Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Alishikamana na Mambo Yenye Anaamini

Alishikamana na Mambo Yenye Anaamini

Wakati Song Hee alikuwa na miaka 11, mama yake alitambua kuwa alikuwa na sehemu fulani yenye kujikunja katika mugongo wake. Muganga fulani alivumbua kuwa mufupa wa katikati ya mugongo wa Song Hee ulikuwa wenye kujikunja kuelekea upande mumoja. Tatizo hilo linafanya mufupa wa katikati ya mugongo ukuwe na umbo la “C” ao “S.” Hali ya Song Hee ilifikia kuwa mubaya sana, kwa hiyo iliomba apasuliwe. Lakini Song Hee hangeitika kutiwa damu katika mishipa. Gazeti “Amuka!” lilimuuliza juu ya mambo yenye yalimufikia.

Wakati ulivumbuliwa na tatizo hilo, waganga waliweza kukusaidia?

Kwa miaka karibu tatu, waganga wawili walikuwa wanafuata hali yangu, lakini mufupa wangu wa katikati ya mugongo uliendelea kujikunja. Hali ikakuwa mubaya sana mupaka mufupa huo ukaanza kufinya moyo na mapafu yangu, na hilo lilifanya nikuwe na magumu ya kupumua. Iliomba kabisa nipasuliwe.

Uliitika kupasuliwa?

Ndiyo. Lakini niliambiwa kama upasuaji utakuwa mugumu. Wakati huo, mufupa wangu wa katikati ya mugongo ulijikunja sana mupaka kufikia digrii 116. Hiyo ni hali yenye kuwa hatari sana. Lakini, juu ya hali yangu, kupasuliwa kulitokeza tatizo la pekee. Kwa sababu ya mambo ninaamini, yenye kutegemea Biblia, singeitika kutiwa damu katika mishipa. *

Ulipata muganga mwenye alikuwa tayari kukupasua bila kukutia damu?

Mimi na mama yangu tulipata muganga mwenye kujua muzuri tatizo langu katika jimbo letu la Florida, inchi ya Amerika. Lakini, wakati nilimuambia kama sitaitika kutiwa damu katika mishipa, alisema kama hakuna muganga mwenye anaweza kufanya upasuaji huo mugumu bila kunitia damu. Tena, alisema kama, ikiwa sipasuliwe, pengine sitafikisha miaka 20. Nilikuwa tu na miaka 14.

Ulimufasiria sababu gani ulikataa kutiwa damu?

Ndiyo. Nilimuambia kama mambo yenye ninaamini yanategemea Biblia. Nilimuonyesha kama Mungu anaona damu kuwa takatifu, iwe ya mutu ao ya munyama. * Muisraeli mwenye alikula damu alipaswa kuuawa! * Tena, nilimuonyesha andiko la Matendo 15:19, 20. Andiko hilo linahusu Wakristo, sehemu yake moja inasema hivi: ‘Mujiepushe na . . . damu.’ Hilo linamaanisha kama damu haipaswe kuingizwa ndani ya mwili kwa njia yoyote, iwe kwa kuikula ao kwa kuitia katika mishipa.

Mupasuaji huyo alielewa?

Aliendelea kukazia kama anapaswa tu kunitia damu. Na jambo la kushangaza ni kwamba hospitali ilisema kama nikiitika kutiwa damu, sitaombwa kulipa kitu chochote.

Hiyo ilikuwa zawadi ya muzuri! Lakini wewe na mama yako mulifanya nini?

Hata kama hakuna muganga mwenye alionekana kuwa tayari kunipasua bila kunitia damu, tuliamua kushikamana kabisa na mambo yenye tunaamini. Kisha mambo yakakuwa magumu zaidi. Kupatana na sheria ya inchi yetu, nilikuwa ningali mutoto. Kwa sababu hali yangu iliendelea kuwa ngumu, tatizo langu lilipelekwa kwenye tribinali. Jambo la kufurahisha ni hili: tribinali ilitupatia siku 30 ili kutafuta muganga mwenye angekubali kunipasua bila kutumia damu.

Muganga huyo alipatikana?

Ndiyo! Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali ya Mashahidi wa Yehova katika muji wetu ilizungumuza na muganga mumoja katika muji wa New York mwenye anajua kutunza tatizo langu. Muganga huyo alikuwa tayari kunipasua bila kutumia damu na aliitika kuniona. Kwa hiyo, tulipata muganga huyo mbele siku 30 zienee. *

Upasuaji ulipita namna gani?

Ulipita muzuri kabisa! Ili kunyoosha mufupa wangu wa katikati ya mugongo, mupasuaji Robert Bernstein aliniingiza vitu vyenye kufanana fimbo ndani ya mugongo. Vitu hivyo vinaweza kuondolewa. Alifanya upasuaji huo katika sehemu mbili majuma mawili tofauti.

Sababu gani katika sehemu mbili?

Ikiwa katika sehemu ya kwanza ya upasuaji ningepoteza damu nyingi sana, mwili wangu ungekuwa na wakati wa kutoa chembe nyekundu za damu mbele ya kufanya sehemu ya pili ya upasuaji. Kwa sababu kikundi cha wapasuaji kilipanga mambo muzuri, kilikuwa na ufundi, na kilifanya kazi kwa uangalifu, mambo yalipita muzuri; katika sehemu hizo mbili za upasuaji, nilipoteza damu kidogo. Tena, nilipona haraka bila kupatwa na magumu yanayoweza kutokea kwa sababu ya kutiwa damu. *

Muganga wako alijisikia namna gani juu ya matokeo hayo?

Waganga wanapaswa kuhangaikia mambo yote juu ya mugonjwa

Alifurahi sana! Alisema kama “matunzo haiko tu kupasua watu.” Aliona kama waganga wanapaswa kuhangaikia mambo yote juu ya mugonjwa, hata mambo yenye anaamini na kanuni zake. Watu wengi wasiokuwa Mashahidi wa Yehova wanaweza pia kukubali kabisa mawazo hayo.

^ fu. 7 Mama ya Song Hee ni Shahidi wa Yehova. Song Hee iko na imani kama ya mama yake, alibatizwa katika mwaka wa 2012. Alikuwa na miaka 16.

^ fu. 17 Halmashauri za Uhusiano na Hospitali zinasaidia Mashahidi wenye kuwa wagonjwa kupata waganga wenye watawatunza bila kutumikisha damu.

^ fu. 21 Katika habari moja iliyosema juu ya hatari za kutia mutu damu katika mishipa, shirika moja la Australia lenye kuhangaikia afya lilisema hivi: “Kutia mutu damu katika mishipa ni sawa vile unamutia kiungo kingine ndani ya mwili. Kwa kawaida mwili wa mwanadamu unajaribu kukataa kiungo kigeni. Kuingiza kiungo kigeni ndani ya mwili kunaleta hatari kubwa juu ya afya.”