Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JAMHURI YA DOMINIKA

Kushughulikia Ongezeko

Kushughulikia Ongezeko

Watu wa Namna Zote Waokolewe”

Mapenzi ya Yehova ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Kupatana na hilo, Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Dominika wamejitahidi kuwafikia watu katika kila sehemu ya eneo lao, kutia ndani wafungwa walio gerezani.

Mwaka wa 1997, kila juma mapainia wawili wa pekee walikuwa wakitembelea Gereza la Najayo huko San Cristóbal walipokutana na Gloria, mwanamke mwenye umri wa miaka 23 kutoka Kolombia aliyefungwa kwa sababu ya kusafirisha dawa za kulevya. Alikuwa akizungumza na dada ambaye alifungwa kimakosa. Ili kujibu maswali ya Gloria, ndugu hao walimpelekea kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko na machapisho mengine. Alikuwa mwenye shauku na bidii ya kujifunza hivi kwamba wafungwa wengine walipendezwa, na hivyo kikundi kilichotembelewa kila juma kikazidi kukua.

Kweli ilimbadili sana Gloria, kisha mwaka wa 1999 akastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Kila juma alihubiri kwa zaidi ya saa 70 gerezani, na aliwafundisha Biblia wafungwa wenzake sita ambao walifanya maendeleo mazuri. Kisha mwaka wa 2000, alituma barua ya maombi ili kupata msamaha wa rais, na akakubaliwa kwa sababu ya tabia yake nzuri. Aliachiliwa na kurudishwa Kolombia. Mwaka wa 2001, muda mfupi baada ya kurudi Kolombia, alibatizwa ingawa familia yake ilipinga vikali uamuzi wake.

Gloria Cardona alijifunza kweli akiwa gerezani. Sasa, yeye na mume wake ni mapainia

Baada ya kubatizwa, Gloria alianza kufanya upainia. Aliolewa na ndugu ambaye ni mzee wa kutaniko, na wote ni mapainia wa kawaida. Sasa wanatumikia nchini Kolombia katika eneo lenye uhitaji mkubwa. Gloria amewasaidia wanafunzi wake wengi wajiweke wakfu na kubatizwa. Anasema kwamba anahisi ana deni kwa Yehova, na njia bora ya kumlipa ni kuwafanyia wengine jambo alilofanyiwa, yaani, kuwafundisha kweli.

Kama kisa cha Gloria kinavyoonyesha, milango ya gereza haijazuia wafungwa kujifunza kweli inayookoa uhai. Wawakilishi wa ofisi ya tawi walizungumza na maofisa wa Magereza na kuomba kibali ili akina ndugu waruhusiwe kuingia katika magereza mengine na kuwafundisha wafungwa Biblia. Matokeo ni kwamba ndugu 43 na dada 6 wamepewa vibali vya kufundisha Biblia katika magereza 13.

“Refusha Kamba za Hema Lako”

Mwishoni mwa karne ya 20, Jamhuri ya Dominika ilikuwa na wahubiri 21,684 katika makutaniko 342, na mafunzo ya Biblia 34,380 yalikuwa yakiongozwa. Hudhurio la Ukumbusho lilikuwa 72,679. Kwa sababu ya ongezeko hilo, watu wa Yehova wametii bila kusita maneno haya ya Isaya: ‘Fanya mahali pa hema lako pawe na nafasi kubwa zaidi. Nyoosha hema la maskani yako kuu. Usizuie. Refusha kamba za hema lako.’—Isaya 54:2.

Changamoto moja ilikuwa ni kupata Jumba la Kusanyiko ambalo lingetumiwa na idadi iliyokuwa ikiongezeka ya wahubiri. Mwaka wa 1996 Jumba la Kusanyiko lililokuwa karibu na ofisi ya tawi jijini Santo Domingo lilikamilika, na likatumiwa na makutaniko ya jiji hilo na maeneo ya karibu. Ingawa hivyo, Jumba la Kusanyiko huko Villa González, ambalo lilitumiwa na makutaniko mengine nchini lilihitaji kufanyiwa ukarabati mkubwa au kujengwa upya.

Katika mwaka wa 2001, Baraza Linaloongoza liliidhinisha ujenzi wa Jumba la Kusanyiko linalotoshea watu 2,500 katika kiwanja hicho huko Villa González. Akina ndugu walifurahi kusikia kwamba majengo mengine yangejengwa kwa ajili ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma (sasa ni Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme). Majengo hayo yangekuwa kando ya Jumba la Kusanyiko na yangekuwa na vyumba vya kulala, darasa, maktaba, jiko, na ukumbi wa kulia chakula. Mwaka wa 2004, Theodore Jaracz mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuweka wakfu majengo hayo. Tangu wakati huo, wanafunzi wa madarasa 15 wamehitimu shule hiyo.