Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova—Mungu Tunayepaswa Kumjua

Yehova—Mungu Tunayepaswa Kumjua

Yehova—Mungu Tunayepaswa Kumjua

JE, UNAKOSA kutambua na kunufaika na jambo fulani muhimu maishani? Ikiwa humjui Mungu sana, basi yaonekana hutambui jambo hilo. Kwa nini? Kwa sababu, kama vile mamilioni ya watu wamegundua, kumjua Mungu anayetajwa katika Biblia hunufaisha sana maishani. Mtu huanza kunufaika sasa, na huendelea kunufaika zaidi wakati ujao.

Yehova Mungu, Mtungaji wa Biblia, anataka tumjue. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Anatambua kwamba tutanufaika kwa kumjua. “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida.” Tunanufaikaje kwa kumjua Yehova Mungu, Aliye Juu Zaidi?—Zaburi 83:18; Isaya 48:17.

Faida moja ni kwamba tunapata mwongozo wa kukabiliana na matatizo ya kila siku, tunakuwa na tumaini hakika la wakati ujao, na amani ya akili. Isitoshe, kumjua Yehova vizuri hutuchochea kusitawisha mtazamo tofauti kuhusiana na masuala muhimu zaidi yanayowakabili watu ulimwenguni pote leo. Ni masuala gani hayo?

Je, Maisha Yako Yana Kusudi?

Licha ya maendeleo makubwa sana ya kitekinolojia ambayo wanadamu wamefanya, bado watu hujiuliza maswali haya muhimu: ‘Kwa nini nipo hapa? Ninaelekea wapi? Ni nini kusudi la maisha?’ Mtu asipopata majibu yenye kuridhisha, atakosa kusudi halisi maishani. Je, watu wengi wamekosa kusudi maishani? Uchunguzi uliofanywa nchini Ujerumani mwishoni mwa miaka ya 1990 ulionyesha kwamba mara nyingi nusu ya watu waliohojiwa walihisi kwamba maisha hayana kusudi. Labda watu wanahisi hivyo mahali unapoishi.

Maisha yasipokuwa na kusudi, mtu hawezi kuwa na sababu ya kuweka miradi ya kibinafsi. Wengi hujaribu kutafuta maisha yenye kusudi kwa kufuatia kazi yenye mshahara mnono au kulundika mali. Hata hivyo, bado mtu anaweza kufadhaika kwa kukosa kusudi. Watu fulani hufadhaika sana kwa kukosa kusudi maishani kiasi kwamba wanaona hakuna haja ya kuishi. Ndivyo ilivyokuwa kwa mwanamke kijana mrembo, ambaye kulingana na kichapo International Herald Tribune, alilelewa katika familia “yenye utajiri mwingi na anasa.” Ingawa aliishi maisha ya anasa, alikuwa mpweke na alihisi kwamba maisha yake hayana kusudi. Alimeza vidonge vya usingizi na akapatikana amekufa. Huenda unawajua watu wengine wenye upweke waliokufa kwa njia hiyo ya kuhuzunisha.

Hata hivyo, je, umewahi kusikia watu wanaodai kwamba sayansi inaweza kutueleza mambo yote kuhusu maisha? Gazeti la Ujerumani, Die Woche, linalochapishwa kila juma linasema: “Ingawa sayansi inaweza kusema kweli, imepungukiwa kwa upande wa kiroho. Nadharia ya mageuzi huonekana kuwa muhimu na hata fizikia ambayo hubadilika-badilika, haileti faraja na usalama.” Uvumbuzi wa kisayansi umesaidia sana kufafanua namna mbalimbali za uhai na kuelezea taratibu mbalimbali ambazo huendeleza uhai. Hata hivyo, sayansi haiwezi kutuambia kwa nini tupo hapa na mahali tunapoelekea. Tukitegemea sayansi pekee, hatutapata majibu kuhusu kusudi la maisha. Gazeti moja linaloitwa Süddeutsche Zeitung lilisema kwamba “kila mahali watu wanahitaji mwongozo.”

Ni Muumba pekee yake anayeweza kutoa mwongozo huo. Kwa kuwa yeye ndiye aliyewaweka wanadamu wa kwanza duniani hapo mwanzo, ni lazima awe anajua ni kwa nini wapo hapa. Biblia inaeleza kwamba Yehova aliumba wanadamu ili waijaze dunia na kuitunza. Katika utendaji wao wote, wanadamu walipaswa kuonyesha sifa za Mungu kama vile haki, hekima, na upendo. Tukielewa sababu iliyofanya Yehova atuumbe, tutajua ni kwa nini tupo hapa.—Mwanzo 1:26-28.

Unaweza Kufanya Nini?

Namna gani ikiwa hapo awali hukupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali: ‘Kwa nini nipo hapa? Ninaelekea wapi? Ni nini kusudi la maisha?’ Biblia inakuhimiza umjue Yehova kibinafsi. Kwa kweli, Yesu alisema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ Pia unatiwa moyo usitawishe sifa za kimungu, hasa upendo, na uweke mradi wa kuwa raia wa Ufalme wa Kimesiya wa Mungu unaokuja. Ndipo utakapokuwa na kusudi maishani na tumaini zuri na hakika la wakati ujao. Yaelekea maswali muhimu yaliyokuwa yakikusumbua yatajibiwa.—Yohana 17:3; Mhubiri 12:13.

Majibu ya maswali hayo muhimu yatakuathirije? Hans anajua jinsi majibu hayo yanavyoweza kumwathiri mtu. * Miaka kadhaa iliyopita alikuwa na imani ya kijuujuu tu kumhusu Mungu. Imani ya Hans haikuathiri maisha yake. Hans alipenda dawa za kulevya, wanawake wasio na maadili, uhalifu mdogo-mdogo, na pikipiki. “Lakini maisha hayakuwa na kusudi, wala hayakuridhisha,” yeye asema. Alipokuwa na umri wa miaka 20 na kitu, Hans aliamua kumjua Mungu kibinafsi kwa kusoma Biblia kwa makini. Baada ya kumjua Yehova kibinafsi na kuelewa kusudi la maisha, Hans alibadili maisha yake, akabatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka kumi sasa. Anasema hivi waziwazi: “Kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Hakuna jambo jingine lililo bora kuliko kumtumikia Yehova. Nimepata kusudi maishani kwa kumjua Yehova.”

Bila shaka, kuna mambo mengine yanayowahangaisha watu mbali na kutaka kujua kusudi la maisha. Kadiri hali za ulimwengu zinavyozidi kuzorota, watu wengi zaidi wanatatizwa na jambo jingine muhimu.

Kwa Nini Nilipatwa na Msiba?

Msiba unapotokea, mara nyingi mtu hujiuliza swali moja: Kwa nini nilipatwa na msiba huu? Uwezo wa kukabiliana na msiba hutegemea sana kupata jibu linalofaa kwa swali hilo. Ikiwa hakuna jibu lenye kuridhisha, huenda mtu akaendelea kuteseka na kukata tamaa. Kwa mfano, fikiria msiba uliompata Bruni.

“Mtoto wangu msichana alikufa miaka kadhaa iliyopita,” asema Bruni, ambaye sasa ni mama wa makamo. “Nilimwamini Mungu, kwa hiyo nilienda kwa kasisi ili anifariji. Aliniambia kwamba Mungu amemchukua Susanne akaishi mbinguni, na sasa yeye ni malaika. Maisha yangu yalibadilika kabisa baada ya binti yangu kufa na nilimchukia Mungu kwa sababu ya kumchukua.” Bruni aliendelea kuumia na kuteseka kwa miaka kadhaa. “Kisha mmoja wa Mashahidi wa Yehova akanionyesha katika Biblia ni kwa nini sipaswi kumchukia Mungu. Yehova hakumchukua Susanne akaishi mbinguni, wala yeye si malaika. Alipatwa na ugonjwa kwa sababu ya kutokamilika kwa wanadamu. Susanne amelala katika kifo, akingojea Yehova amfufue. Pia nilijifunza kwamba Mungu aliumba wanadamu waishi milele katika paradiso duniani, na kwamba kusudi hilo litatimizwa hivi karibuni. Nilianza kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova nilipofahamu sifa zake, na maumivu yangu yakaanza kupungua.”—Zaburi 37:29; Matendo 24:15; Waroma 5:12.

Mamilioni ya watu wanakabiliwa na shida mbalimbali: misiba ya kibinafsi, vita, njaa, au msiba wa asili. Bruni alipata kitulizo alipojifunza Biblia na kufahamu kwamba hatupaswi kumlaumu Yehova kwa misiba inayotupata, Yeye hakukusudia wanadamu wateseke, na hivi karibuni atakomesha uovu. Kuongezeka kwa uovu ni ishara ya kwamba sasa tunaishi katika “siku za mwisho” wa mfumo huu wa mambo. Badiliko la pekee litakaloleta hali nzuri na ambalo sote tunalitazamia kwa hamu liko karibu.—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:7, 8.

Kumjua Mungu

Hans na Bruni walimjua Mungu kijuujuu tu. Walimwamini lakini hawakumjua sana. Walipotenga wakati ili wapate kumjua Yehova kwa usahihi, walithawabishwa kwa jitihada zao. Walipata majibu yanayofaa kwa maswali muhimu sana leo. Walipata amani ya akili na tumaini hakika la wakati ujao. Mamilioni ya watumishi wa Yehova wamepata tumaini hilo.

Mtu huanza kumjua Yehova kwa kujifunza Biblia kwa makini. Biblia hutueleza kumhusu Mungu na mambo anayotaka tufanye. Hivyo ndivyo walivyofanya watu fulani katika karne ya kwanza. Luka ambaye alikuwa mwanahistoria na tabibu anasema kwamba washiriki wa kutaniko la Kiyahudi huko Beroya, Ugiriki, “walilipokea neno [kutoka kwa Paulo na Sila] kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.”—Matendo 17:10, 11.

Pia Wakristo wa karne ya kwanza walikusanyika pamoja kwenye makutaniko. (Matendo 2:41, 42, 46; 1 Wakorintho 1:1, 2; Wagalatia 1:1, 2; 2 Wathesalonike 1:1) Ndivyo ilivyo leo. Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova hukusanyika pamoja kwa ajili ya mikutano yao ambayo imekusudiwa hasa kusaidia watu wamkaribie Yehova zaidi na wafurahie kumtumikia. Kuna manufaa zaidi za kushirikiana na Mashahidi. Kwa kuwa wanadamu hudhihirisha hatua kwa hatua sifa za Mungu wanayeabudu, Mashahidi wa Yehova huonyesha sifa kama za Yehova japo si kikamilifu. Kwa hiyo tunaweza kumjua Yehova vizuri zaidi kwa kukusanyika pamoja na Mashahidi.—Waebrania 10:24, 25.

Je, tunahitaji kujitahidi sana hivyo ili kumjua Mungu? Bila shaka jitihada inahitajiwa. Lakini je, si kweli kwamba wewe hujitahidi sana kutimiza mambo mengi unayotaka maishani? Fikiria jinsi mwana-michezo anavyojitahidi wakati wa mazoezi. Kwa mfano, mshindi wa nishani ya dhahabu katika michezo ya Olimpiki ya kuteleza barafuni, Jean-Claude Killy wa Ufaransa, anasema hivi kuhusu mambo yanayoweza kumsaidia mtu awe mshindanaji wa kimataifa: “Lazima uanze miaka 10 kabla ya michezo ya Olimpiki na kupanga kwa miaka mingi huku ukifikiri juu ya mashindano hayo kila siku . . . Ni kazi ya kiakili na kimwili inayohitaji kufanywa kila siku.” Jitihada yote hiyo inahitajiwa ili kushindana katika shindano linaloweza kuchukua muda wa dakika kumi tu! Tukijitahidi kumjua Yehova, tunaweza kupata faida kubwa na ya kudumu.

Uhusiano Unaozidi Kukua

Ni nani angependa kukosa kunufaika na kitu fulani muhimu maishani? Hakuna. Kwa hiyo, iwapo unahisi kwamba maisha yako hayana kusudi au ikiwa ungependa kujua ni kwa nini tunapatwa na misiba, basi azimia kabisa kumjua Yehova, Mungu wa Biblia. Maisha yako yanaweza kubadilika na kuwa mazuri kwa umilele, ukijifunza kumhusu Yehova.

Je, tutakoma kujifunza kumhusu Yehova? Wale ambao wamekuwa wakimtumikia kwa miaka mingi bado wanashangazwa na mambo ambayo wamejifunza kumhusu na mambo mapya wanayoendelea kujifunza juu yake. Tunapata furaha na kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Mungu tunapojifunza mambo hayo. Na tukubaliane maneno haya ya mtume Paulo aliyeandika hivi: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia! Kwa maana ‘ni nani amekuja kuijua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake?’”—Waroma 11:33, 34.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Watu bado huuliza maswali yaleyale muhimu: ‘Kwa nini nipo hapa? Ninaelekea wapi? Ni nini kusudi la maisha?’

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Nilianza kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova nilipofahamu sifa zake”

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Kumtumikia Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Hakuna jambo jingine lililo bora kuliko kumtumikia Yehova. Nimepata kusudi maishani kwa kumjua Yehova”