Hamia kwenye habari

Kuhitimu kwa Darasa la 135 la Shule ya Biblia ya Gileadi

Kuhitimu kwa Darasa la 135 la Shule ya Biblia ya Gileadi

Septemba 14, 2013, watu 10,563 walikusanyika kwa ajili ya programu ya kuhitimu kwa darasa la 135 la Shule ya Biblia ya Gileadi iliyofanywa kwenye kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova huko Patterson, New York. Shule hiyo huwazoeza wahudumu wenye uzoefu wa Mashahidi wa Yehova kuwa wenye matokeo zaidi katika migawo yao.

Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova na mwenyekiti wa programu, alitegemeza maneno yake ya utangulizi kwenye andiko la Mathayo 28:19, 20: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”

Ndugu Pierce alisema kwamba maneno hayo ya Yesu yalianzisha jambo ambalo limeendelea hadi leo. Tunapowafanya watu kuwa wanafunzi, tunawafundisha kutimiza mambo yote ambayo Yesu aliamuru. Bila shaka, hilo linatia ndani amri ya kuhubiri “hii habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Kwa njia hiyo, kila mwanafunzi mpya anahubiri na kufundisha kuhusu Ufalme. Matokeo yamekuwaje? “Idadi ya watu [ulimwenguni] imeongezeka,” akasema Ndugu Pierce, “na pia idadi ya watu wa Mungu imeongezeka.”

“Walitoa Kupita Uwezo Wao Halisi.” Thomas Cheiky, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alizungumzia kichwa kilichotegemea 2 Wakorintho 8:​1-4. Licha ya umaskini mwingi, makutaniko ya Makedonia ya karne ya kwanza yalitoa michango kwa ajili ya ndugu zao kule Yerusalemu waliokuwa na uhitaji. Wanafunzi wa Gileadi wameonyesha roho hiyohiyo ya ukarimu na kujidhabihu.

Tunaweza kuamini kwamba Wamakedonia walikuwa pia wenye busara, hawakutoa kiasi kikubwa kupita kiasi hivi kwamba wakaathiri familia zao au ibada yao kwa Mungu. Ndugu Cheiky aliwashauri wanafunzi hao wawaige Wamakedonia kwa kudumisha usawaziko wanapotoa.

“Shule Imekwisha.” Samuel Herd mshiriki wa Baraza Linaloongoza alikazia kwa nini wanafunzi wanapaswa kukumbuka mambo waliyojionea katika Shule ya Gileadi. Kama muziki mtamu unaosikika asubuhi ambao mtu huendelea kuukumbuka siku nzima, kumbukumbu zenye thamani za Gileadi zinaweza kuwategemeza wanafunzi muda mrefu baada ya shule kwisha.

Ndugu Herd aliwakumbusha wanafunzi kwamba Mungu ana kumbukumbu isiyo na mipaka. Amezipatia nyota zote majina ingawa kuna mabilioni ya nyota ulimwenguni, na hatawahi kusahau nyota yoyote. (Zaburi 147:4) Basi hatasahau pia jitihada ambazo wanafunzi walitia ili kupokea mazoezi ya Gileadi! Wamekusanya “hazina mbinguni,” na hakuna anayeweza kuiba mawazo yenye thamani ambayo Yehova amehifadhi katika kumbukumbu lake kuhusu wanafunzi hao.​—Mathayo 6:​20.

Kwa kuwa Mungu anakumbuka kazi ya wanafunzi hao na upendo wao kumwelekea, wanafunzi wanaweza kuthamini mambo wanayokumbuka kuhusu Gileadi. “Unapokumbuka mambo yenye kufurahisha kuhusu shule hii,” akasema Ndugu Herd, “usisahau kumshukuru yule aliyefanya iwezekane kwako kuifurahia​—Yehova. Usichoke kukumbuka mambo uliyojifunza. Utapata faida zisizosahaulika.”

“Pata Faraja Kutokana na Nguvu za Yehova Zisizo na Kifani.” Mwalimu wa Gileadi Sam Roberson aliwatia moyo wanafunzi watumie nguvu za Yehova badala ya kutumia nguvu zao wenyewe wanapokabiliana na magumu mapya. Waefeso 3:​20 inasema kwamba Mungu anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” Nguvu zake zinazidi uwezo wetu wa kufikiri hivi kwamba hata maneno ‘kufanya kwa wingi zaidi kuliko tunachoweza kufikiri’ hayawezi kufafanua anachoweza kufanya, kwa sababu mstari huo unaonyesha anaweza kufanya mengi zaidi “kupita” tunachofikiri.

Yehova yuko tayari kumpa kila Mkristo nguvu zake zisizo na kifani. Tunapokabili matatizo makubwa yeye anakuwa kama “mwenye nguvu anayetisha,” au “shujaa anayetisha.” (Yeremia 20:11; God’s Word Bible) Ndugu Roberson aliwakumbusha wanafunzi kwamba Yehova atawasaidia kukabiliana na matatizo au magumu yoyote wanayokabili.

“Dumisha Heshima Yako Katika Utumishi wa Ufalme.” William Samuelson, ambaye pia ni mwalimu wa Gileadi, alieleza kwamba wanafunzi wa Gileadi wamepata heshima katika utumishi wa Ufalme katika njia mbili. Wameonyesha wazi kwamba wanastahili heshima kwa sababu ya kazi yao kabla na wakati wa shule, na pia wataendelea kupata heshima kwa kuwakilisha serikali kuu zaidi ulimwenguni​—Ufalme wa Mungu.

Wanafunzi wanaweza kudumishaje heshima yao? Ndugu Samuelson aliwatia moyo wampe Yehova utukufu na wawaheshimu wengine, kama vile Yesu alivyowaheshimu wale waliomzunguka hata alipohitaji kuwasahihisha au kuwashauri. Matokeo yatakuwaje? Kama mtume Paulo, wanafunzi watapata heshima zaidi, na wataitukuza huduma badala ya kujitafutia utukufu.​—Waroma 11:13.

“Mamlaka ya Farasi Wale Imo Katika Vinywa Vyao.” Michael Burnett, mwalimu mwingine wa Gileadi, alionyesha jinsi tunavyotenda kupatana na utimizo wa Ufunuo 9:​19 tunapotumia mambo tunayojifunza katika mikutano ya Kikristo ili kusema kwa mamlaka tunapohubiri. Kisha akazungumza na wanafunzi walioeleza au kuigiza mambo waliyojionea katika utumishi walipokuwa Gileadi. Kwa mfano, mwanafunzi mmoja alichochea upendezi wa mhudumu wa kituo cha mafuta kwa kumwuliza, “Nyakati zilizowekwa za mataifa zilianza lini na ziliisha lini?” (Luka 21:24) Baadaye, alimsaidia mtu huyo kupata jibu la swali hilo kwa kutumia Danieli sura ya 4, pamoja na nyongeza ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

“Mioyo Yao Imepewa Uthabiti.” Adrian Fernandez, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alimhoji Ndugu Helge Schumi na mke wake pamoja na Ndugu Peter Canning na mke wake. Ndugu Schumi alieleza kwamba kwa kuwa Biblia inaonyesha kwamba nyakati nyingine watumishi fulani wa Mungu wamekuwa na kiburi baada ya kupokea pendeleo la pekee, mara nyingi mtaala wa Shule ya Gileadi ulitia ndani ushauri kuhusu kuendelea kuwa wanyenyekevu. (2 Mambo ya Nyakati 26:16) Vivyo hivyo, Ndugu Canning alikumbuka mashauri yenye hekima kutoka kwa hotuba moja ya Gileadi kuhusu kujifunza lugha ya kienyeji: “Usiwe mwenye kiburi. Uwe tayari kuonekana kama mpumbavu.” Wahitimu wote wanne walishukuru sana kwa njia ambayo mtaala huo ulikuwa umewaimarisha kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele yao. Mioyo yao ilipata uthabiti kwa sababu ya mtaala huo.​—Waebrania 13:9.

“Shangilieni kwa Sababu Majina Yenu Yameandikwa Mbinguni.” (Luka 10:20) Geoffrey Jackson mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba kuu ya programu hiyo. Tofauti na wale waliohudhuria Shule ya Gileadi katika nyakati zilizopita, wahitimu wa sasa hawapewi migawo yenye kusisimua wala hawatapata mambo yaliyoonwa yenye kusisimua sana ambayo wengine hupata kwa kuhubiri katika maeneo ambayo hayajawahi kuhubiriwa. Wanapaswa kutendaje?

Wale wanafunzi 70 ambao Yesu aliwatuma katika kampeni ya kuhubiri waliporudi, waliripoti kwa shangwe kwamba walikuwa wamewafukuza roho waovu katika jina la Yesu. (Luka 10:​1, 17) Yesu alikubali kwamba matokeo hayo yalikuwa yenye kusisimua, lakini akasema: “Hata hivyo, msishangilie juu ya hili, kwamba roho wanatiishwa kwenu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” (Luka 10:20) Hivyo, alionyesha kwamba si kila siku wangepata matokeo yenye kusisimua kama hayo. Walipaswa kukazia fikira, si matokeo wanayopata, bali uaminifu wao kwa Yehova na majina yao ‘kuandikwa mbinguni.’

“Jambo ambalo Yesu aliwafundisha wale wanafunzi 70 linatuhusu sisi pia,” akasema Ndugu Jackson. Hatupaswi kuona kwamba matokeo tunayopata shambani ndio msingi pekee wa kuwa na shangwe au kipimo cha msingi cha uaminifu wetu. Badala yake, tunapata shangwe na kuthibitisha kwamba sisi ni waaminifu kwa kuendelea kuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova na kuwa na bidii katika utumishi wake.

Yesu pia alikabili hali ambazo zingeweza kumvunja moyo. Kwa mfano, baada ya kulisha maelfu ya watu kimuujiza, watu hao walianza kumfuata. (Yohana 6:​10-​14, 22-​24) Hata hivyo, muda mfupi baada ya hapo wengi wao walikwazwa na mafundisho ya Yesu, hivi kwamba ongezeko hilo kubwa la wanafunzi lilipungua upesi sana. (Yohana 6:​48-​56, 60, 61, 66) Tofauti na hilo, mitume washikamanifu walikuwa wameazimia kushikamana na Yesu. Walituwekea mfano mzuri wa kutohangaikia mtu anapata matokeo gani, na badala yake kujitahidi kuwa waaminifu na kuwa na uhusiano mzuri na Yehova.​—Yohana 6:​67-​69.

Umalizio. Wanafunzi walipokea diploma zao, na baada ya hapo mmoja wa wahitimu alisoma barua ya shukrani kwa niaba ya darasa. Ndugu Pierce alimalizia kwa kusema kwamba watu wa Mungu, kutia ndani wahitimu hao wa Gileadi, hawatambuliwi na ulimwengu kuwa watu wa maana. (Matendo 4:​13; 1 Wakorintho 1:​27-​31) Hata hivyo, Yehova anakubali kujitoa kwetu na anatupa roho yake takatifu. Ndugu Pierce alisema kwamba ingawa Yehova hastaajabishwi na elimu yetu, “anapendezwa sana na ushikamanifu wetu, uaminifu wetu, na ujitoaji wetu kwake.”