Hamia kwenye habari

Je, Nikijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova Watatazamia Niwe Mmoja Wao?

Je, Nikijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova Watatazamia Niwe Mmoja Wao?

 Hapana, huwajibiki kwa njia yoyote. Mamilioni ya watu wamenufaika na programu ya kujifunza Biblia bila kubadilisha dini na kuwa Mashahidi wa Yehova. * Kusudi la programu ya kujifunza ni kukuonyesha mambo ambayo Biblia inafundisha. Wewe ndiye utakayeamua jinsi ya kutumia ujuzi huo. Tunatambua kwamba imani ya mtu ni jambo la kibinafsi.​—Yoshua 24:15.

Je, ninaweza kutumia Biblia yangu wakati wa funzo?

 Ndiyo. Ingawa tunapenda kutumia Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyo na lugha ya kisasa na ambayo unaweza kupata bila malipo, tutafurahi ukitumia Biblia yako mwenyewe. Unaweza kujifunza kuhusu ujumbe wa Biblia unaotoa tumaini na wokovu kwa kutumia tafsiri yoyote.

Kwa nini mnajifunza na watu ambao hawajiungi nanyi katika dini yenu?

  •   Tunachochewa hasa na upendo kwa Yehova Mungu, ambaye anataka Wakristo wawafundishe wengine mambo ambayo wamejifunza. (Mathayo 22:37, 38; 28:19, 20) Tunahisi kwamba hakuna pendeleo kubwa zaidi kuliko kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” katika kuwasaidia watu wajifunze mambo ambayo Neno lake linafundisha.​—1 Wakorintho 3:6-9.

  •   Pia tunachochewa na upendo wetu kwa jirani. (Mathayo 22:39) Tunapata shangwe kwa kuwaeleza wengine mambo mazuri ambayo tumejifunza.​—Matendo 20:35.

^ Ili kuonyesha tunajifunza na watu wengi kadiri gani, katika mwaka wa 2022 tuliongoza mafunzo, 5,666,996 ya Biblia kila mwezi. Mengi ya mafunzo haya yaliongozwa na watu kadhaa wakati uleule. Hata hivyo, mwaka huo, ni watu 145,552 pekee waliobatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.