Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nikope Pesa?

Je, Nikope Pesa?

“Kukopa harusi; kulipa matanga.” —Methali ya Kiswahili.

MSEMO huo unajulikana sana na watu wa Afrika Mashariki, na bila shaka watu wengi ulimwenguni kote watakubaliana nao. Je, wewe huhisi hivyo kuhusu kukopa pesa? Hata ingawa huenda nyakati nyingine ukalazimika kukopa, unalionaje jambo hilo? Kuna hatari na mitego gani inayotokana na kukopa pesa?

Methali nyingine ya Kiswahili inayosisitiza hatari ya kukopa inasema hivi: “Kiharibucho urafiki ni kukopa na kuazima.” Kwa kweli, madeni yanaweza kuharibu uhusiano na urafiki. Hata kukiwa na mipango na nia nzuri kabisa, nyakati nyingine huenda matokeo yasiwe mazuri. Kwa mfano, ukichelewa kulipa deni huenda yule aliyekukopesha akakasirika. Huenda hata akaanza kuwa na kinyongo, na uhusiano kati yako na yeye na hata kati ya familia zenu ukadhoofika. Kwa kuwa mikopo inaweza kuwa chanzo cha kutoelewana, basi isingefaa tukimbilie kukopa ili tu kusuluhisha tatizo fulani la kifedha.

Pia, kukopa pesa kunaweza kuhatarisha uhusiano wa mtu na Mungu. Jinsi gani? Kwanza kabisa, Biblia inasema kwamba mtu anayekataa kimakusudi kulipa madeni yake ni mwovu. (Zaburi 37:21) Vilevile inaeleza wazi kwamba “mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.” (Methali 22:7) Ni lazima mkopaji atambue kwamba ana wajibu wa kurudisha pesa alizokopa. Pia kuna usemi mwingine wa Kiafrika unaosema: “Ukiazima miguu ya mtu, utaenda popote anapotaka uende.” Usemi huo unamaanisha kwamba mtu mwenye madeni hana uhuru wa kufanya mambo anayopenda.

Kwa hiyo, unapokopa unapaswa kuona kwamba kulipa deni lako ni jambo muhimu sana. La sivyo, huenda matatizo yakatokea. Madeni chungu nzima yanaweza kumfanya mtu apatwe na mkazo, akose usingizi, afanye kazi kupita kiasi, agombane na mume au mke wake, na hata yanaweza kusababisha kuvunjika kwa familia, kutia ndani kesi au kufungwa gerezani. Zingatia hekima inayopatikana kwenye andiko la Waroma 13:8: “Msiwe na deni la hata jambo  moja la mtu yeyote, isipokuwa kupendana.”

JE, NI LAZIMA NIKOPE?

Mambo tuliyotaja yanaonyesha kwamba ni lazima tuwe waangalifu tunapotaka kukopa pesa. Ni jambo la busara kujiuliza hivi: Je, kweli ninahitaji kukopa? Je, ninakopa pesa kwa sababu ninazihitaji ili nitunze familia yangu? Je, ni kwa sababu ya pupa, au labda ni tamaa ya kuishi zaidi ya mapato yangu? Mara nyingi, ni afadhali kuridhika na vitu vichache kuliko kukopa.

Bila shaka, wakati mwingine unaweza kukopa dharura inapotokea au inapoonekana hakuna la kufanya. Hata hivyo, ikiwa unaamua kukopa, unapaswa kuwa mnyoofu na mwaminifu. Unawezaje kufanya hivyo?

Kwanza, si vema kutolipa deni eti kwa sababu aliyekukopesha ana pesa au vitu vingi kuliko wengine. Hatupaswi kufikiri kwamba mtu anapokuwa tajiri, ni lazima atusaidie kifedha. Wala kufikiri kwamba hatupaswi kumlipa deni lake. Usiwaonee wivu matajiri.—Methali 28:22.

Kisha, hakikisha kwamba unalipa deni, na ufanye hivyo kwa wakati. Ikiwa mkopeshaji hakuambii tarehe hususa ya kulipa deni, pendekeza tarehe na ulipe kwa wakati mliokubaliana. Inapendekezwa kwamba mwandike makubaliano yenu ili mwepuke kutoelewana. (Yeremia 32:9, 10) Ikiwezekana, unapotaka kulipa deni nenda wewe mwenyewe kwa aliyekukopesha ili upate nafasi ya kumshukuru. Kulipa deni kwa wakati mliokubaliana hudumisha uhusiano. Katika Mahubiri yake ya Mlimani Yesu alisema hivi: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.” (Mathayo 5:37) Kwa kuongezea, sikuzote kumbuka kanuni hii muhimu: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

KANUNI ZA BIBLIA ZINAZOWEZA KUKUSAIDIA

Biblia inatusaidia kuepuka tamaa ya kukopa pesa. Inasema hivi: “Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu.” (1 Timotheo 6:6) Kwa maneno mengine, kuridhika na kile ambacho mtu anacho ni njia bora ya kuepuka matokeo yenye kuhuzunisha ya kukopa. Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu kuridhika katika ulimwengu wa leo ambapo watu hutiwa moyo watosheleze tamaa zao papo kwa hapo. Tunahitaji kuwa na sifa ya “ujitoaji kimungu.” Jinsi gani?

Kwa mfano, wafikirie mume na mke fulani Wakristo huko Asia. Walipokuwa vijana, walitamani kumiliki nyumba kama wengine. Kwa hiyo, waliamua kutumia akiba yao, wakakopa pesa benki na kwa watu wa ukoo ili wanunue nyumba. Hata hivyo, baada ya muda mfupi walianza kulemewa na madeni makubwa waliyokuwa wakilipa kila mwezi. Walitafuta kazi ya ziada, wakafanya kazi kwa saa nyingi, jambo lililowafanya wabaki na muda kidogo tu wa kuwa na watoto wao. Mume anasema hivi: “Mkazo, maumivu, na kukosa usingizi kulinikosesha amani na utulivu. Nilihisi nimelemewa.”

“Kuwa na usawaziko na kufuata ushauri wa Biblia kuhusu vitu vya kimwili ni ulinzi”

Baada ya muda, walikumbuka maneno ya andiko la 1 Timotheo 6:6 na wakaamua kwamba suluhisho pekee ni kuuza nyumba hiyo. Ilichukua miaka miwili ili kuwa huru kutokana na madeni yao. Walijifunza nini kutokana na mambo yaliyowapata? Hatimaye walisema hivi: “Kuwa na usawaziko na kufuata ushauri wa Biblia kuhusu vitu vya kimwili ni ulinzi.”

Watu wengi wanaijua methali ya Kiswahili iliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Hata hivyo, methali hiyo haijawafanya watu waache kukopa. Kwa sababu ya kanuni za Biblia tulizochunguza, je, halingekuwa jambo la hekima kufikiria kwa makini kuhusu swali hili, Je, nikope pesa?