Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inasema Nini Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Wakati Wetu Ujao?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Wakati Wetu Ujao?

 “Hali ya hewa imekuwa mbaya sana hivi kwamba tayari dunia haikaliki tena.”​—Gazeti The Guardian.

 Wanadamu wanakabili janga ambalo wamejisababishia wenyewe. Wanasayansi wengi wanakubali kwamba utendaji wa wanadamu ndio umesababisha kuongezeka kwa kiwango cha joto duniani. Kuongezeka huko kwa joto kumebadili hali ya hewa na kutokeza madhara makubwa. Madhara hayo yanatia ndani yafuatayo:

  •   Mambo kama vile kupanda sana kwa joto, ukame, na dhoruba hutokea mara nyingi, nayo hutokeza mafuriko zaidi na mioto mingi zaidi ya misitu.

  •   Kuyeyuka kwa miamba ya barafu na barafu ya Aktiki.

  •   Kupanda kwa kiwango cha maji baharini.

 Matatizo ya hali ya hewa yameathiri kila sehemu ya dunia. Baada ya kufafanua hali zilivyo katika nchi 193, ripoti moja katika gazeti New York Times ilisema hivi: “Dunia inatutumia ujumbe wa kuomba msaada.” Kwa sababu ya vifo na kuteseka ambako kumesababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa, Shirika la Afya Ulimwenguni lilisema mabadiliko ya hali ya hewa ndiyo “hatari kubwa zaidi ya afya inayokabili wanadamu.”

 Hata hivyo, tuna sababu nzuri ya kuwa na tumaini kwa ajili ya wakati ujao. Biblia ilitabiri mambo ambayo tunaona yakitukia leo, kutia ndani sababu inayotufanya tutazamie kwamba Mungu atatenda, na kile ambacho atafanya ili kulinda wakati wetu ujao.

Je, kubadilika kwa hali ya hewa kunatimiza unabii wa Biblia?

 Ndiyo. Matatizo ya hali ya hewa yanayosababishwa na kuongezeka kwa kiwango cha joto duniani yanapatana na mambo ambayo Biblia ilitabiri yangetokea katika siku zetu.

 Unabii: Mungu ‘atawaangamiza wale wanaoiangamiza dunia.’​—Ufunuo 11:18, maelezo ya chini.

 Biblia ilitabiri kuhusu wakati ambapo matendo ya wanadamu yangekaribia kuiangamiza dunia. Kwa sababu ya kuongezeka kwa kiwango cha joto duniani, watu leo wanaiharibu dunia kwa kiwango kikubwa sana.

 Unabii huu unaonyesha sababu moja kwa nini hatuwezi kuwatazamia wanadamu waiokoe dunia. Ona kwamba Mungu atachukua hatua wakati ambapo watu watakuwa ‘wakiiangamiza dunia.’ Maendeleo yoyote ambayo watu wenye nia nzuri wanafanya katika pambano dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa, hayatatosha kuwazuia wanadamu wasiiharibu dunia.

 Unabii: “Kutakuwa na mambo yenye kuogopesha.”​—Luka 21:11.

 Biblia ilitabiri kwamba “mambo yenye kuogopesha” yangetokea katika siku zetu. Mabadiliko ya hali ya hewa yametokeza matukio yenye kutisha ya hali ya hewa duniani pote. Leo, watu fulani wameathiriwa na wasiwasi mwingi kwamba wataangamia kwa sababu ya uharibifu wa mazingira.

 Unabii: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasio washikamanifu, . . . wasiotaka makubaliano yoyote, . . . wasaliti, wenye vichwa vigumu.”​—2 Timotheo 3:1-4.

 Biblia ilitabiri tabia ambazo zimetokeza matatizo ya hali ya hewa. Serikali na biashara zimetanguliza faida za kifedha badala ya kufikiria hali itakuwaje kwa ajili ya watu wakati ujao. Hata wanapojaribu kushirikiana, hawawezi kukubaliana kuhusu hatua zinazohitajika ili kuzuia kuongezeka kwa kiwango cha joto duniani.

 Unabii huo unaonyesha kwamba hatupaswi kutazamia kwamba watu kwa ujumla watabadili matendo yao na kuilinda dunia. Badala yake, Biblia inasema kwamba watu wanaoonyesha sifa za kichoyo “wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.”​—2 Timotheo 3:13.

Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatenda?

 Biblia inafunua kwamba Yehova a Mungu, Muumba wetu, anaijali sana sayari yetu na wale wanaoishi ndani yake. Fikiria mistari mitatu tu ya Biblia inayoonyesha kwamba Mungu atatenda.

  1.  1. Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu, lakini aliiumba ili ikaliwe.”​—Isaya 45:18.

     Mungu atatimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia. (Isaya 55:11) Hata iruhusu iharibiwe au watu wasiweze kuishi ndani yake.

  2.  2. “Lakini wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani. Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.”​—Zaburi 37:11, 29.

     Mungu anaahidi kwamba wanadamu wataishi duniani milele chini ya hali zenye amani.

  3.  3. “Lakini waovu, wataangamizwa kutoka duniani.”​—Methali 2:22.

     Mungu anaahidi kuwaondoa wale wanaoendelea kutenda maovu, kutia ndani wale wanaoiharibu dunia.

Mambo ambayo Mungu atafanya wakati ujao

 Mungu atatimizaje ahadi zake kwa dunia? Atatumia serikali ya ulimwenguni pote inayoitwa Ufalme wa Mungu. (Mathayo 6:10) Ufalme huo utatawala kutoka mbinguni. Hautahitaji kufanya mikataba na serikali za wanadamu kuhusu masuala yanayohusu dunia na mazingira. Badala yake, Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali za wanadamu.​—Danieli 2:44.

 Ufalme wa Mungu utatenda mambo yenye kupendeza kwa ajili ya wanadamu wote na kwa ajili ya dunia. (Zaburi 96:10-13) Fikiria kile ambacho Yehova Mungu atafanya kupitia Ufalme wake.

  •   Atarekebisha mazingira

     Biblia inasema nini? “Nyika na nchi iliyokauka zitafurahi, na jangwa tambarare litashangilia na kuchanua maua kama zafarani.”​—Isaya 35:1.

     Hilo litamaanisha nini kwa ajili ya wakati wetu ujao? Yehova ataponya sayari yetu, hata katika maeneo ambayo imeharibiwa vibaya na wanadamu.

  •   Atadhibiti hali mbaya sana ya hewa

     Biblia inasema nini? “[Yehova] huituliza dhoruba ya upepo; Mawimbi ya bahari hunyamaza.”​—Zaburi 107:29.

     Hilo litamaanisha nini kwa ajili ya wakati wetu ujao? Yehova ana nguvu za kudhibiti hali za asili. Watu hawataathiriwa tena na hali mbaya sana ya hewa.

  •   Atawafundisha wanadamu kuitunza dunia

     Biblia inasema nini? “Nitakupa ufahamu na kukufundisha njia unayopaswa kufuata.”​—Zaburi 32:8.

     Hilo litamaanisha nini kwa ajili ya wakati wetu ujao? Yehova aliwapa wanadamu daraka la kuitunza dunia. (Mwanzo 1:28; 2:15) Atawafundisha njia bora zaidi ya kutimiza jukumu hilo la kutunza uumbaji wake, na kuishi kwa njia ambayo haitadhuru mazingira.

a Yehova ndilo jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye “Yehova Ni Nani?