Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MICHANGO YAKO INAVYOTUMIWA

Maandishi ya Vipofu Yanabadili Maisha

Maandishi ya Vipofu Yanabadili Maisha

OKTOBA 1, 2021

 Toleo la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1912 lilisema hivi: “Huenda wengi wa wasomaji wetu wanawafahamu watu ambao ni vipofu. . . . Wanaweza kupata machapisho ya kusoma bila malipo . . . . Machapisho hayo hutolewa katika herufi zilizoinuliwa ambazo vipofu wanaweza kusoma.” Gazeti hilo lilisema hivi pia: “Vipofu wengi wanathamini sana ujumbe kwamba baraka za pekee zitakuja ulimwenguni.”

 Maneno hayo yalipoandikwa, nchi ambazo hazizungumzi Kiingereza zilikuwa na mfumo tofauti wa kuandika maandishi ya vipofu. Hata hivyo, tayari Mashahidi wa Yehova walikuwa wakisambaza kweli za Biblia katika maandishi ya vipofu. Na bado tunafanya hivyo hadi leo! Sasa machapisho katika lugha hiyo yanapatikana katika zaidi ya lugha 50. Yanatokezwaje?

Herufi hufanyizwa kwa kitufe kimoja hadi sita vilivyoinuliwa. Vitufe vilivyoinuliwa hupangwa katika sehemu sita hususa

Kuandika na Kutia Nakshi

 Hatua ya kwanza ya kutokeza maandishi ya vipofu ni kuandika herufi zote katika maandishi hayo. Michael Millen anayefanya kazi katika Idara ya Huduma za Kutokeza Maandishi iliyoko Patterson, New York anaeleza hivi: “Zamani tulitumia programu zilizotokezwa na kampuni za kibiashara ili kutokeza maandishi ya vipofu, lakini hazikuweza kutokeza lugha zote tulizohitaji. Sasa tunatumia Mfumo wa Watchtower wa Kutafsiri (Watchtower Translation System), unayoweza kutokeza maandishi ya vipofu katika lugha nyingi ulimwenguni. Sidhani kuna programu nyingine kama hiyo ulimwenguni.”

 Mbali tu na kuwa na maandishi, machapisho ya maandishi ya vipofu yana ufafanuzi wa picha zilizo katika chapisho. Kwa mfano, picha iliyo kwenye jalada la toleo la maandishi ya vipofu la Furahia Maisha Milele! linafafanuliwa hivi: “Mwanamume anaanza kutembea kwenye kijia kilichojipinda kilichozungukwa na mimea na milima maridadi.” Jamshed, mtumishi wa huduma na painia ambaye ni kipofu anasema hivi: “Ufafanuzi wa picha hizo ni muhimu sana kwangu.”

 Baada ya herufi zote kuandikwa, faili hutumwa kwenye ofisi za tawi zinazofanyiza herufi zinazoweza kusomwa kwa kupapasa chapisho lenyewe. Kwenye ofisi hizo herufi hizo zilizo kama vitufe vidogo vilivyoinuka hushindiliwa kwenye karatasi ngumu ambayo haipasuki wala ambayo haiwezi kupoteza umbo la vitufe hivyo licha ya kutumiwa mara nyingi. Kisha karatasi za chapisho zima hukusanywa, kuunganishwa, na kusafirishwa pamoja na upakizi wa kawaida wa machapisho ya kutaniko au kwa kutumia posta ikiwa kuna “mfumo wa usafirishaji wa bila malipo kwa ajili ya vipofu.” Inapohitajika, ofisi za tawi hupanga usafirishaji wa haraka ili ndugu ambao ni vipofu wapate machapisho wanayohitaji kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.

 Kazi yote hiyo inatumia muda na pesa nyingi sana. Kwa kweli, kiwanda cha uchapishaji cha Wallkill, New York, hutokeza Biblia 50,000 za kawaida katika muda unaotumiwa kutokeza Biblia 2 tu za maandishi ya vipofu. Kila Biblia ya daraja la pili la maandishi ya vipofu ya Kiingereza ina mabuku 25, na vifaa vinavyohitajika kutokeza mabuku hayo hugharimu mara 123 zaidi ya pesa zinazohitajika kutokeza Biblia ya kawaida. a Majalada tu ya mabuku 25 yanayofanyiza Biblia moja hugharimu dola 150 hivi (za Marekani)!

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya maandishi ya vipofu ya Kiingereza daraja la pili imefanyizwa kwa mabuku 25!

 Wale wanaosaidia kutokeza machapisho ya maandishi ya vipofu wanahisije kuhusu kazi yao? Nadia, anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Afrika Kusini anasema hivi: “Ndugu na dada zetu vipofu wana maisha magumu, kwa hiyo ni baraka kwangu kutengeneza kitu kitakachowasaidia. Ni wazi kwamba Yehova anawapenda sana.”

Learn to Read Braille

 Lakini vipi ikiwa kipofu hajui kusoma maandishi ya vipofu? Miaka michache iliyopita, tulitoa broshua yenye kichwa Learn to Read Braille ambayo ina maandishi ya kawaida na yaliyochapishwa. Imekusudiwa itumiwe na mtu anayeweza kuona pamoja na kipofu. Broshua hiyo ni sehemu ya upakizi ulio na vifaa ambavyo kipofu anaweza kutumia kuandika maandishi ya vipofu. Mwanafunzi wa maandishi ya vipofu hutumia vifaa hivyo kujiandika kila herufi ya maandishi ya vipofu. Mazoezi hayo ya kuandika yatamsaidia mwanafunzi kukumbuka kila herufi na kuitambua anapoigusa.

“Nimekuwa ‘Mraibu’ Kabisa”

 Ndugu na dada vipofu wamenufaikaje kutokana na machapisho hayo? Ernst, anayeishi nchini Haiti, alikuwa akihudhuria mikutano ya kutaniko, lakini hakuwa na machapisho yoyote ya maandishi ya vipofu. Kwa sababu hiyo, alilazimika kutegemea kumbukumbu yake anapotoa migawo ya wanafunzi na anapotoa maelezo wakati wa sehemu za maswali na majibu. Anasema hivi: “Lakini sasa ninaweza kunyoosha mkono na kutoa maelezo wakati wowote. Ninajihisi nikiwa na umoja na ndugu na dada zangu. Sote tunapokea chakula kilekile cha kiroho!”

 Jan, mzee ambaye ana matatizo ya kuona nchini Austria na ambaye huongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Biblia la Kutaniko anasema hivi: “Machapisho yetu yako wazi kabisa kuliko machapisho mengine ya maandishi ya vipofu ambayo nimewahi kusoma. Kwa mfano, tuna namba za ukurasa, maelezo ya chini ambayo ni rahisi kupata, na ufafanuzi hususa wa picha.”

 Seon-ok, painia nchini Korea Kusini, ni kipofu na kiziwi. Zamani alitegemea mtu amtolee ishara kwenye mikono yake wakati wa mikutano, lakini sasa anaweza kusoma machapisho ya kujifunzia Biblia katika maandishi ya vipofu. Anasema hivi: “Inaweza kuwa vigumu kusoma machapisho mengine ya maandishi ya vipofu kwa sababu huenda vitufe fulani vikawa vinakosekana, mistari haijajipanga vizuri, au karatasi ni nyembamba sana. Lakini Mashahidi wa Yehova hutumia karatasi bora kabisa na wanatokeza vitufe vya wazi kabisa, na hilo hufanya iwe rahisi zaidi kusoma.” Dada huyo anaongezea hivi: “Zamani, ningeweza tu kujifunza machapisho ya Biblia nikisaidiwa na watu wengine. Hata hivyo, sasa ninaweza kujifunza mwenyewe. Ninafurahi kwamba ninaweza kutayarisha mikutano ya Kikristo ya kila juma na kushiriki kikamili. Ninasoma machapisho yote ya maandishi ya vipofu. Unaweza kusema kwamba nimekuwa ‘mraibu’ kabisa wa machapisho hayo.”

 Kama machapisho yetu mengine, machapisho ya maandishi ya vipofu yanatia ndani maneno yafuatayo: “[Chapisho] hili haliuzwi. Ni sehemu ya kazi ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote inayotegemezwa kwa michango ya hiari.” Asante sana kwa kutoa michango hiyo kwa kutumia mbinu zinazotajwa kwenye donate.dan124.com. Ukarimu wako unasaidia kuhakikisha chakula cha kiroho kinapatikana kwa watu wote, kutia ndani vipofu na walio na matatizo ya kuona.

a Katika mifumo fulani ya maandishi ya vipofu, maneno yamefupishwa ili kuokoa nafasi. Kwa mfano, maandishi ya vipofu ya daraja la pili hufupisha maneno na herufi zinazofahamika. Hivyo, kitabu cha maandishi ya vipofu daraja la pili ni kidogo zaidi kuliko kitabu kilekile cha maandishi ya vipofu daraja la kwanza.