Hamia kwenye habari

Wanaomba Kazi Lakini Si Malipo

Wanaomba Kazi Lakini Si Malipo

Kwa zaidi ya miaka 28 iliyopita, zaidi ya Mashahidi wa Yehova 11,000 wamekuwa wakijenga majengo katika nchi 120. Wote hao wamejitolea kutumia ufundi, na muda wao bila malipo.

Wengi wao wamejilipia nauli ili wafike katika eneo la ujenzi. Wengine walitumia siku zao za likizo ili wasaidie kazi. Hata wengine waliwaomba waajiri wao ili wapewe siku za mapumziko, jambo lililofanya kiasi fulani cha mshahara wao kipunguzwe.

Hawakuwa chini ya wajibu wa kujidhabihu mambo hayo, hata hivyo, walijitoa wenyewe kwa kupenda ili waendeleze kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme duniani kote. (Mathayo 24:14) Wamejenga makazi, ofisi mbalimbali, na majengo ya viwanda vinavyochapisha Biblia na machapisho yanategemea Biblia. Pia, Mashahidi wa Yehova wamejenga Majumba ya Kusanyiko ambayo baadhi yanaweza kubeba watu 10,000 na Majumba ya Ufalme yenye uwezo wa kubeba hadi watu 300.

Kazi ya ujenzi bado inaendelea. Wafanyakazi wanapowasili tu katika eneo la ujenzi, basi ofisi ya tawi inawapatia mahali pa kulala, chakula, kuwafulia nguo, na mahitaji mengine ya kila siku. Mashahidi wanaoishi katika eneo hilo pia wanafurahia kushiriki katika kazi ya ujenzi.

Katika mwaka wa 1985 programu ya kimataifa ilianzishwa ili kupanga na kusimamia kazi hii kubwa. Ili mtu ajiunge kusaidia katika programu hiyo, ni lazima awe Shahidi wa Yehova mwenye umri kati ya miaka 19 na 55, pia awe na ustadi fulani katika mambo ya ujenzi. Kwa kawaida, wajitoleaji hufanya kazi kwa muda wa wiki mbili hadi miezi mitatu, hata hivyo, nyakati nyingine kazi inaweza kuendelea hadi mwaka mmoja au zaidi.

Wake wa wafanyakazi wamefundishwa kufanya kazi mbalimbali, kwa mfano, kuunganisha vyuma kwa kutumia waya, kupanga vigae, au kusugua mahali ili papakwe rangi. Wengine wanasaidia kupika chakula kwa ajili ya wale wanaofanya kazi au wanasafisha mahali pa kulala.

Pindi wanaporudi nyumbani baada ya ujenzi kukamilika, baadhi ya wajitoleaji huandika barua ili kushukuru kwa sababu ya kualikwa. Wanandoa fulani waliandika hivi: “Tungependa kuwashukuru sana kwa kutupatia pendeleo la kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Budapest. Mashahidi wa Yehova nchini Hungaria walitupenda na kututunza vizuri sana! Tulihuzunika sana siku ya kuachana baada ya kuwa nao kwa muda wa mwezi mmoja. Lakini kusema kweli, hivyo ndivyo ilivyo Mashahidi wanapoachana! Tunatumaini kwamba tutaweza kurudi tena wakati ujao, wakati mimea inapochipuka. Kila mara tulipoenda katika mgawo wa ujenzi, tumekuwa tukihisi kwamba huo ndio ulikuwa mwezi bora zaidi maishani mwetu.”