Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ona Mambo Kama Mungu Anavyoyaona

Ona Mambo Kama Mungu Anavyoyaona

Ona Mambo Kama Mungu Anavyoyaona

SEPTEMBA 14, 2002 ilikuwa siku nzuri yenye joto na jua katika jimbo la New York, Marekani. Siku hiyo, watu 6,521 kutoka nchi mbalimbali walikusanyika kwenye Kituo cha Elimu cha Patterson cha Mashahidi wa Yehova na vilevile huko Brooklyn na Wallkill. Watu hao walikuwa wamekuja kuhudhuria kuhitimu kwa darasa la 113 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Wanafunzi walitoka nchi 14 na kwa muda wa miezi mitano walikuwa wakijitayarisha kwa ajili ya utumishi wa mishonari katika nchi 19 ambako wangetumwa.

Carey Barber mwenye umri wa miaka 97 na ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikuwa mwenyekiti wa pindi hiyo. Alitaja kwamba kwa karibu miaka 60, maelfu ya watu wamezoezwa kazi ya umishonari katika Shule ya Gileadi. Ndugu Barber alisema hivi: “Hatutii chumvi tukisema kwamba mazoezi hayo yameleta matokeo mazuri ajabu. Wamishonari waliozoezwa wamewasaidia maelfu ya watu wanyenyekevu duniani pote kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova, kuanza kumwabudu kwa njia ya kweli, na kumtolea utumishi mtakatifu.”

Kabla ya kwenda Shule ya Gileadi, wengi wa wanafunzi hao walitaka kupanua huduma yao. Wenzi fulani wa ndoa walikuwa wamejifunza Kichina kwa zaidi ya mwaka mmoja ili waweze kuwahubiria Wachina wengi wanaoishi katika eneo la kwao huko Kanada. Wenzi wengine wa ndoa walijifunza Kialbania na hatimaye wakahamia Albania ili kusaidia kufanya kazi ya kufundisha Biblia huko. Wanafunzi wengine walitoka Hungaria, Guatemala, na Jamhuri ya Dominika. Walikuwa wamehamia nchi hizo kwa sababu kulikuwa na uhitaji mkubwa wa walimu wa Neno la Mungu.

Sasa, kabla ya kwenda Afrika, Ulaya Mashariki, Amerika ya Kusini na ya Kati, au Mashariki ya Mbali, wanafunzi wote waliokuwa wakihitimu walihimizwa wamkumbuke Mungu katika shughuli zao zote.

Ona Mambo Kama Mungu Anavyoyaona

Baada ya maneno yake ya utangulizi, Ndugu Barber alimwalika Maxwell Lloyd aliye mshiriki wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi la Marekani. Yeye alizungumzia kichwa, “Ona Mambo Yote Kama Mungu Anavyoyaona.” Ndugu Lloyd alizungumzia mifano ya Daudi na Mwana wa Mungu, Yesu. (1 Samweli 24:6; 26:11; Luka 22:42) Baada ya kuwakumbusha wanafunzi kwamba masomo yao ya Biblia ya miezi mitano yamewazoeza kuyaona mambo kama Mungu anavyoyaona, msemaji aliuliza: “Utakapoongoza mafunzo ya Biblia pamoja na watu mahali utakapotumwa, je, utawasaidia kuyaona mambo kama Mungu anavyoyaona?” Kuhusiana na kuwashauri wengine, alipendekeza hivi: “Usiseme, ‘Kwa maoni yangu, mimi naona . . . ’ Badala yake, wasaidie kutambua maoni ya Mungu. Ukifanya hivyo, utakuwa baraka kwelikweli kwa wale ambao utashirikiana nao mahali utakapotumwa.”

Msemaji aliyefuata alikuwa Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Katika hotuba yake yenye kichwa “Mimi Ni Pamoja Nawe,” alionyesha kwamba katika pindi nyingi Yehova aliwaambia watumishi wake waaminifu, “Mimi ni pamoja nawe.” (Mwanzo 26:23, 24; 28:15; Yoshua 1:5; Yeremia 1:7, 8) Tukibaki waaminifu tutaweza kuwa na tumaini hilohilo leo. Ndugu Lösch alisema hivi: “Je, una wasiwasi kwamba hutapata watu wa kujifunza Biblia pamoja nao? Kumbuka kwamba Yehova alisema, ‘Mimi ni pamoja nawe.’ Je, una wasiwasi kwamba utakosa vitu vya kimwili? Yehova alisema hivi: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.” (Waebrania 13:5) Ndugu Lösch alimalizia kwa kuwakumbusha wanafunzi kwamba Yesu aliahidi kuwa pamoja na wafuasi wake waaminifu katika kazi ya kufanya wanafunzi.—Mathayo 28:20.

Lawrence Bowen, aliye mmoja wa walimu wa Shule ya Gileadi, alitoa hotuba yenye kichwa: “Je, Utakuwa Salama Utakapojaribiwa Vikali Kama kwa Moto?” Alionyesha kwamba kwa sababu ya masuala yaliyozuka huko Edeni, wote ambao wamejitahidi kumwabudu Yehova pekee wamekabili magumu, na nyakati nyingine, majaribu makali sana. Aliwatia moyo wanafunzi wenye kuhitimu kufuata mfano wa Yesu aliyepata usalama wa kweli kwa kumtegemea Yehova kabisa na kukubali majaribu makali ambayo Yehova aliruhusu ili kukamilisha utii wa Mwanawe. (Waebrania 5:8, 9) Yehova anaweza kulinganishwa na mtu asafishaye dhahabu, ambaye hutumia kiasi kinachofaa kabisa cha joto ili kuondoa uchafu. Bila shaka, imani iliyojaribiwa kwa moto inaleta usalama mkubwa kuliko dhahabu iliyosafishwa. Kwa nini? “Kwa maana imani iliyojaribiwa inaweza kustahimili majaribu yoyote yale, na inatutayarisha kuvumilia hadi ‘mwisho,’” Ndugu Bowen akajibu.—Mathayo 24:13.

Mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi, Mark Noumair, aliuliza swali hili: “Je, Utapendwa?” Hotuba yake ilikazia hasa maneno ya 1 Samweli 2:26, Biblia Habari Njema, yanayomfafanua Samweli kuwa mtu ‘aliyependwa na Mwenyezi-Mungu na watu.’ Baada ya kuzungumzia mfano wa Samweli, Ndugu Noumair, ambaye alitumikia akiwa mishonari huku Afrika kwa zaidi ya miaka kumi, alisema hivi: “Unaweza pia kupendwa na Mungu ukifanya kazi ambayo Mungu amekupatia kwa uaminifu bila kuacha. Amekupatia kazi ya maana sana ya umishonari.” Kisha Ndugu Noumair aliwahimiza wanafunzi wa darasa hilo waliokuwa wakihitimu waione kazi yao ya umishonari kuwa amana takatifu kutoka kwa Mungu na wawe na maoni ya Mungu wanapofanya kazi hiyo.

Katika miezi mitano ambayo wanafunzi walikuwa shuleni, walikuwa na fursa nyingi siku ya Jumamosi na Jumapili kuongea na watu katika eneo hilo juu ya “mambo yenye fahari ya Mungu” yanayotajwa katika Biblia. (Matendo 2:11) Walizungumzia mambo hayo katika lugha kumi mbalimbali. Wallace Liverance, mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi, aliwahoji wanafunzi kadhaa walioeleza mambo waliyoona. Kichwa kilichokaziwa katika mahojiano hayo kilikuwa “‘Mambo Yenye Fahari ya Mungu’ Huwachochea Watu Kutenda.” Alisema hivi: “Roho iliwachochea wale waliokuwa katika chumba cha juu siku ya Pentekoste waseme kuhusu ‘mambo yenye fahari ya Mungu.’ Roho hiyo ndiyo inayowachochea watumishi wote waaminifu wa Mungu leo. Wengine wao wamesukumwa kujifunza lugha mpya ili waweze kuwahubiria watu wengi zaidi.

Ushauri Mzuri Kuhusu Jinsi ya Kuyaona Mambo Kama Mungu Anavyoyaona

Baada ya hotuba za kwanza, Gary Breaux na William Young, wafanyakazi kwenye Ofisi ya Tawi ya Marekani, waliwahoji washiriki wa halmashauri mbalimbali za ofisi za tawi za nchi ambako mishonari hutumikia. Waliwahoji vilevile wenzi wa ndoa ambao wamekuwa mishonari kwa miaka 41. Walikazia jambo hili: “Wale wanaodumu kwa muda mrefu katika kazi ya umishonari ni wale wasiozingatia maisha ya starehe. Wao hutia maanani kusudi kuu la kazi ya umishonari. Wanajua kwamba kusudi hilo ni kuhubiri habari njema na kuwasaidia watu kumjua Yehova.”

Mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, David Splane, alimalizia pindi hiyo kwa hotuba yenye kichwa “Hamtakwenda Mbali!” Maneno yake yalimaanisha nini, hali wanafunzi 46 waliohitimu wangetumwa kotekote duniani? Alieleza hivi: “Hata ukiwa wapi duniani, utakuwa katika nyumba ya Mungu maadamu utakuwa mwaminifu.” Naam, Wakristo wote waaminifu, mahali potepote walipo, wanamtumikia Mungu katika hekalu lake kuu la kiroho, au nyumba yake, ambalo limekuwapo tangu Yesu abatizwe katika karne ya kwanza. (Waebrania 9:9) Wasikilizaji wote walifarijika kama nini kujua kwamba Yehova yu karibu na watumishi wake wote waaminifu duniani! Popote tulipo, Yehova anatujali sisi sote na utumishi wetu Kwake, kama alivyomjali Yesu alipokuwa duniani. Kwa hiyo, kwa habari ya ibada, hatuko mbali na Wakristo wenzetu wala Yehova na Yesu.

Baada ya kutaja salamu za kutoka sehemu mbalimbali za dunia, kutangaza nchi ambazo wanafunzi wangetumwa, na kusoma barua ya shukrani kutoka kwa wanafunzi kwa mazoezi waliyopata, mwenyekiti alimalizia pindi hiyo kwa kuwatia moyo mishonari hao wapya waendelee na kazi yao nzuri na washangilie katika utumishi wa Yehova.—Wafilipi 3:1.

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

TAKWIMU ZA DARASA

Wanafunzi walitoka nchi: 14

Wanafunzi wametumwa katika nchi: 19

Idadi ya wanafunzi: 46

Wastani wa umri: 35.0

Wastani wa miaka katika kweli: 17.2

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.7

[Picha katika ukurasa wa 24]

Darasa la 113 lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Ligthart, M.; Hosoi, S.; Berktold, A.; Liem, C.; Aoki, J. (2) Baglyas, J.; Bouqué, S.; Bossi, A.; Alton, J.; Escobar, I.; Escobar, F. (3) Stoica, A.; Stoica, D.; Freimuth, S.; Karlsson, M.; LeBlanc, R. (4) Bianchi, R.; Bianchi, S.; Kaminski, L.; Joseph, L.; Paris, S.; LeBlanc, L. (5) Paris, M.; Skidmore, B.; Horton, J.; Horton, L.; Skidmore, G. (6) Liem, B.; Alton, G.; Quirici, E.; Langlois, M.; Steininger, S.; Aoki, H. (7) Langlois, J.; Steininger, M.; Bossi, F.; Kaminski, J.; Bouqué, J.; Ligthart, E.; Hosoi, K. (8) Baglyas, J.; Quirici, M.; Karlsson, L.; Freimuth, C.; Berktold, W.; Joseph, R.