Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini Bora la Wakati Ujao

Tumaini Bora la Wakati Ujao

 Je, unafikiri kwamba hali zitakuwa bora wakati ujao? Watu wengi wanajaribu kuwa na mtazamo unaofaa licha ya matatizo mengi tunayokabili leo. Hata hivyo, je, kweli tunaweza kutazamia kwamba hali zitakuwa bora? Ndiyo! Biblia inatupatia tumaini lenye kutegemeka kwamba kutakuwa na wakati ujao ulio bora.

 Biblia inatoa tumaini gani?

 Biblia inaonyesha wazi kwamba wanadamu wanakabili matatizo makubwa sana. Hata hivyo, inaahidi kwamba matatizo hayo hayataendelea milele. Fikiria mifano michache hususa.

  •   Tatizo: Ukosefu wa makazi

     Biblia inasema nini: “Watajenga nyumba na kuishi ndani yake.”—Isaya 65:21.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Watu watamiliki nyumba zao wenyewe.

  •   Tatizo: Ukosefu wa kazi na umaskini

     Biblia inasema nini: “Watu wangu niliowachagua watafurahia kikamili kazi ya mikono yao.”—Isaya 65:22.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Wanadamu wote watafurahia kufanya kazi yenye kuridhisha na kuthawabisha.

  •   Tatizo: Ukosefu wa haki

     Biblia inasema nini: “Wakuu watatawala kwa haki.”—Isaya 32:1.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Watu hawatatendewa isivyo haki kwa kubaguliwa kwa sababu ya rangi, cheo, na hali yao ya kiuchumi. Kila mtu atatendewa kwa haki.

  •   Tatizo: Utapiamlo na Njaa

     Biblia inasema nini: “Kutakuwa na nafaka nyingi duniani; itafurika juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Kila mtu ataweza kupata chakula cha kutosha kilicho na lishe. Hakuna mtu yeyote atakayelala njaa au kuwa na utapiamlo.

  •   Tatizo: Uhalifu na jeuri

     Biblia inasema nini: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.”—Mika 4:4.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Kila mtu atakuwa salama kwa sababu watu waovu hawatakuwepo tena, na “waadilifu wataimiliki dunia.”—Zaburi 37:10, 29.

  •   Tatizo: Vita

     Biblia inasema nini: “Taifa halitainua upanga dhidi ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Dunia nzima itakuwa na amani. (Zaburi 72:7) Hakutakuwa na mtu yeyote atakayehuzunika kwa sababu ya kufiwa na mpendwa wake katika vita au atakayekuwa mkimbizi kwa sababu ya vita.

  •   Tatizo: Magonjwa na maradhi

     Biblia inasema nini: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Watu hawatateseka tena kwa sababu ya ulemavu au magonjwa. (Isaya 35:5, 6) Biblia hata inaahidi kwamba “kifo hakitakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

  •   Tatizo: Uharibifu wa mazingira

     Biblia inasema nini: “Nyika na nchi iliyokauka zitafurahi, na jangwa tambarare litashangilia na kuchanua maua kama zafarani.”—Isaya 35:1.

     Inachomaanisha kuhusu wakati ujao: Dunia yote itakuwa paradiso ili wanadamu waweze kuishi kama Mungu alivyokusudia mwanzoni.—Mwanzo 2:15; Isaya 45:18.

 Je, kweli tumaini hilo la Biblia litatimizwa?

 Huenda ukahisi halitatimizwa. Hata hivyo, tunakutia moyo uchunguze zaidi maoni ya Biblia kuhusu wakati ujao. Kwa nini? Ahadi zinazopatikana katika Biblia ni tofauti na ahadi na utabiri unaotolewa na watu. Ahadi zinazopatikana katika Biblia zinatoka kwa Mungu. Ona sababu zinazofanya jambo hilo kuwa la pekee:

  •   Mungu anategemeka. Biblia inasema kwamba Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Kwa kuongezea, ni Mungu tu aliye na uwezo wa kutabiri mambo yatakayotokea wakati ujao. (Isaya 46:10) Biblia ina mifano mingi inayothibitisha kwamba mambo anayotabiri Mungu sikuzote hutimizwa. Kwa habari zaidi, tazama video Tunawezaje Kuwa na Hakika Kwamba Yale Yaliyoandikwa Katika Biblia Ni ya Kweli?

  •   Mungu ana nguvu za kuondoa matatizo yetu. Biblia inasema kwamba Mungu ana nguvu za ‘kufanya kila jambo apendalo.’ (Zaburi 135:5, 6) Kwa maneno mengine, hakuna chochote kitakachomzuia Mungu kutimiza ahadi zake. Kwa kuongezea, Mungu anataka kutusaidia kwa sababu anatupenda.—Yohana 3:16.

 Huenda ukajiuliza, ‘ikiwa Mungu anataka kutusaidia na ana nguvu za kutusaidia, kwa nini bado tunapata matatizo mengi?’ Ili kujibu swali hilo, tazama video Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka?

 Tumaini hilo litatimizwaje?

 Mungu atatumia Ufalme wake, serikali iliyo mbinguni, ili kutimiza ahadi zake. Amemweka rasmi Yesu Kristo kuwa Mtawala wa Ufalme huo, na amempa mamlaka ya kutunza dunia na watu watakaoishi ndani yake. Yesu alipokuwa duniani, aliponya wagonjwa, alilisha wenye njaa, alidhibiti hali mbaya za hewa, na hata aliwafufua wafu. (Marko 4:39; 6:41-44; Luka 4:40; Yohana 11:43, 44) Hivyo, alionyesha kile atakachofanya akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu.

 Tazama video Ufalme wa Mungu Ni Nini? ili ujifunze mengi zaidi kuhusu jinsi Ufalme wa Mungu utakavyokunufaisha.

 Tumaini hilo litatimizwa lini?

 Hivi karibuni! Tunawezaje kuwa na uhakika? Biblia ilitabiri matukio yatakayoonyesha kwamba Ufalme wa Mungu unakaribia kuanza kutawala duniani. (Luka 21:10, 11) Hali za sasa duniani zinafanana na mambo ambayo Biblia ilitabiri.

 Ili kujifunza mengi zaidi, soma makala “Ufalme wa Mungu Utaanza Kutawala Dunia Lini?

 Tumaini linalotolewa katika Biblia linaweza kukusaidiaje leo?

 Mwandishi mmoja wa Biblia alifananisha tumaini linalotolewa katika Biblia na “nanga ya nafsi.” (Waebrania 6:19) Sawa na nanga inayoshikilia meli isitikisike wakati wa dhoruba, tumaini hakika la Biblia la wakati ujao linaweza kutusaidia kuvumilia matatizo tunayokabili leo. Tumaini letu linaweza kulinda na kuimarisha akili na hisia zetu, na hata afya yetu ya kimwili.—1 Wathesalonike 5:8.