Hamia kwenye habari

Waokolewa Wasijiue

Waokolewa Wasijiue

Mashahidi wawili wa Yehova walibisha nyumba moja walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba. Mwanamume aliyekuwa amefadhaika alifungua mlango; nyuma yake kulikuwa na kamba iliyokuwa ikining’inia juu ya ngazi.

Mwanamume huyo alipowakaribisha Mashahidi ndani, walimwuliza kamba hiyo ilikuwa ikifanya nini mahali hapo. Mwanamume huyo alijibu kwamba alikuwa amepanga kujinyonga, lakini mlango ulipobishwa, aliamua kuufungua kwa mara ya mwisho. Mashahidi walizungumza na mwanamume huyo na wakampeleka kwa daktari ambaye alimsaidia.

Kisa hicho kiliripotiwa katika gazeti moja la Ubelgiji. Hata hivyo, hiyo si mara ya kwanza ambayo Mashahidi wa Yehova wamemwokoa mtu asijiue. Soma kuhusu visa vingine kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni.

Mwanamke mmoja nchini Ugiriki aliandika hivi: “Nilikatishwa tamaa sana na mwanamume fulani na nikashuka sana moyo. Niliumia sana kihisia hivi kwamba niliamua kujiua. Wazo la kujiua lilinipa kitulizo—nilitaka maumivu hayo yaishe.”

Badala ya kujiua, mwanamke huyo alitafuta msaada wa daktari. Muda mfupi baadaye, aliwasiliana na Mashahidi, akaanza kujifunza Biblia, na kuhudhuria mikutano. “Akina ndugu wamenionyesha upendo usio na ubinafsi niliokuwa nikitafuta kwa miaka mingi.” Aliandika hivi: “Nimepata marafiki wa kweli ambao ninaweza kuwatumaini. Nina shangwe na nimetulia, sina wasiwasi wowote kuhusu wakati ujao.”

Shahidi mmoja nchini Uingereza anaandika hivi: “Mtu mmoja ninayefahamiana naye alinipigia simu akiwa amefadhaika sana na kuniambia kwamba atajiua usiku huo. Nikitumia habari kutoka makala iliyokuwa katika gazeti Amkeni! la Mei 2008 ambayo ilikuwa ikiwashauri watu wasijiue, nilizungumza naye na kumsomea maandiko yenye kufariji. Hataki tena kujiua licha ya matatizo yake.”

Nchini Ghana, Michael, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alianza kuzungumza na mwanamke fulani mahali alipokuwa akifanya kazi. Siku moja, Michael aliona kwamba mwanamke huyo alikuwa ameshuka sana moyo, na akamwuliza sababu.

Alimwambia kwamba alitaka kujiua kwa sababu mume wake alikuwa amemwacha na kuchukua mwanamke mwingine. Michael alimfariji na kumpa vitabu viwili vinavyoeleza mambo kuhusu Maandiko. Habari aliyosoma ilimfanya aache kufikiria kujiua. Mwanamke huyo aliendelea kujifunza Biblia na sasa yeye ni Shahidi wa Yehova.

Gazeti moja nchini Marekani liliripoti kwamba alipokuwa akihubiri mwanamke mmoja Shahidi aliona gari lililokuwa limeegeshwa lakini injini ilikuwa ikinguruma.

Mwanamke huyo alisema: “Niliona ncha moja ya bomba la mpira wenye kipenyo cha inchi nne ikiwa imeunganishwa kwenye bomba la kutolea moshi la gari. Ncha ile nyingine ilipitishwa kwenye dirisha la gari lililokuwa limefungwa kwa utepe.”

Nilienda haraka kwenye gari hilo, nikatazama kupitia dirishani na kumwona mwanamke mmoja akilia huku gari lote likiwa limejaa moshi mzito. ‘Unafanya nini?’ Nikamwuliza kwa sauti.

Nilipokuwa nikijaribu kufungua mlango, niliona watoto watatu wachanga wakiwa wameketi kwenye kiti cha nyuma. Nilipofungua mlango, mwanamke huyo aliniambia: ‘Lazima niende! Lazima niende! Lazima niende pamoja na watoto wangu.’

“Nilimwambia, ‘Tafadhali usijiue, hilo si suluhisho!’

“Alinijibu: ‘Lazima niende mbinguni. Lazima niende pamoja na watoto wangu.’

“Alipokuwa akilia, nilipiga magoti huku nikilia pia. Nikamwambia tena, ‘Tafadhali usijiue.’ Kisha nikaingia kwenye gari na kumshika begani, na kumtoa nje polepole.

“Kisha akapaza sauti, ‘Waokoe watoto wangu!’

“Wakaninyoshea mikono yao. Walikuwa wasichana wawili wenye umri wa miaka minne na mitano na mvulana mwenye umri wa miaka miwili. Walikuwa wameketi kimya kwenye kiti cha nyuma bila kujua kwamba baada ya muda mfupi wangekuwa wamekufa.”

“Wote wanne walipotoka ndani ya gari, nikazima injini. Sote watano tuliketi kwenye ukuta mfupi na nikamwambia mwanamke huyo anieleze matatizo yake.”

Mashahidi wa Yehova huona uhai kuwa zawadi yenye thamani kutoka kwa Muumba wetu. Duniani pote, wao hujitahidi kuwafariji watu ambao wapendwa wao wamejiua, na kuwasaidia wale ambao wamejaribu kujiua.

Jifunze Mengi: Kwa nini nisijiue?