Hamia kwenye habari

Ripoti ya Mkutano wa Kila Mwaka—Mwaka wa 2014

Miaka 100 ya Utawala wa Ufalme!

Ripoti ya Mkutano wa Kila Mwaka—Mwaka wa 2014

Oktoba 4, 2014, karibu watu 19,000 walikusanyika kwa ajili ya mkutano wa 130 wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania. Programu hiyo ilifanyiwa kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova la Jersey City, New Jersey, Marekani, na maeneo kadhaa yaliunganishwa kupitia Intaneti.

Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alikuwa mwenyekiti wa mkutano huo. Katika utangulizi wake, alikazia kwamba mkutano huo ulikuwa wa kihistoria, kwa kuwa ni mwadhimisho wa miaka 100 tangu kusimamishwa kwa Ufalme wa Kimasihi.

Ndugu Sanderson alizungumzia mambo matatu muhimu yaliyotimizwa na Ufalme katika miaka hiyo mia moja:

  • Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Yehova amewasaidia watu wake waeneze habari njema ya Ufalme bila kuchoka. Idadi yetu imeongezeka kutoka elfu chache mwaka 1914 hadi zaidi ya milioni nane katika mwaka wa utumishi wa 2014. Tutaendelea kuhubiri kwa bidii mpaka Yehova atakaposema kazi imekwisha.

  • Ulinzi kwa raia wa Ufalme wakiwa kikundi. Tumepingwa sana na wenye mamlaka katika dini na serikalini, na hata wamejaribu kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova kabisa. Hata hivyo, Yehova amewalinda waabudu wake wakiwa kikundi. Ushindi mwingi wa kisheria, kutia ndani ushindi kwenye Mahakama Kuu ya Marekani na kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, unathibitisha kwamba Yehova anaendelea kutulinda.

  • Kuunganishwa kwa watu wa mataifa yote. Ufalme wa Mungu umeunganisha watu kutoka malezi, mataifa, na lugha mbalimbali. Umewasaidia kukabiliana na changamoto tofauti-tofauti na kuwaunganisha kuwa kikundi kimoja cha waabudu. Ndugu Sanderson alisema hivi: “Ni Yehova Mungu peke yake ambaye angeweza kutimiza jambo hilo.” Kisha alikazia jinsi lilivyo pendeleo kubwa kuhudhuria mkutano huo wa kihistoria.

Mfululizo wa video za Uwe Rafiki ya Yehova.

Sehemu iliyofuata katika programu ya mkutano huo ilihusu mfululizo wa video za watoto ambazo tumefurahia kuzitazama kwa zaidi ya miaka miwili sasa. Kwanza, Ndugu Sanderson alionyesha video ya watoto kutoka sehemu mbalimbali duniani wakihojiwa. Watoto hao walishukuru sana kwa mambo yote waliyojifunza kutokana na video hizo. Maneno yao ya kutoka moyoni yaliwagusa moyo wote waliohudhuria.

Kisha wahudhuriaji walionyeshwa video mpya katika mfululizo huo. Ilikuwa na kichwa “Yehova Atakusaidia Uwe Jasiri.” Video hiyo ya dakika 12 inaelezea kwa njia yenye kusisimua simulizi la Biblia la msichana Mwisraeli aliyezungumza kwa ujasiri na mke wa Naamani kumhusu Yehova. (2 Wafalme 5:​1-​14) Video hiyo iliwekwa kwenye Tovuti ya jw.org Jumatatu, Oktoba 6, 2014, na inapatikana katika lugha zaidi ya 20.

JW Lugha.

Ndugu Sanderson alitangaza kutolewa kwa programu hiyo mpya katika vifaa fulani vya kieletroni. Programu hiyo itawasaidia Mashahidi wa Yehova ambao wanataka kujifunza lugha mpya ili wapanue huduma yao. Programu hiyo ina zaidi ya maneno na misemo 4,000 katika lugha 18. Mipango inafanywa ili kuongeza maneno na misemo zaidi, tangulizi za kutumia katika utumishi wa shambani, na vipengele vingine.

JW Broadcasting.

Wahudhuriaji walifurahi kusikia kuhusu kituo kipya cha televisheni cha Intaneti cha Mashahidi wa Yehova, kilichoanzishwa kwa majaribio katika lugha ya Kiingereza tu. Studio zake ziko katika makao makuu Brooklyn, New York, Marekani. Kitakuwa na video zetu, muziki, na drama za usomaji wa Biblia. Pia, kitaonyesha programu ya kila mwezi ambayo itaongozwa na mshiriki wa Baraza Linaloongoza au msaidizi wa moja ya halmashauri zake.

Ndugu Sanderson alionyesha sehemu fupi ya programu ya mwezi wa Oktoba. Programu hiyo iliyoongozwa na Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza, ilionyesha kazi iliyofanywa ili kuandaa studio za kituo hicho kipya cha televisheni. JW Broadcasting ilianzishwa Oktoba 6, 2014, na unaweza kuipata kwa kutembelea Tovuti ya tv.dan124.com.

“Ufalme—Miaka 100 ya Utawala.”

Samuel Herd wa Baraza Linaloogoza alikuwa msimuliaji katika video iliyoonyesha jinsi ambavyo Ufalme wa Mungu umetusaidia hatua kwa hatua kukua na kufanya maendeleo katika kazi yetu ya kuhubiri. Ilitia ndani video za zamani, maigizo, na mambo yaliyoonwa yaliyosimuliwa na Mashahidi ambao wametumikia kwa miaka mingi. Video hiyo ilizungumzia mambo kama vile kutokezwa na kuonyeshwa kwa sinema ya “Photo-Drama of Creation”; matumizi ya gramafoni, kadi za kutoa ushahidi, maandamano ya kutangaza habari, na magari yenye vipaza sauti; na shule mbalimbali za kutuzoeza kwa ajili ya huduma.

Tunafaidikaje kwa kutafakari mambo ambayo Ufalme umetimiza katika miaka hiyo 100? Kufanya hivyo kunatusaidia kuuona Ufalme ukiwa halisi zaidi na hivyo kutazamia kwa hamu kile ambacho utatimiza wakati ujao.

Nyimbo za Ibada.

David Splane wa Baraza Linaloongoza aliwafurahisha wote waliohudhuria alipotangaza kwamba kitabu chetu cha nyimbo, Mwimbieni Yehova, kinarekebishwa. Jalada lake litafanana na lile la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza. Kukitengeneza kwa vifaa vya hali ya juu hivyo kunaonyesha wazi kwamba muziki ni muhimu sana katika ibada yetu.

Ndugu Splane alitangaza pia kwamba kuna nyimbo kadhaa zitakazoongezwa katika kitabu hicho cha nyimbo. Lakini hatuhitaji kusubiri kitabu hicho kilichorekebishwa kichapishwe ili tuanze kuimba nyimbo hizo mpya. Zitapatikana kwenye Tovuti ya jw.org mara tu zitakapokuwa tayari.

Nyimbo tatu mpya, ambazo Familia ya Betheli ilikuwa imejizoeza mapema juma hilo, ziliimbwa katika mkutano huo. Ndugu Splane aliongoza kikundi cha waimbaji kilichoimba wimbo mpya wenye kichwa “Ufalme Umeanza Kutawala—Na Uje!” Wimbo huo ulitungwa hasa ili kuadhimisha miaka 100 tangu kusimamishwa kwa Ufalme. Baada ya waimbaji hao kuimba wimbo huo, wote waliohudhuria waliuimba pamoja nao. Baadaye, kikundi hicho cha waimbaji pamoja na wote waliohudhuria waliimba wimbo mwingine mpya wenye kichwa “Tupe Ujasiri.

Mahojiano.

Gerrit Lösch mshiriki wa Baraza Linaloongoza aliongoza mahojiano yaliyorekodiwa mapema ya ndugu watatu na wake zao, waliotumikia kwa miaka mingi katika utumishi wa Betheli. Walisimulia mabadiliko kadhaa waliyojionea katika tengenezo. Mabadiliko hayo yaliyoonyesha wazi kwamba watu wa Mungu wanasonga mbele. Ndugu Lösch alieleza kwamba Biblia ilitabiri kuhusu mabadiliko ya kitengenezo, na akawatia moyo wote waliohudhuria waendelee kusonga mbele na tengenezo la Yehova.​—Isaya 60:17.

“Vivuli na Ufananisho.”

Ndugu Splane alitoa hotuba hiyo, iliyoeleza kwa nini katika miaka ya karibuni machapisho yetu hayazungumzii kuhusu vivuli na ufananisho kama yalivyofanya zamani.

Zamani tulisema kwamba wanaume na wanawake wengi waaminifu wanaotajwa katika Biblia, waliwakilisha vikundi vya Wakristo waaminifu wa wakati wetu. Vivyo hivyo, masimulizi kadhaa ya Biblia yalidhaniwa kuwa na ulinganisho wa kinabii wa matukio yanayowahusu watumishi wa Mungu wa siku zetu. Ni kweli kwamba kujifunza kuhusu ulinganifu huo kunasisimua. Basi, kwa nini machapisho yetu ya karibuni zaidi hayazungumzii sana ulinganifu huo wa vivuli au ufananisho?

Biblia inaonyesha kwamba wahusika fulani na matukio fulani yalitangulia kuonyesha mtu fulani au tukio fulani kubwa zaidi la wakati ujao. Kwa hiyo, Biblia inapoonyesha wazi uhusiano uliopo kati ya kivuli na ufananisho wake, tunaukubali. Kisha Ndugu Splane akasema: “Lakini Biblia isiposema chochote, sisi hatupaswi kusema.” Tunapaswa kuepuka kuongeza ufafanuzi wetu tunaposoma masimulizi ya Biblia. Zaidi ya hilo, iwe tunatumaini la kuishi mbinguni au la kuishi duniani, tunapojishughulisha kupita kiasi kutafuta vivuli na ufananisho wa masimulizi mbalimbali, tunakosa kuona mambo muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi hayo ya Biblia.​—Waroma 15:4. *

“Je, ‘Utaendelea Kukesha’?”

Hotuba hiyo, iliyotolewa na Ndugu Lett, ilisahihisha uelewaji wetu wa mfano wa Yesu wa mabikira kumi. (Mathayo 25:​1-​13) Sasa tunaelewa mfano huo hivi: Bwana-arusi ni Yesu, na mabikira ni wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu. (Luka 5:​34, 35; 2 Wakorintho 11:2) Mfano huu unahusu siku za mwisho, na unatimia kikamili wakati wa dhiki kuu. Alipozungumza kuhusu mabikira watano wapumbavu, Yesu hakuwa akimaanisha eti wengi wa watumishi wake watiwa-mafuta wangekosa kuwa waaminifu na hivyo mahali pao pachukuliwe na wengine. Badala yake, alikuwa akitoa onyo kali. Mabikira watano walikuwa wenye busara na watano wapumbavu, kwa hiyo, kila mtiwa-mafuta ana nafasi ya kuchagua ama kuwa tayari na kuendelea kukesha au kutokuwa mwaminifu.

Kupatana na kanuni ya kuepuka kuongeza ufafanuzi wetu tunaposoma masimulizi ya Biblia, hatupaswi kujishughulisha kupita kiasi kuchanganua mfano huo na kutafuta ulinganisho wa kinabii kuhusu kila jambo. Badala yake, ni vizuri kutafuta mambo tunayojifunza kutokana mfano huo. Iwe sisi ni watiwa-mafuta au ni “kondoo wengine,” sote tuna daraka la kuacha nuru yetu iangaze na ‘kuendelea kukesha.’ (Yohana 10:16; Marko 13:37; Mathayo 5:16) Hakuna anayeweza kuwa mwaminifu kwa niaba yetu. Kila mmoja wetu ‘lazima achague uzima’ kwa kuendelea kukaa macho kiroho na kuwa mwenye bidii katika huduma.​—Kumbukumbu la Torati 30:19.

“Mfano wa Talanta.”

Anthony Morris mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba iliyofuata, na aliwasaidia wahudhuriaji kufahamu uelewaji wetu uliorekebishwa wa mfano wa talanta. (Mathayo 25:14-​30) Sasa tunaelewa kwamba bwana katika mfano huo (Yesu) atawathawabisha wakati ujao watumwa wake (wafuasi wake watiwa-mafuta waaminifu walio duniani) atakapofika na kuwapa uhai mbinguni. Alipozungumzia yatakayompata “mtumwa goigoi na mwovu,” Yesu hakuwa akitabiri kwamba sehemu kubwa ya wafuasi watiwa-mafuta wangekosa kuwa waaminifu. Badala yake, alikuwa akiwaonya watiwa-mafuta kuhusu umuhimu wa kuwa wenye bidii na kuepuka mitazamo na matendo ya mtumwa mwovu.

Ni mambo gani muhimu tunayojifunza kutokana na mfano huo? Bwana anayetajwa katika mfano huo aliwakabidhi watumwa wake kitu chenye thamani. Vivyo hivyo, Yesu amewakabidhi wafuasi wake kitu chenye thamani machoni pake, yaani, kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Anatarajia sote tushiriki kwa bidii katika kazi hiyo kulingana na hali zetu. Ndugu Morris aliwapongeza wote waliohudhuria kwa bidii yao katika shughuli za Ufalme.

“Ni Nani Atakayewashambulia Watu wa Mungu Hivi Karibuni”

Hicho kilikuwa kichwa chenye kusisimua cha hotuba ya mwisho ya programu hiyo, na ilitolewa na Geoffrey Jackson wa Baraza Linaloongoza. Ndugu Jackson alizungumzia mashambulizi ya wakati ujao ya Gogu wa Magogu dhidi ya watu wa Mungu.​—Ezekieli 38:14-​23.

Wakati uliopita, tulielewa kwamba Gogu ni jina lingine la Shetani Ibilisi baada ya kufukuzwa kutoka mbinguni. Lakini Ndugu Jackson alizungumzia changamoto zinazotokezwa na ufafanuzi huo. Kwa mfano, Yehova alitabiri kwamba Gogu atakaposhindwa, Yehova atamfanya awe “chakula cha ndege wenye kuwinda, na ndege wa kila namna ya bawa, na wanyama wa mwituni.” (Ezekieli 39:4) Yehova pia alitabiri kwamba “Gogu na umati wake wote” watapewa kaburi la kuzikwa duniani. (Ezekieli 39:11) Mambo hayo yanawezaje kumpata kiumbe wa roho? Shetani atatupwa katika abiso kwa miaka 1,000; hataliwa wala hatazikwa. (Ufunuo 20:​1, 2) Zaidi ya hilo, mwishoni mwa ile miaka 1,000, Shetani atafunguliwa kutoka katika abiso naye “ataenda kuyapotosha yale mataifa yaliyo katika pembe nne za dunia, Gogu na Magogu.” (Ufunuo 20:​7, 8) Ni wazi kwamba Shetani hawezi kumpotosha Gogu ikiwa yeye mwenyewe ndiye Gogu.

Ndugu Jackson alieleza kwamba Gogu wa Magogu katika unabii wa Ezekieli si Shetani, bali ni muungano wa mataifa yatakayowashambulia watu wa Mungu wakati ujao. Inaelekea kwamba shambulio la Gogu na lile la “mfalme wa kaskazini” na la “wafalme wa dunia” ni shambulio lilelile moja.​—Danieli 11:40, 44, 45; Ufunuo 17:12-14; 19:19.

“Mfalme wa kaskazini” ni nani? Tutasuburi tuone. Hata hivyo, imani yetu inaimarishwa tunapoona jinsi uelewaji wetu wa matukio hayo ya wakati ujao unavyoboreshwa kadiri siku hiyo inavyokaribia. Hatuogopi shambulio hilo la wakati ujao dhidi ya watu wa Mungu, kwa kuwa tunajua kwamba Gogu atakaposhambulia, atashindwa na kuangamizwa kabisa—na watu wa Mungu watadumu milele. *

Umalizio.

Ndugu Sanderson alitangaza kwamba Biblia ndogo ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya toleo lililorekebishwa, sasa inapatikana. Pia rekodi za usomaji wa Biblia zinatayarishwa, ambazo zitakuwa na sauti tofauti-tofauti kuwakilisha wahusika mbalimbali katika Biblia. Rekodi hizo zitapatikana hatua kwa hatua kwenye Tovuti ya jw.org, kuanzia na usomaji wa kitabu cha Mathayo.

Ndugu Sanderson alitangaza kwamba andiko la mwaka wa 2015 litakuwa Zaburi 106:1: “Mshukuruni Yehova, kwa maana yeye ni mwema.” Aliwatia moyo wote wafikirie sababu za kumshukuru Yehova kila siku.

Wimbo wa mwisho wa programu ulikuwa wimbo mpya wa tatu, wenye kichwa “Jina Lako Ni Yehova.” Washiriki wote saba wa Baraza Linaloongoza walienda jukwaani kujiunga na kikundi cha waimbaji, na hivyo wote waliohudhuria wakaimba pamoja wimbo huo mzuri na kumalizia mkutano huo wa kihistoria kwa njia inayofaa kabisa!

^ fu. 22 Hotuba hii na hotuba mbili zilizofuata zimetokana na makala itakayopatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2015

^ fu. 30 Hotuba hii imetokana na makala itakayopatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2015