Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fadhili—Sifa Muhimu Machoni pa Mungu

Fadhili—Sifa Muhimu Machoni pa Mungu

KIJANA mmoja huko Japani alichochewa kwa sababu mwanamume fulani mzee alimtendea kwa fadhili. Mwanamume huyo ambaye ni mmishonari, hakuwa amekaa kwa muda mrefu katika nchi hiyo iliyo Asia na bado hakufahamu Kijapani vizuri. Hata hivyo, kila juma alienda nyumbani kwa yule kijana ili kuzungumzia Biblia. Kwa kutabasamu na kwa fadhili, alijibu kwa subira maswali mengi ambayo kijana huyo aliuliza.

Kijana yule hatasahau kamwe jinsi mmishonari huyo mzee-mzee alivyomtendea kwa fadhili. Kijana huyo alijiambia hivi: ‘Ikiwa Biblia inaweza kumfanya mtu awe mwenye fadhili na upendo hivyo, basi lazima nijifunze Biblia.’ Hilo lilimchochea atamani kujifunza jambo jipya kabisa. Ndiyo, fadhili hugusa moyo wa mwanadamu na kuuchochea kuliko hata maneno yenye nguvu.

Sifa Inayofunua Utu wa Mungu

Ni jambo la kawaida kwetu kuwatendea kwa fadhili watu ambao tuna uhusiano wa karibu nao, kwa sababu neno fadhili linamaanisha hasa uhusiano wa kiukoo. * Hata hivyo, kimsingi fadhili ni sifa inayotokana na Mungu. Yesu alisema kwamba Baba yake wa mbinguni si mwenye fadhili tu kwa wale wanaompenda bali pia kuelekea wale “wasio na shukrani.” Yesu aliwahimiza wafuasi wake wamwige Mungu kwa kuonyesha sifa hiyo: “Muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”​—Luka 6:35; Mathayo 5:48; Kutoka 34:6.

Wanadamu walioumbwa kwa mfano wa Mungu, wanaweza kuonyesha sifa ya fadhili. (Mwanzo 1:27) Ndiyo, tunaweza kumwiga Mungu na hata kuwaonyesha fadhili watu ambao hatuna uhusiano nao. Biblia inaeleza kwamba fadhili ni moja kati ya sifa zenye kuvutia za roho takatifu ya Mungu, au nguvu ya utendaji. (Wagalatia 5:22) Hivyo, mtu anaweza kuisitawisha anapoendelea kujifunza mengi kumhusu Mungu, ambaye ni Muumba, na kumkaribia zaidi.

Kwa kuwa wanadamu wameumbwa wakiwa na sifa ya fadhili na vilevile Mungu anaithamini sana, hivyo, ni jambo linalopatana na akili kwamba Mungu anatuambia: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi.” (Waefeso 4:32) Pia, tunakumbushwa hivi: “Msisahau ukaribishaji-wageni,” au kuwatendea kwa fadhili watu tusiowajua.​—Waebrania 13:2.

Katika ulimwengu wa leo usio na shukrani na ambao kwa kiwango kikubwa hauna fadhili, je, tunaweza kuwatendea wengine kwa fadhili, hata watu tusiowajua? Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo? Na kwa nini tupendezwe na sifa hiyo?

Sifa Muhimu Machoni pa Mungu

Inapendeza kuona kwamba baada ya mtume Paulo kuzungumza kuhusu kuwatendea kwa fadhili watu tusiowajua, aliongezea hivi: “Kupitia huo [ukaribishaji-wageni] watu wengine, bila wao wenyewe kujua, waliwakaribisha malaika.” Unaweza kuwazia jinsi ambavyo ungehisi ikiwa ungepewa nafasi ya kuwakaribisha malaika? Lakini kwanza Paulo anasema “bila wao wenyewe kujua.” Kwa maneno mengine, alimaanisha kwamba ikiwa tuna zoea la kuwatendea wengine kwa fadhili, kutia ndani watu tusiowajua kabisa, au hata watu ambao hatuwajui vizuri, huenda tukathawabishwa kwa njia tusizotazamia.

Tafsiri nyingi za Biblia zenye marejezo zinahusianisha maneno ya Paulo na masimulizi kuhusu Abrahamu na Loti yaliyo katika Mwanzo sura ya 18 na 19. Katika visa vyote viwili, tunasoma kuhusu malaika wakiwatokea wakiwa na ujumbe muhimu bila wanaume hao kuwatambua. Katika kisa cha Abrahamu, ujumbe ulihusu utimizo wa ahadi ya Mungu ya kumpa mwana, na katika kisa cha Loti, ujumbe ulihusu kukombolewa kutoka kwa uharibifu uliokuwa ukija juu ya majiji ya Sodoma na Gomora.​—Mwanzo 18:1-10; 19:1-3, 15-17.

Ukisoma maandiko yaliyotajwa hapo juu, utaona kwamba Abrahamu na Loti waliwatendea kwa fadhili wapita-njia ambao hawakuwafahamu. Bila shaka, katika nyakati za Biblia, ilikuwa wajibu na pia desturi kwa watu kuwakaribisha wasafiri na wapita-njia, iwe walikuwa marafiki, watu wa ukoo, au watu wasiojulikana. Hata Sheria ya Musa iliwaagiza Waisraeli wasipuuze mahitaji ya watu wasio Waisraeli katika nchi yao. (Kumbukumbu la Torati 10:17-19) Ingawa watu walikuwa na mazoea hayo, inaonekana kwamba Abrahamu na Loti walifanya mengi zaidi kuliko mambo yaliyokuja kuandikwa kwenye sheria baadaye. Walijitahidi isivyo kawaida kuwatendea kwa fadhili watu wasiowajua, na walibarikiwa kwa kufanya hivyo.

Matendo ya Abrahamu ya kuonyesha fadhili hayakumletea yeye mwenyewe tu baraka kwa vile alipata mwana, bali yalitufaidi sisi pia. Kwa njia gani? Abrahamu na mwanaye Isaka walitimiza sehemu muhimu sana katika utimizo wa kusudi la Mungu. Wakawa watu muhimu sana katika ukoo wa familia iliyotokeza yule Masihi, Yesu. Na maisha yao ya uaminifu yalionyesha kimbele jinsi ambavyo Mungu angeweka msingi wa kuwakomboa wanadamu kupitia upendo na fadhili zake zisizostahiliwa.​—Mwanzo 22:1-18; Mathayo 1:1, 2; Yohana 3:16.

Masimulizi hayo yanaonyesha wazi yale ambayo Mungu anatazamia kutoka kwa watu anaowaonyesha kibali na jinsi anavyothamini sifa ya fadhili. Haipaswi kamwe kupuuzwa bali ni sifa muhimu machoni pa Mungu.

Kuonyesha Fadhili Hutusaidia Kumjua Mungu Vizuri Zaidi

Biblia inasema kwamba katika siku zetu watu wengi wangekuwa “wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:1-3) Bila shaka, unakutana na watu kama hao kila siku. Hata hivyo, hiyo si sababu ya kutowatendea wengine kwa fadhili. Wakristo wanakumbushwa hivi: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote.”​—Waroma 12:17.

Tunaweza kujitahidi kuwa tayari kuwatendea wengine kwa fadhili. Biblia inasema: “Kila mtu ambaye hupenda . . . hupata kumjua Mungu,” na njia moja tunayoonyesha upendo ni kwa kuwatendea wengine kwa fadhili. (1 Yohana 4:7; 1 Wakorintho 13:4) Ndiyo, kwa kuwatendea wanadamu wenzetu kwa fadhili, tunapata kumjua Mungu vizuri zaidi na hilo linafanya tuwe na furaha hata zaidi. Yesu alisema hivi kwenye Mahubiri yake ya Mlimani: “Wenye furaha ni wenye fadhili, kwa kuwa wataonyeshwa fadhili. Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu.”​—Mathayo 5:7, 8, Young’s Literal Translation.

Usipokuwa na uhakika wa jambo unalopaswa kufanya au kusema katika hali fulani, sema au utende kwa fadhili

Fikiria mfano wa Aki, mwanamke kijana anayeishi Japani ambaye ameolewa na ana wavulana wawili. Baada ya kumpoteza mama yake kwa ghafula katika kifo, alishuka moyo sana. Nyakati nyingine, hali yake ilikuwa mbaya sana hivi kwamba alilazimika kumwona daktari. Kisha, familia fulani ikahamia katika eneo lao. Walikuwa wamempoteza baba yao muda mfupi uliokuwa umepita katika aksidenti, na mama yao alibaki na watoto wadogo watano. Aki aliihurumia familia hiyo na akajitahidi sana kuwa rafiki ya mama huyo na watoto wake. Alijitahidi alivyoweza kuisaidia familia hiyo kwa kuwapa chakula, mavazi ambayo familia yake haikuyahitaji, na vitu vingine, na hilo lilimsaidia Aki kurudia hali nzuri ya kihisia. Alijionea ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ndiyo, kuwatendea wengine kwa fadhili ndilo jambo bora zaidi unaloweza kujifanyia unaposhuka moyo.

‘Kumkopesha Yehova’

Si lazima mtu atumie pesa nyingi ili aonyeshe fadhili. Wala haitegemei uwezo wako au nguvu zako za kimwili. Tabasamu, maneno ya huruma, msaada, zawadi nzuri inayofaa, au hata kuwaruhusu wengine wakutangulie mnapokuwa kwenye foleni ni matendo ya fadhili. Usipokuwa na uhakika wa jambo unalopaswa kufanya au kusema katika hali fulani, sema au utende kwa fadhili. Kijana aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, aliguswa moyo sana na jinsi yule mmishonari mzee alivyomtendea kwa fadhili, sifa ambayo ilimchochea hata kuliko maneno ya mmishonari huyo. Basi, haishangazi kwamba takwa moja la Mungu kuwaelekea waabudu wake ni “kupenda fadhili”!​—Mika 6:8.

“Neno moja la fadhili linaweza kupasha joto miezi mitatu ya majira ya baridi kali.” Kama inavyoelezwa vizuri na msemo huo wa nchi za Mashariki, tendo moja la fadhili linaweza kuwa na matokeo makubwa. Tendo kama hilo linapofanywa kwa nia nzuri, na hasa linapochochewa na upendo wa mtu kuelekea Mungu, linaweza kuwaletea shangwe wale wanaohusika. Hata watu wasipothamini matendo yako ya fadhili, hilo halimaanishi kwamba umefanya kazi ya bure. Mungu anathamini matendo ya fadhili. Biblia inatuhakikishia kwamba tukiwatendea wengine kwa fadhili, ni kana kwamba ‘tunamkopesha Yehova.’ (Methali 19:17) Kwa nini usitafute nafasi za kuwatendea kwa fadhili watu walio karibu nawe?

^ fu. 5 Kamusi ya The Oxford English Dictionary inaonyesha kwamba maana ya awali ya neno “fadhili” ni “ukoo; uhusiano wa karibu; upendo wa asili unaotokana na uhusiano huo.”