Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Taarifa kwa Wazazi

Taarifa kwa Wazazi

Taarifa kwa Wazazi

Kwa vijana, kipindi cha kubalehe chaweza kulinganishwa na kutembea juu ya kamba. Huenda kila hatua ikaonekana kuwa ngumu zaidi na yenye kuogopesha kwelikweli. Mkiwa wazazi, huenda nyakati nyingine mkatamani kwamba laiti mngeweza kuwaepusha vijana wenu wasitembee katika “kamba” hiyo. Ukweli ni kwamba hamwezi kuwaepusha, hata hivyo mnaweza kuwa kama ufito wa kuwapa usawaziko wanapotembea. Ninyi hasa ndio mnaoweza kuwasaidia watoto wenu waendelee kutembea ifaavyo na hatimaye kuwa watu wazima wenye kutegemeka.

Je, mnaona ni rahisi kusema kuliko kutenda? Ni kweli. Juzijuzi tu mwana wenu alikuwa mtoto mwenye kurukaruka huku na huku, asiyetulia; sasa ni kijana mnyamavu ambaye hataki hata kuzungumza nanyi. Muda mfupi uliopita binti yenu mdogo alitaka kuandamana nanyi kila mahali mlipokwenda; sasa afadhali afe kuliko kuonekana pamoja na wazazi wake hadharani!

Hata hivyo, msiyaone mabadiliko hayo kama mlima mkubwa msioweza kuupanda. Kuna hazina ya hekima inayoweza kuwapa mwongozo bora ninyi na watoto wenu. Hazina hiyo ya hekima ni Neno la Mungu, Biblia.

Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kimekusudiwa kumpa mtoto wenu kanuni nzuri sana za Kimaandiko. Ukitazama Yaliyomo katika ukurasa wa 4 na 5 utaona habari mbalimbali zinazozungumziwa katika kitabu hiki. Hata hivyo, kitabu hiki kimekusudiwa kutimiza mengi zaidi. Fikiria mambo yafuatayo:

(1) Kitabu hiki kinamhusisha msomaji. Katika sehemu nyingi mtoto wenu atahitajika kuandika majibu ya maswali au taarifa fulani kulingana na maoni yake. Kwa mfano, sehemu yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” katika ukurasa wa 132 na 133, itamsaidia mtoto wenu kufikiria magumu mbalimbali na jinsi ya kukabiliana nayo. Isitoshe, katika kila moja ya sehemu tisa za kitabu hiki kuna ukurasa wenye kichwa “Daftari,” ambapo mtoto wenu anaweza kuandika maoni na hisia zake mwenyewe kuhusu habari iliyo katika sehemu hiyo.

(2) Kitabu hiki kinachochea mazungumzo. Kwa mfano, katika ukurasa wa 63 na 64 kuna sanduku lenye kichwa “Ninaweza Kuzungumza Namna Gani na Baba Yangu au Mama Yangu Kuhusu Ngono?” Pia, mwishoni mwa kila sura, kuna sanduku lenye kichwa “Una Maoni Gani?” Mbali na kuwa njia ya kujikumbusha mambo makuu, sanduku hilo laweza kutumiwa kuwa msingi wa mazungumzo ya familia. Tena, kila sura ina sehemu yenye kichwa “Hatua za Kuchukua!” Taarifa ya mwisho kabisa inamtaka kijana amalizie sentensi inayoanza kwa maneno: “Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni . . . ” Sehemu hiyo itawatia moyo vijana kuwategemea wazazi wao ili kupata mashauri yenye usawaziko yatakayowawezesha kutembea katika ile kamba ya mfano, kipindi cha kubalehe.

Tahadhari: Ili vijana wenu waandike majibu yao kwa unyoofu, acheni walichoandika katika nakala zao kiwe siri yao. Baadaye, huenda hata wakawa huru kuzungumza nanyi kuhusu mambo ambayo wameandika katika vitabu vyao.

Mwe na nakala yenu wenyewe ya kitabu hiki, na kukisoma kwa uangalifu. Mnapokisoma, jaribuni kukumbuka jinsi ilivyokuwa siku zenu, vituko, hekaheka, na mahangaiko yote mliyokuwa nayo mlipokuwa mkibalehe. Inapofaa, zungumzieni mambo hayo pamoja na mwana au binti yenu. Hilo litawachochea vijana wenu kuwafunulia yaliyo mioyoni mwao. Wanapozungumza, sikilizeni! Jitihada zenu za kuzungumza nao zikiambulia patupu, msikate tamaa. Hata ikionekana kana kwamba wanapuuza mashauri yenu, kwa kawaida watoto huthamini mashauri ya wazazi wao kuliko ya vijana wenzao.

Tunafurahi kuwaandalia ninyi na watoto wenu kifaa hiki kinachotegemea Biblia, nasi tunasali kwamba kitaisaidia sana familia yenu.

Wachapishaji