundikwa kwenye mti wa mateso katikati ya wahalifu wawili. (Mt. 27:35-38) Hata hivyo, baadhi ya watu wanatilia shaka kuhusu usahihi wa simulizi hilo la Biblia kwamba baadaye mwili wa Yesu ulifanyiwa matayarisho kwa ajili ya kuzikwa na kuwekwa kaburini.​—Marko 15:42-46.

Baadhi ya watu wanaokosoa vitabu vya Injili, wametilia shaka kwamba mtu aliyekuwa ametundikwa mtini angezikwa kwa heshima, kama vile kaburini. Badala yake, wanaamini kwamba inaelekea alitendewa kwa njia tofauti. Mwandishi wa habari Ariel Sabar, wa gazeti la Smithsonian, anafafanua hivi chanzo cha maoni hayo: “Adhabu ya kutundikwa mtini ilikuwa kwa ajili ya watu wabaya zaidi kwenye jamii, na baadhi ya wataalamu wanafikiri kwamba lingekuwa jambo la kipumbavu kwa Waroma kuwazika watu hao kwa heshima.” Waroma walitaka watu waliohukumiwa kwa uhalifu waaibishwe kadiri inavyowezekana, hivyo mara nyingi miili yao ingeachwa mtini ili iliwe na wanyama. Baada ya hapo, huenda mabaki ya miili yao yalitupwa kwenye kaburi la ujumla.

Hata hivyo, wavumbuzi wa vitu vya kale wamegundua jambo fulani tofauti, angalau kuhusu mabaki ya baadhi ya Wayahudi waliouawa. Mwaka wa 1968, mabaki ya mifupa ya mtu aliyeuawa katika karne ya kwanza yalipatikana. Yalipatikana kwenye kaburi la kawaida la familia ya Kiyahudi karibu na Yerusalemu. Mabaki hayo yalikuwa kwenye sanduku la mifupa. Mfupa wa kisigino ulikuwa miongoni mwa mabaki hayo. Ulikuwa umepigiliwa kwenye mbao kwa msumari wa chuma wenye sentimita 11.5 (inchi 4.5). Sabar anasema: “Mfupa huo uliokuwa wa mwanamume aliyeitwa Yehokanani, ulisaidia kumaliza mabishano ya muda mrefu kuhusu masimulizi ya Injili kwamba Yesu alizikwa kaburini.” Ni wazi kwamba “mfupa wa kisigino wa Yehokanani ulitoa mfano wa mtu aliyetundikwa mtini katika siku za Yesu ambaye Waroma waliruhusu azikwe kulingana na tamaduni za Kiyahudi.”

Huenda kuna maoni mbalimbali kuhusu jambo ambalo mfupa huo wa kisigino unafunua kuhusiana na jinsi Yesu alivyotundikwa mtini. Hata hivyo, jambo lililo wazi ni kwamba baadhi ya wahalifu waliouawa walizikwa na hawakutupwa tu. Ni wazi kwamba kile ambacho Biblia inasema kuhusu mwili wa Yesu kuzikwa kaburini ni sahihi. Uthibitisho huo unaunga mkono jambo ambalo Biblia inasema.

Jambo muhimu hata zaidi, Yehova alikuwa ametabiri kwamba Yesu angezikwa katika kaburi la mtu tajiri, na hakuna anayeweza kuzuia neno la Mungu kutimizwa.​—Isa. 53:9; 55:11.