Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomsaidia mwanamume fulani ambaye alikabiliana na hali ngumu utotoni awe baba na mume mwenye furaha na mafanikio? Ni nini kilichomchochea mwanamke aliyekuwa na mwenendo mbaya aache mazoea machafu? Soma mambo ambayo watu hao wanasema.

“Nilijihisi sifai.”​—VÍCTOR HUGO HERRERA

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1974

  • NCHI: CHILE

  • HISTORIA: MRAIBU WA POMBE

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika jiji la Angol, lililo katika eneo maridadi kusini mwa Chile. Sikuwahi kukutana na baba yangu. Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, mama yangu alihama pamoja nami na ndugu yangu na kwenda kwenye jiji kuu, Santiago. Tulianza kuishi katika chumba kidogo kilichokuwa kwenye eneo la mabanda lililotengewa watu wasio na makao. Tulitumia choo cha uma, na tulichota maji kwenye bomba la maji la wazima moto.

Baada ya miaka miwili hivi, serikali ilitupatia nyumba ndogo. Jambo la kusikitisha ni kwamba eneo hilo lilijaa watu waliotumia dawa za kulevya, walevi, wahalifu, na makahaba.

Siku moja mama yangu alikutana na mwanamume fulani na mwishowe wakaoana. Baba yangu wa kambo alikuwa mlevi kupindukia. Alitupiga mimi na mama yangu. Mara nyingi nililia nilipokuwa peke yangu, na nikatamani kuwa na baba wa kunilinda.

Ingawa mama yangu alifanya kazi kwa bidii ili kutuandalia, tulikuwa maskini sana. Tulipohisi njaa, nyakati nyingine tulilazimika kula maziwa ya unga na sukari. Ili kujitumbuiza, mimi na ndugu yangu tulikuwa tukijificha na kuchungulia kwenye dirisha la jirani yetu ili kutazama televisheni. Lakini siku moja alitushika na huo ndio uliokuwa mwisho wa zoea hilo!

Mara chache wakati ambapo baba yangu wa kambo hakuwa mlevi, alitununulia mimi na ndugu yangu kitu cha kula. Pindi fulani, alitununulia televisheni ndogo. Hiyo ni moja kati ya mara chache ambazo ninakumbuka nilipata furaha.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilijifunza kusoma. Mwaka mmoja baadaye, niliacha shule na nikaanza kufanya kazi ya wakati wote. Baada ya kazi, nilienda pamoja na wafanyakazi wenzangu ambao walikuwa watu wazima kwenye sherehe ambako tungelewa na kutumia dawa za kulevya. Baada ya muda, nikawa mraibu.

Nilipokuwa na umri wa miaka 20, nilikutana na Cati, na tukaoana. Mwanzoni, mambo yalienda vizuri, lakini baadaye nilirudia mazoea yangu ya zamani. Mwenendo wangu ukazidi kuwa mbaya zaidi. Mwishowe nikatambua kwamba ningeishia gerezani au kaburini. Jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba nilikuwa nikimfanya mwanangu Víctor ateseke jinsi nilivyoteseka nilipokuwa mtoto. Nilijihisi sifai, nikahuzunika, na kujikasirikia.

Karibu mwaka wa 2001, Mashahidi wawili wa Yehova walitutembelea nyumbani, na Cati akaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Alinieleza mambo aliyokuwa akijifunza. Nikitamani kujua mengi, mimi pia nilianza kujifunza Biblia. Mwaka wa 2003, Cati alibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Siku moja, nilisoma andiko la Ruthu 2:12, ambalo linasema kwamba Yehova huwathawabisha wale wanaotenda kwa imani, na kutafuta kimbilio kwake. Nilitambua kwamba ikiwa ningefanya mabadiliko, ningempendeza Mungu naye angenithawabisha. Niligundua jinsi Biblia inavyokataza ulevi tena na tena. Maneno yaliyo kwenye 2 Wakorintho 7:1 yalinigusa moyo sana. Andiko hilo linatuhimiza “tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.” Hivyo, nikaanza kuacha mazoea yangu mabaya. Nilipokuwa nikifanya hivyo, mwanzoni hasira yangu iliongezeka, lakini Cati hakuacha kamwe kunisaidia.

Hatimaye niliacha kazi yangu kwa sababu nilikabili mkazo mwingi wa kuvuta sigara na kunywa pombe. Ijapokuwa sikuwa na kazi kwa muda fulani, tuliishi kwa mapato kidogo, lakini nilipata muda mwingi zaidi wa kujifunza Biblia. Huo ndio wakati nilianza kufanya maendeleo ya kiroho. Cati hakudai mengi kamwe kuliko nilivyoweza kuandaa kimwili, wala hakunishtumu kwa sababu ya maisha yetu rahisi. Ninathamini kwelikweli msaada wake wenye upendo.

Pole kwa pole nikaanza kushirikiana kwa ukaribu zaidi na Mashahidi. Walinisaidia kuelewa kwamba ingawa sikuwa na elimu ya kilimwengu, Yehova alithamini tamaa yangu ya kutoka moyoni ya kumtumikia. Upendo na umoja tulioona katika kutaniko la Kikristo ulichochea sana familia yetu. Hatukuwa tumepata amani kama hiyo mahali pengine. Desemba mwaka wa 2004, mimi pia nikabatizwa.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Nimejionea ukweli wa maneno ya Yehova yaliyoandikwa katika Isaya 48:17, ambapo anasema: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.” Mama yangu na ndugu yangu walifurahi sana nilipofanya mabadiliko hivi kwamba sasa wao pia wanajifunza Biblia. Hata jirani zangu wanafurahi kuona jinsi nilivyobadilika na jinsi familia yetu ilivyo na furaha.

Nina mke anayempenda Mungu na ambaye ananiona kuwa rafiki na mwandamani wake mwenye kutegemeka. Ingawa sikumjua kamwe baba yangu, Biblia imenifundisha jinsi ya kuwalea wavulana wangu watatu. Wote wananiheshimu. Jambo la maana zaidi, wanamwona Yehova kuwa Mtu halisi, na wamesitawisha upendo kumwelekea.

“Ingawa sikumjua kamwe baba yangu, Biblia imenifundisha jinsi ya kuwalea wavulana wangu watatu”

Ninathamini sana kwamba ingawa nilikabiliana na hali ngumu utotoni, Yehova amenipa nafasi ya kuwa mwanamume mwenye furaha.

“Nikawa msichana mwenye hasira na mjeuri.”—NABIHA LAZAROVA

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1974

  • NCHI: BULGARIA

  • HISTORIA: MLANGUZI WA DAWA ZA KULEVYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa huko Sofia, Bulgaria, katika familia ambayo haikuwa tajiri sana. Baba yangu aliiacha familia yetu nilipokuwa na umri wa miaka sita. Jambo hilo lilinishtua sana, na likanisababishia uchungu mwingi wa kihisia. Nilihisi kwamba nimekataliwa na kwamba sifai kupendwa. Kadiri nilivyozidi kuwa mkubwa ndivyo hisia zangu zilivyozidi kunifanya niwe mwasi. Nikawa msichana mwenye hasira na mjeuri.

Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilitoroka nyumbani kwa mara ya kwanza. Mara kwa mara nilimwibia pesa mama yangu na pia babu na nyanya yangu. Nilipokuwa shuleni, mara nyingi nilipata matatizo kwa sababu ya hasira yangu kali, na hivyo, nilipelekwa kwenye shule tano tofauti-tofauti katika muda wa miaka michache tu. Miaka mitatu kabla ya kuhitimu, niliacha shule. Niliishi maisha mapotovu sana kiadili. Nikawa mraibu wa kuvuta sigara na bangi. Nilikunywa pombe kupindukia na kwenda kwenye sherehe kila wakati na pia, nilijihusisha na ulanguzi wa dawa za kulevya. Sikuona umuhimu wa kuishi katika ulimwengu wenye kukatisha tamaa ambamo watu huteseka na kufa. Hivyo, kila siku niliishi tu nikihangaikia kupata raha.

Mwaka wa 1998, nilipokuwa na umri wa miaka 24, nilikamatwa nikiwa kwenye uwanja wa ndege wa São Paulo, Brazili, ambako nilikuwa nikijihusisha na ulanguzi wa dawa za kulevya. Nilihukumiwa kifungo cha miaka minne gerezani.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwaka wa 2000, Mashahidi wa Yehova walianza kutembelea gereza letu mara moja kwa juma. Mmoja wa Mashahidi hao ambaye aliitwa Marines, alinitendea kwa fadhili sana. Alinichochea niwe na tamaa ya kutaka kujifunza mengi kuhusu Biblia. Kwa vile sikuwa nimewahi kusikia kuhusu Mashahidi wa Yehova, niliwauliza wafungwa wenzangu kuwahusu. Nilishangaa kwamba watu wengi niliowauliza walisema mambo mabaya kuwahusu Mashahidi. Mfungwa fulani aliniambia nijiunge na dini yoyote ile isipokuwa Mashahidi wa Yehova. Maneno yake yalinifanya niwe na tamaa ya kujua mengi zaidi; nilitaka kujua kwa nini watu hawa wanachukiwa sana. Baadaye nilielewa kwamba ni kwa sababu wao ni wafuasi wa dini ya kweli. Hata Biblia inasema kwamba kila mtu ambaye atamfuata Yesu kwa unyoofu atateswa.—2 Timotheo 3:12.

Wakati huo nilipangiwa kufanya kazi katika jengo la usimamizi la gereza. Siku moja nilipata masanduku fulani yaliyokuwa na magazeti ya zamani ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! * katika stoo. Nilienda na magazeti hayo kwenye seli yangu ya gereza na nikaanza kuyasoma. Kadiri nilivyozidi kuyasoma, ndivyo nilivyozidi kuhisi kama mtu mwenye kiu aliye jangwani ambaye amepata kisima cha maji safi. Kwa vile nilikuwa na wakati mwingi, nilijifunza Biblia kila siku kwa saa nyingi.

Siku moja niliitwa kwenye ofisi ya gereza. Nilitazamia kufunguliwa kutoka gerezani, hivyo nikakusanya haraka vitu vichache nilivyokuwa navyo, nikawaaga wafungwa wenzangu, na kukimbia ofisini. Hata hivyo, nilipofika huko, nilitambua kwamba nilikuwa nimefunguliwa mashtaka mapya ya kuwa na hati bandia. Matokeo ni kwamba nilihukumiwa kufungwa gerezani miaka mingine miwili.

Mwanzoni nilivunjika moyo. Ingawa niliona jambo hilo kuwa baya, mwishowe nilitambua kwamba kifungo hicho kingeniletea baraka. Nilikuwa nimejifunza mambo mengi kutoka katika Biblia, lakini moyoni mwangu bado nilitaka kuendelea na maisha yangu ya zamani baada ya kutoka gerezani. Nilihitaji muda zaidi ili nibadilike.

Wakati fulani nilihisi kwamba Mungu hangenikubali niwe mmoja wa waabudu wake. Lakini nilitafakari maandiko kama vile 1 Wakorintho 6:9-11. Andiko hilo linaonyesha kwamba katika karne ya kwanza W.K., Wakristo fulani walikuwa wezi, walevi, na wanyang’anyi kabla ya kuanza kumtumikia Yehova. Lakini kwa msaada wa Yehova, wakabadilika. Mfano wao ulinitia moyo sana.

Ilikuwa rahisi kuacha baadhi ya mazoea yangu machafu. Kwa mfano, haikuwa vigumu kuacha kutumia dawa za kulevya. Lakini ilikuwa vigumu zaidi kuacha kuvuta sigara. Hatimaye, baada ya mwaka mmoja nilifaulu kuacha zoea hilo. Jambo moja lililonisaidia ni kusoma kuhusu madhara ya kiafya ambayo mtu hupata kwa kuvuta sigara. Zaidi ya yote, kuendelea kusali kwa Yehova kulinisaidia kuacha zoea hilo.

“Nilitambua kwamba nilikuwa nimempata Baba bora zaidi, ambaye hangeniacha kamwe!”

Nilipozidi kumkaribia Yehova pole kwa pole niliacha kuhisi sipendwi, hisia ambazo nilikuwa nimepambana nazo baada ya baba yangu kutuacha. Maneno yaliyo katika Zaburi 27:10 yalipenya ndani ya moyo wangu. Mstari huo unasema: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” Nilitambua kwamba nilikuwa nimempata Baba bora zaidi, ambaye hangeniacha kamwe! Sasa maisha yangu yalikuwa na kusudi. Mnamo Aprili 2004, miezi sita baada ya kuachiliwa kutoka gerezani, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Sasa nina furaha. Niko huru kutokana na mazoea yenye kudhuru, ninafurahia afya nzuri kimwili na kihisia kuliko nilipokuwa na umri mdogo. Nina ndoa yenye furaha, na urafiki wa karibu pamoja na Baba yangu wa mbinguni, Yehova. Kati ya waabudu wake, nimepata watu wengi ambao ni kama baba, mama, na dada zangu. (Marko 10:29, 30) Ninathamini kwamba waliona ningeweza kubadilika hata kabla mimi mwenyewe sijatambua jambo hilo.

Nyakati nyingine, ninalemewa na hisia za kuwa na hatia kwa sababu ya maisha yangu ya zamani. Lakini ninafarijiwa kujua kwamba katika ulimwengu mpya ulioahidiwa, kumbukumbu mbaya ‘hazitakumbukwa akilini.’ (Isaya 65:17) Kwa sasa, mambo niliyojionea yananichochea kuwatendea kwa huruma watu wengine ambao wanakabiliana na matatizo kama hayo. Kwa njia hiyo, maisha yangu ya zamani yananisaidia. Kwa mfano, ninaposhiriki katika huduma ya Kikristo, ni rahisi zaidi kwangu kuzungumza na watumiaji wa dawa za kulevya, walevi, au majambazi bila kuwabagua. Nina hakika kwamba ikiwa nilifanikiwa kufanya mabadiliko ili nimpendeze Yehova, basi mtu yeyote anaweza!

^ fu. 29 Yanayochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

nilikuwa nimempata Baba bora zaidi, ambaye hangeniacha kamwe!”