Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA HISTORIA

Plato

Plato

Plato (k. 427-347 K.W.K.) alikuwa mwanafalsafa Mgiriki aliyekuwa mpagani. Alizaliwa huko Athene katika familia tajiri na yenye uvutano mkubwa na akapata elimu nyingi ambayo ilikuwa kawaida kwa vijana Wagiriki kutoka familia tajiri. Mwanafalsafa mashuhuri aliyeitwa Sokratesi na vilevile wafuasi wa Paithogorasi aliyekuwa mwanafalsafa na mwanahisabati, walikuwa na uvutano mkubwa kwake.

BAADA ya kusafiri katika maeneo ya Mediterania na kujihusisha katika siasa huko Sirakusa, lililokuwa jiji la Kigiriki huko Sisili, Plato alirudi Athene ambako alianzisha shule ya falsafa na sayansi iliyoitwa Academy. Shule hiyo ambayo mara nyingi imesemwa kuwa chuo kikuu cha kwanza huko Ulaya, ilikuja kuwa kitovu cha utafiti wa hisabati na falsafa.

KWA NINI HABARI HII IKUPENDEZE?

Mafundisho ya Plato yameathiri sana imani za kidini za mamilioni ya watu, kutia ndani watu wanaodai kuwa Wakristo, ambao wengi wao hufikiri kimakosa kwamba mafundisho hayo yanategemea Biblia. Fundisho la kwanza kati ya mafundisho ya Plato ni lile wazo kwamba nafsi ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mwili kufa.

“Kutokufa kwa nafsi ni mojawapo ya mafundisho ambayo Plato alipenda sana.”​—Body and Soul in Ancient Philosophy

Plato alipendezwa sana na maisha baada ya kifo. Kitabu Body and Soul in Ancient Philosophy kinasema kwamba “kutokufa kwa nafsi ni mojawapo ya mafundisho ambayo Plato alipenda sana.” Alisadiki kabisa kwamba “nafsi huendelea kuishi baada ya mwili wake wa sasa kufa, ili ithawabishwe au kuadhibiwa” katika maisha ya baadaye, kwa kutegemea jinsi mtu alivyoishi alipokuwa duniani. *

MAFUNDISHO YA PLATO YALIENEAJE?

Katika karne tisa ambazo shule hiyo ya Plato ilikuwapo, kuanzia 387 K.W.K. hadi 529 W.K., ilikuwa na uvutano mkubwa. Mawazo ya Plato yalienea sana katika maeneo yaliyotawaliwa na Ugiriki na Roma. Philo wa Aleksandria, aliyekuwa mwanafalsafa Myahudi alifuata mawazo ya Plato, kama tu walivyofanya viongozi wengi wa dini zilizodai kuwa za Kikristo. Kwa sababu hiyo, mawazo ya falsafa za kipagani, kutia ndani kutokufa kwa nafsi, yakawa sehemu ya mafundisho ya Kiyahudi na ya Kikristo.

Kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Mafundisho yote ya dini za Kikristo yanategemea, kwa kadiri fulani, falsafa ya Kigiriki, hasa mafundisho ya Plato, lakini wasomi fulani Wakristo . . . kwa kweli wanastahili kuonwa kuwa wafuasi wa Plato hata ingawa wao ni Wakristo.” Fikiria mambo yanayosemwa na vitabu vifuatavyo.

Plato alisema nini? “[Wakati wa kufa] sehemu halisi ya kila mmoja wetu, ambayo tunasema kuwa ndiyo nafsi isiyoweza kufa, hutoka na kwenda mbele ya miungu mingine, ili . . . kutoa hesabu,—jambo ambalo wale waliokuwa wema hukabili kwa ujasiri, lakini waovu hulikabili kwa hofu nyingi.”​—Plato—​Laws, Book XII.

Biblia inasema nini? Nafsi ndiye mtu mwenyewe au uhai alio nao. Hata wanyama ni nafsi. Mtu anapokufa, hakuna sehemu yoyote inayoendelea kuishi. * Fikiria maandiko yafuatayo:

  • “Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi hai.”​ —1 Wakorintho 15:45.

  • “Mungu akaendelea kusema: ‘Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake, mnyama wa kufugwa na mnyama anayetambaa na mnyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake.’”​—Mwanzo 1:24.

  • “Nafsi yangu na ife.”​—Hesabu 23:10.

  • “Nafsi inayotenda dhambi​—hiyo yenyewe itakufa.”​—Ezekieli 18:4.

Ni wazi kwamba Biblia haifundishi kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Kwa hiyo jiulize hivi, ‘Je, imani yangu inategemea Biblia au falsafa za Plato?’

^ Ingawa Plato ndiye aliyefanya fundisho la kutokufa kwa nafsi liwe maarufu, hakuwa wa kwanza kulifundisha. Dhana hiyo ilikuwepo katika dini za kipagani kwa muda mrefu sana, kutia ndani dini za Misri na Babiloni.

^ Biblia inafundisha ni kana kwamba wafu wamelala, wanasubiri kufufuliwa. (Mhubiri 9:5; Yohana 11:11-14; Matendo 24:15) Tofauti na hilo, kulingana fundisho la Plato, ikiwa nafsi haziwezi kufa, hazihitaji ufufuo.