Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | JE, MUNGU ANAKUJALI?

Mungu Anaweza Kukufariji

Mungu Anaweza Kukufariji

“Mungu, ambaye huwafariji wale walioshushwa chini, alitufariji.” —2 WAKORINTHO 7:6.

‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’WAGALATIA 2:20

KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Hata wanapohitaji faraja kwa hali na mali, baadhi ya watu hudhani haifai kuomba msaada kutoka kwa Mungu ili kukabiliana na matatizo yao. “Ninapofikiria idadi ya watu duniani—na matatizo wanayokabili,” anasema mwanamke aitwaye Raquel, “shida zangu huonekana kidogo sana zikilinganishwa na matatizo yao na hivyo mimi husita kumwomba Mungu msaada.”

BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Mungu amefanya mengi kuwasaidia na kuwafariji wanadamu. Wanadamu wote wamerithi dhambi, hivyo hakuna anayeweza kufuata viwango vya Mungu kikamili. Hata hivyo, Mungu “alitupenda akamtuma [Yesu Kristo] Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yohana 4:10) Kupitia kifo cha kidhabihu cha Yesu, Mungu amefanya iwezekane kwa wanadamu kupata msamaha wa dhambi, dhamiri njema, na tumaini la uzima wa milele katika ulimwengu mpya wenye amani. * Je, dhabihu hiyo ni kwa ajili ya wanadamu wote, au pia inaweza kukunufaisha wewe binafsi?

Mfikirie mtume Paulo. Alichochewa sana na dhabihu ya Yesu hivi kwamba akaandika: “Naishi kwa imani ambayo ni kumwelekea Mwana wa Mungu, aliyenipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.” (Wagalatia 2:20) Kwa kweli, Yesu alikufa kabla Paulo hajawa Mkristo. Hata hivyo, Paulo aliona dhabihu hiyo kuwa zawadi ya Mungu kwake binafsi.

Kifo cha kidhabihu cha Yesu ni zawadi ya kibinafsi kwako wewe pia. Zawadi hiyo inaonyesha jinsi Mungu anavyokuthamini. Inaweza kukupatia “faraja ya milele na tumaini jema” na hivyo ‘kukuimarisha wewe katika kila tendo na neno jema.’—2 Wathesalonike 2:16, 17.

Hata hivyo, Yesu alidhabihu uhai wake karibu miaka 2,000 iliyopita. Kuna uthibitisho gani kwamba Mungu anataka umkaribie leo?

^ fu. 5 Ili ujifunze mengi kuhusu dhabihu ya Yesu, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.