Ona video zinazopatikana

TUIGE IMANI YAO | YOBU

“Sitaacha Uaminifu-Mushikamanifu Wangu!”

“Sitaacha Uaminifu-Mushikamanifu Wangu!”

Mwanaume mumoja amekaa chini, mwili wake umejaa majipu yenye maumivu makali, ao vidonda. Umuwazie, ameinamisha kichwa, amekunja mabega yake, iko peke yake na hana hata nguvu za kufukuza mainzi yenye kumuzunguka. Amekaa mu majivu ili kuonyesha kama iko anaomboleza, na kile anaweza tu kufanya ni kukuna ngozi yake kwa kutumia kipande cha chombo cha udongo. Watu walikuwa wanamuheshimia sana, lakini sasa wanamuzarau! Marafiki wake, majirani wake, na watu wa jamaa yake wamemuacha. Watu wanamuchekelea, na hata watoto. Anawaza kama Yehova, Mungu wake, amemugeukia, lakini haiko vile.​—Yobu 2:8; 19:18, 22.

Ule mwanaume ni Yobu. Mungu alisema hivi juu yake: “Hakuna mutu kama yeye juu ya dunia.” (Yobu 1:8) Miaka mingi kisha, Yehova aliendelea kumuona Yobu kuwa mumoja kati ya watu wenye haki wenye waliishi ku dunia.​—Ezekieli 14:14, 20.

Uko unapiganisha magumu na hali za nguvu? Habari ya Yobu inaweza kukufariji sana. Inaweza pia kukusaidia uelewe muzuri zaidi sifa yenye kila mutumishi muaminifu wa Mungu anapaswa kuwa nayo, ni kusema, uaminifu-mushikamanifu. Mutu anaonyesha kama iko muaminifu-mushikamanifu wakati anashikamana kabisa na Mungu na hivyo anaendelea kufanya mapenzi yake, hata wakati wa magumu. Tuone basi namna mufano wa Yobu unatusaidia kuelewa jambo hilo.

Mambo Yenye Yobu Hakujua

Inaonekana kama Musa, mwanaume muaminifu, aliandika habari juu ya maisha ya Yobu wakati fulani kisha Yobu kufa. Kwa sababu Musa aliongozwa na roho ya Mungu, aliweza kufunua mambo yenye ilimupata Yobu ku dunia, na pia mambo fulani yenye ilitokea mbinguni.

Ku mwanzo wa habari ya Yobu, tunaona kama Yobu alikuwa na maisha ya muzuri na yenye furaha. Alikuwa tajiri sana, alikuwa anajulikana sana na kuheshimiwa mu inchi ya Usi, yenye pengine ilikuwa kaskazini mwa Arabia. Alikuwa tayari kusaidia maskini na alitetea watu wenye hawana uwezo. Yobu na bibi yake walibarikiwa kwa kuzaa watoto kumi. Zaidi ya yote, Yobu alikuwa mutu wa kiroho. Alijikaza sana kumufurahisha Yehova, sawasawa tu na watu wa jamaa yake wenye waliishi zamani kama vile Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu. Kama wazee hao wa ukoo, Yobu alikuwa kuhani kwa ajili ya familia yake, alikuwa anatoa zabihu kwa ukawaida kwa ajili ya watoto wake.​—Yobu 1:1-5; 31:16-22.

Kisha, mambo inabadilika kwa kushitukia. Tunasoma juu ya mambo yenye ilitokea mbinguni, na tunajifunza mambo yenye Yobu hakukuwa anajua. Malaika waaminifu wa Mungu walikuwa wamekusanyika mbele yake, na malaika muasi Shetani akaingia. Yehova alijua kama Shetani alikuwa anamuzarau Yobu, mwanaume mwenye haki, njo maana alizungumuza na Shetani na kumuonyesha kama Yobu alikuwa muaminifu-mushikamanifu kwa njia ya pekee. Bila kuogopa, Shetani alijibu: “Je, Yobu anamuogopa Mungu bure? Je, haukutia ukuta wa ulinzi kumuzunguka yeye na nyumba yake na kila kitu chenye iko nacho?” Shetani anachukia watu wenye kuonyesha uaminifu-mushikamanifu. Wakati wanashikamana na Yehova kwa moyo wao wote, wanaonyesha kama Shetani ni musaliti mwenye hana upendo. Kwa hiyo, Shetani alikazia kama Yobu anamutumikia Mungu juu ya faida zake mwenyewe tu. Shetani alisema kama, ikiwa Yobu angepoteza kila kitu, angemulaani Yehova mbele ya uso wake!​—Yobu 1:6-11.

Yobu hajue, lakini Yehova amemupatia pendeleo kubwa la kuonyesha kama Shetani ni muongo. Alimuruhusu Shetani anyanganye Yobu vitu vyake vyote. Hakumuruhusu tu kumuua Yobu. Kwa hiyo, Shetani alianza kumutesa Yobu kwa ukali. Mu siku moja tu, mambo mingi sana ya kuhuzunisha ilimupata Yobu. Alipata habari kama mifugo yake ilikuwa imeuawa kwa kushitukia: kwanza ngombe na punda zake, kisha kondoo zake, na kisha ngamia zake. Jambo la kuhuzunisha sana, watumishi wenye walikuwa wanachunga ile mifugo yake waliuawa. Kuhusu kikundi kimoja cha watumishi wake, Yobu alipata habari kama ni “moto kutoka kwa Mungu,” pengine umeme wa radi, njo uliwaua. Mbele hata Yobu afikie kuelewa mambo yenye ilitokea, namna wale watu wote walikuwa wamekufa na namna alikuwa sasa maskini, jambo lingine la mubaya zaidi lilitokea. Watoto wake kumi walikuwa wamekusanyika pamoja mu nyumba ya ndugu yao mukubwa, na kwa kushitukia upepo mukali ulipiga ile nyumba, na kuiharibu na kuwaua wote!​—Yobu 1:12-19.

Ni nguvu, na pengine haiwezekane, kuelewa namna Yobu alijisikia. Alipasua manguo yake, akakata nywele zake, na kuanguka chini. Yobu alisema kama Mungu amemupatia na Mungu amechukua. Lakini, kwa werevu, Shetani alifanya ionekane kama Mungu njo alileta ile misiba. Hata hivyo, Yobu hakumulaani Mungu sawa vile Shetani alikuwa amesema. Lakini, Yobu alisema hivi: “Jina la Yehova liendelee kusifiwa.”​—Yobu 1:20-22.

Yobu hakujua kama Shetani alikuwa anamushitaki mambo ya uongo mbele ya Mungu

“Atakulaani Mbele ya Uso Wako”

Shetani alikasirika sana, na hakupenda kuacha. Alienda tena mbele ya Yehova wakati wa mukusanyiko wa malaika. Tena, Yehova alimusifu Yobu juu ya uaminifu-mushikamanifu wake, wenye aliendelea kuonyesha ijapokuwa mashambulizi yote ya Shetani. Shetani alijibu hivi: “Ngozi kwa ngozi. Mutu atatoa kila kitu chenye iko nacho ili aokoe uzima wake. Lakini, ili mambo yabadilike, unyooshe mukono wako na upige mufupa wake na nyama yake, na hakika atakulaani mbele ya uso wako.” Shetani alikuwa hakika kama, ikiwa Yobu angegonjwa sana, angemulaani Mungu. Kwa sababu Yehova alimutumainia sana Yobu, alimuruhusu Shetani amuletee ugonjwa, lakini hakumuruhusu amuue.​—Yobu 2:1-6.

Bila kukawia, Yobu alijikuta mu hali yenye tulizungumuzia ku mwanzo wa habari hii. Wazia namna bibi yake alikuwa anajisikia. Tayari alikuwa na huzuni juu ya kufiwa na watoto wake kumi, na sasa anapaswa kuangalia, bila kuwa na jambo la kufanya, namna bwana yake anateseka sana! Juu ya huzuni mingi, anamuambia Yobu hivi: “Ungali unashikilia sana uaminifu-mushikamanifu wako? Laani Mungu na ukufe!” Ile haiko maneno yenye bibi ya Yobu angepaswa kusema. Yobu alitambua tu kama bibi yake anasema sawa vile mutu mwenye amepoteza akili. Lakini, Yobu alikataa kumulaani Mungu. Hakusema jambo lolote lenye lingeonwa kuwa zambi.​—Yobu 2:7-10.

Ulijua kama habari hii ya kuhuzunisha na ya kweli inakuhusu kipekee? Ujue kwamba mashitaka ya mubaya sana ya Shetani haikumuhusu tu Yobu, lakini inahusu wanadamu wote. Alisema hivi: “Mutu atatoa kila kitu chenye iko nacho ili aokoe uzima wake.” Ni kusema, Shetani anaamini kama kila mumoja wetu hawezi kuwa muaminifu-mushikamanifu! Anasema kama haumupendi kabisa Mungu, kama utamuacha Mungu haraka juu ya kuokoa uzima wako. Kwa kweli, Shetani anasema kama uko unatafuta faida zako mwenyewe kama vile yeye! Utapenda kuonyesha kama Shetani ni muongo? Kila mumoja wetu iko na pendeleo hilo. (Mezali 27:11) Tuone sasa magumu ingine yenye ilimupata Yobu.

Wafariji wa Uongo

Wanaume tatu wenye walimujua Yobu, wenye Biblia inaita kuwa marafiki wake, walisikia magumu yenye ilimupata na walifanya safari ili kumutembelea na kumufariji. Wakati walimuona kwa mbali, hawakumutambua. Yobu alikuwa na maumivu mingi, ngozi yake ilikuwa mweusi juu ya ugonjwa, alikuwa amebadilika kabisa. Wale wanaume tatu, ni kusema, Elifazi, Bildadi, na Sofari, walijifanya kuwa na huzuni kabisa, walilia kwa sauti na kutupa mavumbi juu ya vichwa vyao. Kisha, walikaa chini karibu na Yobu na hawakusema kitu. Walikaa pale kwa juma moja, usiku na muchana, bila kusema kitu. Hatupaswe kuwaza kama walikaa kimya juu wafikirie namna watamufariji, kwa sababu hawakumuuliza Yobu kitu; kile waliona tu ni kwamba Yobu alikuwa na maumivu makali.​—Yobu 2:11-13; 30:30.

Ku mwisho, Yobu alilazimika kuanzisha mazungumuzo. Alionyesha namna alikuwa na huzuni sana, alilaani siku yake ya kuzaliwa. Na alionyesha sababu moja kubwa yenye ilifanya ateseke sana vile. Aliwaza kama Mungu njo alimuletea magumu! (Yobu 3:1, 2, 23) Hata kama Yobu alikuwa angali na imani, alikuwa na lazima kabisa ya kufarijiwa. Lakini wakati wale marafiki tatu walianza kusema, Yobu alitambua mara moja kama ilikuwa muzuri tu wanyamaze.​—Yobu 13:5.

Elifazi, mwenye pengine alikuwa na miaka mingi zaidi kupita wenzake na kumupita Yobu, alianza kuongea. Kisha, wengine wawili waliongea pia. Kwa ujumla, tunaweza kusema kama, walisema bila kufikiri maneno yenye kufanana ya Elifazi. Maneno fulani yenye walisema ilionekana kuwa haina makosa, kwa sababu walirudilia tu mambo yenye watu walizoea kusema juu ya Mungu, kwa mufano walisema kama Mungu iko juu sana, anapatiaka malipizi watu wabaya, na kubariki watu wazuri. Lakini, kuanzia mwanzo wa mazungumuzo yao, walionyesha kama hawakumuhangaikia Yobu. Elifazi alitumia mawazo yenye ilionekana kuwa inapatana na akili lakini yenye ilikuwa na makosa. Alisema kama, ikiwa Mungu ni mwema na anapatiaka watu wabaya malipizi, na inaonekana wazi kama Yobu alikuwa anapewa malipizi, sasa tuseme nini? Je, Yobu haiko muovu mu njia fulani?​—Yobu 4:1, 7, 8; 5:3-6.

Haishangaze kwamba Yobu hakukubali ile mawazo. Aliipinga kabisa. (Yobu 6:25) Lakini wale washauri tatu wanakuwa hakika tena zaidi kama Yobu alifanya zambi fulani na alikuwa anajaribu kuificha; njo maana alistahili kupatwa na mambo yote ya mubaya yenye ilikuwa inamupata. Elifazi alisema kama Yobu alikuwa na kimbelembele, alikuwa muovu, na hakumuogopa Mungu. (Yobu 15:4, 7-9, 20-24; 22:6-11) Sofari alimuambia Yobu aache kufanya mambo ya mubaya na aache kufurahia zambi. (Yobu 11:2, 3, 14; 20:5, 12, 13) Na Bildadi alisema jambo fulani la kuumiza sana. Alisema kama watoto wanaume wa Yobu walipaswa kuwa walifanya zambi fulani, kwa hiyo, walistahili kabisa kufa!​—Yobu 8:4, 13.

Marafiki tatu wa Yobu hawakumufariji hata kidogo, lakini walimuumiza zaidi

Uaminifu-Mushikamanifu Unashambuliwa!

Wale wanaume wenye hawakukuwa na mawazo ya muzuri walifanya jambo fulani la mubaya hata zaidi. Walisema kama Yobu hakukuwa muaminifu-mushikamanifu kabisa kwa Mungu, na kama haina faida hata kujikaza kuwa muaminifu-mushikamanifu kwa Mungu! Mu mazungumuzo yake ya kwanza, Elifazi alieleza namna alikutana na roho fulani mwenye haonekane na mwenye kuogopesha. Kisha kukutana na ule roho, Elifazi akakuwa na mawazo hii ya mubaya: Mungu “hana imani katika watumishi wake, na anapata makosa ndani ya malaika wake.” Ile mawazo inaonyesha kama wanadamu bure hawawezi hata kidogo kumufurahisha Mungu! Kisha, Bildadi alionyesha kama Mungu hahangaikie uaminifu-mushikamanifu wa Yobu sawa vile hahangaikie uaminifu-mushikamanifu wa funza!​—Yobu 4:12-18; 15:15; 22:2, 3; 25:4-6.

Umekwisha kujaribu kufariji mutu fulani mwenye iko anateseka sana? Haiko mwepesi kufanya vile. Lakini, mufano wa marafiki wa Yobu wenye hawakukuwa na mawazo ya muzuri unaweza kutufundisha mambo mingi, zaidi sana mambo yenye hatupaswe kusema. Wale wanaume tatu walisema mambo mingi yenye ilionekana kuwa ilipatana na akili, lakini hawakumuita Yobu hata kwa jina! Hawakuhangaika kwamba Yobu alikuwa amevunjika moyo na hawakuona kama alikuwa na lazima ya kutendewa kwa fazili. * Kwa hiyo, kama mutu fulani mwenye unapenda iko na huzuni, jaribu kuzungumuza naye kwa uchangamufu, umuhangaikie, na umutendee kwa fazili. Jikaze kumusaidia akuwe na imani ya nguvu na kumutia moyo, umusaidie amutumainie Mungu na ajue kama Mungu ni mwema sana, mwenye rehema, na mwenye haki. Vile njo Yobu angetendea marafiki wake ikiwa wangekuwa mu hali yake. (Yobu 16:4, 5) Lakini, Yobu alitenda namna gani wakati waliendelea kumushambulia juu ya uaminifu-mushikamanifu wake?

Yobu Aliendelea Kuwa Muaminifu-Mushikamanifu

Tayari Yobu alikuwa na huzuni sana wakati ile mazungumuzo ya murefu ilianza. Tangu mwanzo wa ile mazungumuzo, alikubali kama wakati fulani mambo yenye alisema ilikuwa “mazungumuzo ya ovyoovyo” na “maneno ya mutu mwenye amepoteza tumaini.” (Yobu 6:3, 26) Na inaeleweka. Maneno yake ilionyesha kama alikuwa na huzuni sana. Tena, ilionyesha kama hakujua mambo yote. Kwa sababu taabu zenye zilimupata yeye na familia yake zilifika kwa kushitukia na hata zilionekana kuwa zililetwa na nguvu fulani yenye haionekane, Yobu aliwaza kama Yehova njo alimuletea taabu hizo. Kulikuwa matukio fulani ya maana yenye Yobu hakujua, njo maana, mambo fulani yenye alisema ilitegemea mawazo ya uongo.

Lakini, Yobu alikuwa na imani kubwa sana. Imani yake ilionekana wazi mu maneno yenye alisema mu ile mazungumuzo ya murefu. Alisema maneno ya kweli, ya muzuri na yenye inaweza kututia moyo leo. Wakati alizungumuzia mambo ya ajabu yenye Mungu ameumba, alimutukuza Mungu kwa namna yenye hakuna mwanadamu angeweza kufanya bila musaada wa Mungu. Kwa mufano, alisema kama Yehova “ananinginiza dunia mahali kwenye hakuna kitu,” jambo lenye wanasanyansi walifikia kuvumbua kisha miaka mingi. * (Yobu 26:7) Na wakati Yobu alizungumuzia tumaini lake la wakati wenye kuja, alizungumuzia tumaini lenye wanaume wengine waaminifu wa zamani walikuwa nalo pia. Yobu aliamini kwamba, ikiwa angekufa, Mungu angemukumbuka, angetamani kumuona tena, na kisha angemufufua.​—Yobu 14:13-15; Waebrania 11:17-19, 35.

Lakini, tuseme nini juu ya ubishi wenye ulitokezwa kuhusu uaminifu-mushikamanifu? Elifazi na marafiki wake wawili walionyesha tena na tena kama Mungu hahangaikie uaminifu-mushikamanifu wa mwanadamu. Yobu alikubali ile mawazo ya uongo? Hapana! Yobu alionyesha kama Mungu anaona uaminifu-mushimamanifu kuwa wa maana. Kumuhusu Yehova, alisema kwa uhakika hivi: “Atajua uaminifu-mushikamanifu wangu.” (Yobu 31:6) Tena, Yobu alitambua waziwazi kama mawazo ya uongo ya wafariji wake wa uongo ilishambulia uaminifu-mushikamanifu wake. Njo maana alifanya mazungumuzo ya murefu sana, yenye ilifikia kunyamazisha wale wanaume tatu.

Yobu alielewa kama alipaswa kuwa muaminifu-mushikamanifu mu maisha yake ya kila siku. Kwa hiyo, alieleza namna alikuwa anaonyesha uaminifu-mushikamanifu mu mambo yote yenye alikuwa anafanya. Kwa mufano, aliepuka aina yote ya ibada ya sanamu; alitendea wengine kwa fazili na kwa heshima; alikuwa na mwenendo safi kwa sababu aliona ndoa yake kuwa ya maana; na zaidi ya yote, aliendelea kushikamana kabisa na Yehova, Mungu mumoja tu wa kweli. Njo maana Yobu angeweza kusema kwa moyo wake wote hivi: “Mupaka wakati nitakufa, sitaacha uaminifu-mushikamanifu wangu!”​—Yobu 27:5; 31:1, 2, 9-11, 16-18, 26-28.

Yobu alikataa kuacha uaminifu-mushikamanifu wake

Tuige Imani ya Yobu

Unaona uaminifu-mushikamanifu kuwa wa maana kama vile Yobu? Yobu alielewa kama haitoshe tu kusema kama tuko waaminifu-washikamanifu, lakini tunapaswa kuonyesha sifa hiyo kupitia matendo. Tunaonyesha kama tunashikamana kabisa na Mungu kwa moyo wetu wote, kwa kumutii na kufanya mu maisha yetu ya kila siku mambo yenye anaona kuwa ya muzuri, hata wakati wa magumu. Kama tunafanya vile, kwa kweli tutamufurahisha Yehova na kumukasirisha Shetani, adui wake, kama vile Yobu alifanya zamani. Ile njo njia ya muzuri zaidi ya kuiga imani ya Yobu!

Lakini, habari ya Yobu haiishie pale. Juu ya kukosa usawaziko, alijitetea sana ili kuonyesha kama alikuwa mwenye haki, na hivyo alishindwa kutetea haki ya Mungu. Alikuwa na lazima ya kurekebishwa na kupata musaada wa kiroho. Na alikuwa angali na huzuni sana na maumivu makali, na lazima kabisa ya kufarijiwa. Yehova alimufanyia Yobu nini, mwanaume mwenye imani na muaminifu-mushikamanifu? Habari ingine kati ya habari hizi itatupatia jibu.

^ Jambo la kushangaza ni kwamba, Elifazi aliwaza kama yeye na wenzake walizungumuza na Yobu kwa fazili, pengine juu hawakupandisha sauti. (Yobu 15:11) Lakini hata maneno yenye kusemwa kwa sauti ya upole inaweza kuwa makali na yenye kuumiza sana.

^ Kulingana na mambo yenye tunajua, ni kisha miaka 3 000 hivi njo wanasayansi walielewa kama haikukuwa lazima dunia ikae juu ya kitu fulani. Ni kuanzia wakati wanasayansi walianza kukamata picha wakiwa mu anga, njo wanadamu walipata ushuhuda wenye kusadikisha wa kuonyesha kama maneno ya Yobu ilikuwa ya kweli.