Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, elimu ya vitu vya kale inaunga mkono Biblia?

Sargoni wa Pili, Mfalme wa Ashuru anayetajwa katika Isaya 20:1

Makala iliyochapishwa katika gazeti la Biblical Archaeology Review, ilisema kwamba kuwapo kwa watu “50 hivi” wanaotajwa katika Maandiko ya Kiebrania, kunaweza sasa kuthibitishwa na ugunduzi uliofanywa na wachimbuzi wa vitu vya kale. Watu hao hutia ndani wafalme 14 wa Yuda na Israeli kama Daudi na Hezekia, na wengine wasiojulikana sana kama vile Menahemu na Peka. Orodha hiyo inataja pia Mafarao 5 na wafalme 19 wa Ashuru, Babilonia, Moabu, Uajemi, na Siria. Hata hivyo, si watawala tu wanaotajwa katika Biblia na maandishi ya wachimbuzi wa vitu vya kale. Wengine wanaotajwa wanatia ndani watu waliokuwa na vyeo vya kadiri kama vile makuhani wakuu, mwandishi, na maofisa kadhaa.

Makala hiyo inasema kwamba “kuna uthibitisho mkubwa unaokubaliwa na wasomi” unaotambulisha waziwazi watu hao waliotajwa. Ni kweli kwamba Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanarejelea watu wengi wanaotajwa katika historia, na uthibitisho wa wachimbuzi wa vitu vya kale unaounga mkono kuwapo kwa baadhi yao kama vile Herode, Pontio Pilato, Tiberio, Kayafa, na Sergio Paulo.

Simba walioishi katika nchi zinazotajwa katika Biblia walianza kutoweka pindi gani?

Michoro iliyokuwa katika kuta za matofali yenye kung’aa katika Babiloni la kale

Ingawa hakuna simba katika maeneo yenye msitu ya Nchi Takatifu leo, maandiko yanarejelea mnyama huyo mara 150 hivi, kuonyesha kwamba waandishi wa Biblia walimjua mnyama huyo. Marejeo mengi yanatumia lugha ya mfano, hata hivyo baadhi ya masimulizi yanataja kuhusu mapambano pamoja na simba. Kwa mfano, Samsoni, Daudi, na Benaya wanasifiwa kwa sababu ya kuua simba. (Waamuzi 14:5, 6; 1 Samweli 17:34, 35; 2 Samweli 23:20) Watu wengine wanatajwa kwamba waliuawa na simba.1 Wafalme 13:24; 2 Wafalme 17:25.

Katika nyakati za kale, simba wa Asia (Panthera leo persica) walipatikana Asia Ndogo na Ugiriki mpaka Palestina, Siria, Mesopotamia, na kaskazini-magharibi mwa India. Wanyama hao waliheshimiwa na kuogopwa sana, na mara nyingi walionekana katika michoro ya sanaa za kale za Mashariki. Michongo ya picha za simba iliyokuwa katika kuta za matofali yenye kung’aa ilipamba Njia ya Maandamano ya Babiloni la kale.

Kufikia mwishoni mwa karne ya 12 W.K., inasemekana kwamba wapiganaji wa vita vitakatifu waliendelea kuwinda simba huko Palestina. Inaonekana kwamba simba walianza kutoweka katika eneo hilo muda mfupi baada ya mwaka wa 1300. Hata hivyo, inasemekana kwamba baadhi ya simba walipatikana Mesopotamia na Siria kufikia karne ya 19, pia Iran na Iraki kufikia katikati ya karne ya 20.