Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Watu Milioni 6 Wamekufa Kutokana na COVID—Biblia Inasema Nini?

Watu Milioni 6 Wamekufa Kutokana na COVID—Biblia Inasema Nini?

 Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), kufikia Mei 23, 2022, tayari watu milioni 6.27 wamekufa ulimwenguni pote kutokana na COVID-19. Hata hivyo, kulingana na ripoti iliyochapishwa Mei 5, 2022, shirika hilo lilisema kwamba huenda idadi ya vifo ikawa kubwa zaidi kuliko ilivyokadiriwa. Shirika hilo pia lilisema kwamba katika mwaka wa 2020 na 2021, “idadi kamili ya watu waliokufa moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kutokana na janga la COVID-19 . . . inakadiriwa kuwa milioni 14.9.” Je, Biblia inasema jambo lolote kuhusu magonjwa hayo ya mlipuko?

Biblia ilitabiri kungekuwa na magonjwa hatari ya kuambukiza

  •    Yesu alitabiri kwamba kungekuwa na maradhi, au “magonjwa ya kuambukiza,” katika kipindi kinachoitwa “siku za mwisho.”​—Luka 21:11; 2 Timotheo 3:1, Habari Njema Kwa Watu Wote.

 Unabii huo wa Yesu unatimizwa leo. Ili kujifunza mengi zaidi, soma makala “Ni Nini Ishara ya ‘Siku za Mwisho’ au ‘Nyakati za Mwisho’?”

Biblia inatoa faraja

  •    “Mungu wa faraja yote . . . hutufariji katika majaribu yetu yote.”​—2 Wakorintho 1:3, 4.

 Wengi ambao wamefiwa na wapendwa wao wamepata faraja kupitia ujumbe wa Biblia. Jifunze mengi zaidi katika makala “Huzuni ya Kufiwa​—Jinsi ya Kukabiliana Nayo” na “Kitabu Kinachotoa Ushauri Bora Na Faraja.”

Biblia inatoa suluhisho la kudumu

  •    “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”​—Mathayo 6:10.

 Hivi karibuni “Ufalme wa Mungu” utahakikisha kwamba “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Marko 1:14, 15; Isaya 33:24) Tazama video Ufalme wa Mungu Ni Nini? ili ujue mengi zaidi kuhusu serikali hiyo ya mbinguni na mambo itakayofanya.

 Tunakukaribisha ujifunze mengi zaidi kuhusu Biblia ili wewe na familia yako mnufaike kutokana na hekima yake na ahadi nzuri inazotoa kuhusu wakati ujao.