Hamia kwenye habari

Kitabu cha Hadithi za Biblia Chatumiwa Shuleni

Kitabu cha Hadithi za Biblia Chatumiwa Shuleni

Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia katika lugha ya Pangasinan, kilichotolewa mwaka wa 2012, kinatumiwa kuwasaidia watoto wa shule wanaozungumza lugha hiyo nchini Ufilipino. Kutolewa kwa kitabu hicho katika lugha hiyo kunapatana kabisa na mwelekezo wa Wizara ya Elimu ya Ufilipino wa kutumia lugha ya asili ya mtoto katika masomo ya shule za msingi.

Zaidi ya lugha 100 zinazungumzwa nchini Ufilipino, na kwa muda mrefu kumekuwa na mjadala wa ni lugha ipi inayopaswa kutumiwa katika masomo. Katika mwaka wa 2012, Wizara ya Elimu ilitoa agizo linalosema kwamba “kutumia lugha inayotumiwa nyumbani” huwasaidia watoto “kuelewa na kushika mambo wanayojifunza haraka.” Hivyo, mpango wa “Elimu kwa Lugha za Asili” ulianzishwa.

Lugha ya Pangasinan ni moja kati ya lugha zilizochaguliwa kutumiwa katika mpango huo. Lakini kulikuwa na tatizo. Mkuu wa shule moja alisema kuwa kuna vitabu vichache vya kusoma katika lugha ya Pangasinan. Hivyo basi, Mashahidi wa Yehova walipotangaza kutolewa kwa Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia katika lugha ya Pangasinan mnamo Novemba mwaka wa 2012 kwenye makusanyiko ya wilaya, huo ulikuwa wakati unaofaa sana.

Vitabu 10,000 hivi vilichapishwa ili vitolewe kwenye makusanyiko hayo. Watoto wadogo pamoja na wazazi wao walifurahia kupata kitabu katika lugha yao ya asili. Wenzi fulani wa ndoa walisema hivi: “Watoto wetu wanakipenda kitabu hiki kwa sababu wanaweza kukielewa vizuri.”

Muda mfupi baada ya kusanyiko, baadhi ya Mashahidi huko Dagupan City walienda shuleni na vitabu hivyo vipya. Walimu waliokuwa wakihangaika kutafuta vitabu vya kufundishia vya lugha ya Pangasinan, walifurahia sana kitabu hicho. Zaidi ya vitabu 340 viligawanywa. Mara moja walimu walianza kutumia kitabu hicho kuwafundisha watoto kusoma katika lugha yao ya asili.

Mashahidi wa Yehova wanafurahi kwamba kitabu hicho kinasaidia kuwafundisha watoto wadogo. Mtafsiri mmoja aliyesaidia kutafsiri Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia alisema: “Kwa muda mrefu tumetambua umuhimu wa kuandaa machapisho katika lugha za asili za watu ili tuwafikie mioyo yao. Ndiyo maana Mashahidi wa Yehova wanajitahidi sana kutafsiri Biblia na machapisho ya Biblia katika mamia ya lugha.”