Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Niliazimia Kuwa Askari wa Kristo

Niliazimia Kuwa Askari wa Kristo

Wakati risasi zilikuwa zinalia pembeni yangu, polepole, niliweka juu kitambaa cha mweupe. Maaskari wenye walikuwa wanapiga risasi hizo walinilalamikia na kuniambia nitoke mahali nilikuwa ninajificha. Niliwakaribia kwa uangalifu bila kujua ikiwa ningeishi ao ningekufa. Namna gani nilifikia kuwa katika hali hiyo yenye hatari?

NILIZALIWA katika mwaka wa 1926. Nilikuwa mutoto wa saba katika familia ya watoto munane; wazazi wetu walikuwa wafanyakazi wenye bidii katika Karítsa, kijiji kidogo katika inchi ya Ugiriki.

Mwaka moja mbele ya kuzaliwa kwangu, wazazi wangu walikutana na John Papparizos, Mwanafunzi wa Biblia (Mashahidi wa Yehova walikuwa wanaitwa hivyo zamani) mwenye bidii na mwenye kusema mingi. Kwa sababu walishangazwa na namna John alikuwa anafasiria maandiko katika njia yenye kuwa wazi na yenye kueleweka, hilo liliwafanya waanze kukusanyika pamoja na Wanafunzi wa Biblia katika kijiji chetu. Mama yangu alikuwa na imani yenye nguvu sana katika Yehova Mungu, na hata kama hakujua muzuri kusoma na kuandika, alizungumuza na wengine juu ya imani yake kila wakati alipata nafasi ya kufanya hivyo. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba baba yangu alikazia makosa ya watu na pole kwa pole akaacha kuenda kwenye mikutano ya Kikristo.

Mimi na ndugu na dada zangu tuliheshimia Biblia, lakini wakati tulikuwa tunakomaa, tulikengeushwa na tamaa za wakati wa ujana. Kisha, katika mwaka wa 1939, wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilienea katika Ulaya, tukio fulani lilitushitua katika kijiji chetu. Nicolas Psarras, jirani yetu mwenye alikuwa pia mutoto wa ndugu ya baba yetu na mwenye alikuwa Shahidi wa Yehova mwenye alibatizwa hivi karibuni, aliandikishwa katika jeshi la Ugiriki. Bila woga, Nicolas mwenye alikuwa na miaka 20, aliambia wakubwa wa jeshi hivi: “Siwezi kupigana kwa sababu niko askari wa Kristo.” Alisambishwa na tribinali ya kijeshi na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi katika gereza. Tulishangaa sana!

Jambo la kufurahisha ni kwamba mwanzoni mwa mwaka wa 1941, majeshi ya Muungano yaliingia kwa muda mufupi katika Ugiriki, na Nicolas akaachiliwa kutoka katika gereza. Alirudia Karítsa kwenye Ilias, ndugu yangu mukubwa, alimuuliza maulizo mengi sana juu ya Biblia. Nilisikiliza mazungumuzo hayo kwa hamu sana. Kisha, mimi na Ilias na Efmorfia, mudogo yetu mwanamuke, tulianza kujifunza Biblia, na tulienda kwa ukawaida kwenye mikutano ya Mashahidi. Mwaka wenye ulifuata, sisi watatu tulitoa maisha yetu kwa Yehova na kubatizwa. Mwishowe, ndugu na dada zetu wengine ine walifikia pia kuwa Mashahidi waaminifu.

Katika mwaka wa 1942, Kutaniko la Karítsa lilikuwa na vijana wanaume na wanawake kenda wenye kuwa kati ya miaka 15 na 25. Sisi wote tulijua kuwa majaribu makali yalikuwa yanatungojea. Kwa hiyo, ili tukuwe wenye nguvu kiroho, tulikutana pamoja kila wakati iliwezekana kufanya hivyo ili kujifunza Biblia, kuimba nyimbo za kiroho, na kusali. Matokeo ni kwamba imani yetu ilitiwa nguvu.

Demetrius na marafiki wake katika Karítsa

VITA YA WENYEWE KWA WENYEWE

Wakati tu Vita ya Pili ya Ulimwengu ilikaribia kuisha, wakoministi Wagiriki waliasi serikali ya Ugiriki na kuanzisha vita kali ya wenyewe kwa wenyewe. Wapiganaji wakoministi walizunguka-zunguka katika vijiji na kulazimisha wakaaji wa vijiji wajiunge nao. Wakati walishambulia kijiji chetu walikamata kwa nguvu vijana tatu Mashahidi, ni kusema, Antonio Tsoukaris, Ilias, na mimi. Tuliwaambia kama tulikuwa Wakristo wenye hawajiingize katika vita, lakini walitukaza kuenda kwenye Mulima Olympus; ili kutoka katika kijiji chetu na kufika kwenye mulima huo iliomba kutembea kwa saa 12.

Muda mufupi kisha hapo, ofisa fulani mukoministi alituamuru tujiunge na kikundi cha wapiganaji washambulizi. Wakati tulifasiria kuwa Wakristo wa kweli hawakamate silaha ili kuua wanadamu wenzao, mukubwa huyo mwenye kukasirika sana alitupeleka kwa nguvu mbele ya jenerali. Wakati tulifasiria tena musimamo wetu, jenerali huyo alituamuru hivi: “Mukamate basi punda na mubebe kwenye hospitali wale wenye waliumizwa katika vita.”

Tulijibia hivi: “Lakini tutafanya nini ikiwa maaskari wa serikali wanatukamata? Kwa kweli, watatuona kuwa wapiganaji waasi.” Jenerali huyo akasema hivi: “Mupelekee basi wapiganaji mikate kwenye vita.” Tukafikiri naye hivi: “Lakini tutafanya nini ikiwa ofisa fulani anatuona na punda na kutuamuru tupeleke silaha mahali pa vita?” Jenerali huyo alifikiri sana. Mwishowe, akasema hivi: “Munaweza basi kuchunga kondoo! Mubakie kwenye mulima na kuchunga kondoo.”

Kwa sababu vita ya wenyewe kwa wenyewe iliendelea mahali penye tulikuwa, sisi watatu tuliona kuwa zamiri yetu ingeturuhusu kuchunga kondoo. Kwa sababu Ilias alikuwa mutoto mwanaume wa kwanza katika familia yetu, kisha mwaka moja aliruhusiwa kurudia nyumbani ili kuchunga mama yetu mujane. Antonio aligonjwa na akaachiliwa. Lakini mimi niliendelea kufungwa.

Wakati huo, jeshi la Ugiriki lilikuwa linazunguka polepole wakoministi. Wapiganaji wenye walikuwa wamenifunga walikimbia kupitia milima ili kuenda katika inchi jirani ya Albania. Wakati tulikaribia mupaka wa inchi hiyo, mara moja tulitambua kama tumezungukwa na maaskari wa Ugiriki. Waasi hao waliogopa sana na wakakimbia. Nilijificha nyuma ya muti wenye ulikuwa umeanguka, na ni hilo lilifanya nikutane na maaskari wenye nilizungumuzia mwanzoni.

Wakati niliambia maaskari wa Ugiriki kama nilikuwa nimefungwa na wakoministi, walinipeleka nisambe kwenye kambi moja la majeshi karibu na Véroia, muji wa zamani wa Beroya. Huko waliniamuru nichimbe mashimo ya kufichamia kwa ajili ya maaskari. Wakati nilikataa, ofisa musimamizi aliamuru nipelekwe katika kisiwa cha wafungwa cha Makrónisos (Makronisi).

KISIWA CHA MATESO

Kisiwa hicho cha Makrónisos, chenye kukauka, chenye hakina maji na chenye kuwa na joto kali, kinapatikana katika eneo la Attica lenye kuwa pembeni ya bahari kwenye kilometre karibu 50 kutoka muji wa Athene. Kisiwa hicho kiko tu na urefu wa kilometre 13 na upana wa kilometre mbili na nusu. Lakini, kuanzia mwaka wa 1947 mupaka 1958, kisiwa hicho kilikuwa na wafungwa zaidi ya 100000, kutia ndani waasi wakoministi na watu wenye waliwaziwa kuwa wakoministi, watu wenye zamani walikuwa wapiganaji waasi, na hesabu kubwa ya Mashahidi waaminifu wa Yehova.

Wakati nilifika katika kisiwa hicho mwanzoni mwa mwaka wa 1949, wafungwa walikuwa wamegawanywa katika kambi mbalimbali. Niliwekwa katika kambi yenye haikukuwa na ulinzi mukali pamoja na mamia ya wanaume wengine. Watu 40 hivi kati yetu tulilala chini katika hema moja nzito lenye lilitengenezwa kwa ajili ya watu 10. Tulikunywa maji machafu na kukula nyanya na aina fulani ya maragwe yenye kuitwa ndengu. Vumbi ya kila wakati na upepo vilifanya maisha yakuwe magumu sana. Lakini hatukulazimika kabisa kuendelea kupanda na kushuka tukisukuma majiwe makubwa-makubwa, mateso makali sana yenye yaliharibu miili na akili za wafungwa wengi.

Niko katika kisiwa cha Makrónisos pamoja na Mashahidi wengine wenye walipelekwa huko

Siku moja wakati nilikuwa ninatembea pembeni ya bahari, nilikutana na Mashahidi fulani wenye walikuwa katika kambi zingine. Tulifurahi sana kuwa pamoja! Tulikutana kila wakati tuliweza kufanya hivyo, lakini tulikuwa waangalifu sana ili watu wasituone. Tulihubiria pia wafungwa wengine kwa uficho, na wamoja kati yao walifikia kuwa Mashahidi wa Yehova. Kufanya hivyo na kusali kutoka moyoni kulitusaidia tuendelee kuwa nguvu kiroho.

KATIKA MATESO MAKUBWA SANA

Kisha miezi 10 yenye walijaribu kunifanya nibadilishe musimamo wangu, watu wenye walikuwa wamenifunga waliamua kuwa nilipaswa sasa kuvaa nguo za kijeshi. Wakati nilikataa, walinipeleka kwa nguvu mbele ya kamanda wa kambi. Nilipatia kamanda huyo karatasi yenye ilikuwa na maneno haya: “Ninapenda kuwa askari wa Kristo tu.” Kisha kuniogopesha, kamanda huyo alinipeleka kwa kamanda mwenye kumufuatia; kamanda huyo alikuwa askofu Mugiriki wa kanisa la Orthodox, na alikuwa anavaa nguo za viongozi wa dini. Wakati nilijibia kwa ujasiri maulizo yake kwa kutumia Maandiko, alisema hivi kwa ukali: “Mumutoshe hapa. Iko na musimamo mukali!”

Siku ya pili, maaskari waliniamuru tena nivae nguo za kijeshi. Wakati nilikataa, walinipiga ngumi na fimbo zao za miti. Kisha wakanipeleka kwenye hospitali ya kambi ili kuhakikisha kuwa mifupa yangu haikukuwa imevunjika na wakanirudisha katika hema langu. Waliendelea kunitendea hivyo kila siku kwa miezi mbili.

Kwa sababu nilishikamana na imani yangu, mwishowe maaskari hao wenye kukasirika walijaribu njia ya mupya. Walinifunga mikono nyuma, kisha wakanipiga mubaya sana kwenye sehemu ya chini ya miguu yangu kwa kutumia kamba. Katika maumivu hayo makali, nilikumbuka maneno haya ya Yesu: ‘Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu [wanapowatukana] na kuwatesa . . . Mushangilie na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa sawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla [mbele] yenu.’ (Mathayo 5:11, 12) Mwishowe, kisha kupigwa sana, nilizimia.

Wakati niliamuka, nilijikuta katika chumba chenye baridi kali, bila chakula, maji, ao blanketi. Hata hivyo, nilijisikia kuwa salama na mwenye kutulia. Kama vile Biblia inaahidi, “amani ya Mungu” ilikuwa ‘inalinda fikira na moyo wangu.’ (Wafilipi 4:7) Siku yenye kufuata askari mumoja mwenye huruma alinipatia chakula na maji na koti ya baridi. Kisha askari mwengine alinipatia chakula chake. Katika njia hizo na njia zingine nyingi, niliona kuwa Yehova ananihangaikia kabisa.

Wenye mamlaka waliniona kuwa muasi mwenye hawezi kubadilika na wakanipeleka Athene ili nisambe kwenye tribinali ya kijeshi. Huko nilihukumiwa kifungo cha miaka tatu katika gereza lenye kuwa Yíaros (Gyaros), kisiwa chenye kuwa kwenye kilometre 50 mashariki mwa Makrónisos.

“TUNAWEZA KUWATUMAINIA”

Gereza la Yíaros lilikuwa gereza kubwa lenye kujengwa kwa matofali ya rangi nyekundu, na lilikuwa na wafungwa zaidi ya 5000 wenye walifungwa kwa sababu ya mambo ya politike. Lilikuwa pia na Mashahidi wa Yehova saba, na wote walikuwa wamefungwa kwa sababu walikataa kujiingiza katika mambo ya vita. Hata kama ilikatazwa kabisa, sisi Mashahidi saba tulikutana kwa siri ili kujifunza Biblia. Tulipata pia kwa ukawaida magazeti Munara wa Mulinzi kwa njia ya siri, kisha tulifanya kopi za magazeti hayo kwa kuandika kwa mukono na kuzitumia wakati wa funzo letu.

Siku moja wakati tulikuwa tunajifunza kwa siri, mulinzi mumoja wa gereza alituvumbua na akatunyanganya vichapo vyetu. Tuliitwa katika biro ya musimamizi wa gereza, na tuliwazia kabisa kuwa kifungo chetu kingerefushwa. Lakini, musimamizi huyo alisema hivi: “Tunawajua, na tunaheshimia musimamo wenu. Tunajua kama tunaweza kuwatumainia. Muende mutumike.” Alipatia hata wamoja kati yetu kazi zenye kuwa mwepesi. Tulikuwa wenye shukrani sana kwa Yehova. Hata katika gereza, ushikamanifu wetu wa Kikristo ulimuletea Yehova sifa.

Ushikamanifu wetu ulikuwa pia na matokeo mengine ya muzuri. Kisha kuangalia kwa uangalifu mwenendo wetu muzuri, mufungwa mumoja mwenye alikuwa mwalimu wa hesabu alichochewa kutuuliza juu ya imani yetu. Wakati sisi Mashahidi tuliachiliwa mwanzoni mwa mwaka wa 1951, yeye pia aliachiliwa. Kisha alifikia kuwa Shahidi wa Yehova na mweneza-injili wa wakati wote.

NINGALI ASKARI

Mimi na Janette, bibi yangu

Kisha kuachiliwa, nilirudia Karítsa kwenye familia yangu ilikuwa. Kisha, mimi pamoja na watu wengi wa eneo letu, tulihamia Melbourne, Australia. Huko nilikutana na Janette, dada muzuri Mukristo, na tukakomalisha mutoto mumoja mwanaume na watoto watatu wanawake katika njia ya Kikristo.

Leo, niko na zaidi ya miaka 90, na ninaendelea kuwa muzee wa kutaniko. Kwa sababu ya vidonda vyangu vya zamani, wakati fulani mwili wangu na miguu yangu vinaniuma, zaidi sana kisha kufanya kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, ninaazimia kabisa kuendelea kuwa “askari-jeshi mwema wa Kristo.”—2 Timotheo 2:3.