Hamia kwenye habari

Mashamba ya Watchtower​Miaka 50 ya Uvunaji

Mashamba ya Watchtower​Miaka 50 ya Uvunaji

Kilomita 145 hivi kaskazini ya New York City, karibu na eneo la Wallkill, New York, kuna mashamba ambayo yametimiza fungu muhimu katika kazi ya ulimwenguni pote ya elimu ya Biblia inayotolewa na Mashahidi wa Yehova. Shamba la kwanza la Watchtower, lilinunuliwa miaka 50 iliyopita, Januari 2, 1963.

David Walker, Shahidi wa Yehova ambaye ametumikia kule Wallkill tangu mwanzo, anaeleza sababu iliyofanya shamba hilo la kwanza linunuliwe: “Idadi ya wafanyakazi wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova kule Brooklyn, New York, ilikuwa ikiongezeka, na tulihitaji kuwalisha bila gharama kubwa. Ilichukua muda wa saa sita hadi nane kusafirisha bidhaa hadi Brooklyn kutoka kwenye shamba lile lingine la Mashahidi wa Yehova lililokuwa kaskazini mwa New York. Lakini Wallkill ni umbali wa saa mbili tu kutoka Brooklyn. Kwa hiyo, shamba hili lilifaa zaidi mahitaji yetu.” Mwishowe, Mashahidi wa Yehova walitumia shamba la Wallkill kukuza matunda na mboga na kufuga kuku, nguruwe, na ng’ombe kwa ajili ya nyama na bidhaa za maziwa. Baada ya muda, mashamba ya ziada yalinunuliwa.

Katika muda wa miaka 10 ongezeko la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova lilitokeza mabadiliko makubwa kule Wallkill. Mbali na kuzalisha chakula halisi, machapisho yakaanza kutokezwa ambayo yangesaidia katika kazi ya mfano ya kuvuna ambayo Yesu alizungumzia. (Mathayo 9:​37; Luka 10:2; Yohana 4:​35, 36) Fikiria kidogo kuhusu kazi inayofanywa kule Wallkill.

Uchapishaji: Katikati ya karne ya 20, kiwanda cha uchapishaji cha Brooklyn, New York, kilitokeza sehemu kubwa ya machapisho yetu ya Biblia. Lakini kadiri uhitaji wa machapisho ulivyoongezeka, kiwanda cha Brooklyn hakingeweza kushughulikia mahitaji yote hayo. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1973, Mashahidi wa Yehova walikamilisha ujenzi wa kiwanda cha ziada cha uchapishaji kule Wallkill. Tangu wakati huo, majengo yaliyo na mashine za uchapishaji yamepanuliwa mara kadhaa. Yamepanuliwa karibuni zaidi katika mwaka wa 2004.

Teknolojia ya Kompyuta: Mnamo 1979, kikundi cha Mashahidi wa Yehova kule Wallkill kilianza kutengeneza mfumo wa kompyuta wa kutayarisha maandishi kwa ajili ya uchapishaji (MEPS). Mfumo huo sasa unasaidia machapisho yatokezwe katika lugha zaidi ya 600.

Elimu: Mnamo 1988 Shule ya Biblia ya Gileadi ilihamishwa kutoka Brooklyn hadi Wallkill, na Oktoba 17, madarasa yakaanzishwa katika eneo hilo. Shule hiyo iliendelea kufanyiwa hapo hadi Aprili 1995 ilipohamishwa hadi kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower kule Patterson, New York.

Kama ilivyo na mashamba mengine, katika kipindi cha miaka 50 iliyopita mbinu na utendaji mbalimbali katika Mashamba hayo ya Watchtower umebadilika. Hata hiyo, bado jitihada nyingi zinafanywa ili kuandaa chakula kizuri kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova wanaotumikia katika ofisi za Betheli ya Marekani kule New York.

Kwa sasa, Mashahidi wa Yehova wanajenga majengo mapya kwa ajili ya ofisi, makao, na huduma nyinginezo huko Wallkill. Pia wanarekebisha majengo yaliyopo. Kazi hiyo yote itasaidia Mashamba ya Watchtower yaendelee kushughulikia mahitaji ya kiroho ya idadi kubwa ya Mashahidi wa Yehova inayozidi kuongezeka katika eneo hilo la dunia.

David Walker, aliyetajwa awali, anasema: “Kwa miaka 50 iliyopita, nimepata shangwe kubwa kuona jinsi ambavyo majengo ya Wallkill yameongezeka na kuchangia kazi yetu ya ulimwenguni pote ya kuwafundisha watu ujumbe wa Biblia!”