Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Nilikuwa Mukali Sana na Mwenye Jeuri

Nilikuwa Mukali Sana na Mwenye Jeuri
  • ALIZALIWA MWAKA WA 1974

  • INCHI: MEKSIKO

  • ALIKUWA: KIJANA MWENYE JEURI, NA MWENYE KUPIGANA NA WATU KWENYE BARABARA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa katika muji wa Ciudad Mante, muji wenye kupendeza wa jimbo la Tamaulipas, katika inchi ya Meksiko. Kwa kawaida, watu wa muji huo ni wakaribishaji-wageni na wema. Lakini jambo la kuhuzunisha ni kwamba, muji huo ulikuwa hatari sana kwa sababu ya vikundi vya watu wenye jeuri.

Nilikuwa mutoto wa pili kati ya watoto ine wanaume. Wazazi wangu walifanya nibatizwe katika Kanisa la Katoliki, na kisha nikajiunga na kikundi cha waimbaji wa parokia. Nilipenda kumufurahisha Mungu kwa sababu niliogopa sana kuhukumiwa na kuchomwa milele katika moto wa mateso.

Wakati nilikuwa na miaka tano, baba yetu alituacha. Hilo liliniletea huzuni sana na nikajisikia kuwa ninakosa kitu fulani katika moyo wangu. Sikuelewa juu ya nini baba alituacha kwa sababu tulikuwa tunamupenda sana. Mama yetu alipaswa kutumika saa nyingi mbali na kwetu ili kututimizia mahitaji yetu sisi watoto ine.

Ndiyo sababu nilikosa kuenda kwenye masomo ili kufanya urafiki na watoto wenye kunipita miaka. Walinifundisha kutukana, kuvuta tumbako, kuiba, na kupigana kwa kutumia ngumi. Kwa sababu nilipenda kutawala wengine, nilijifunza michezo mbalimbali ya kupigana kama vile kutumia ngumi, kuangushana chini kwa kutumia nguvu, na nilijifunza pia namna ya kutumia silaha mbalimbali. Nilifikia kuwa kijana mwenye jeuri. Mara nyingi nilikuwa katika vikundi vya watu wenye walipigana na vikundi vingine kwa kutumia bunduki, na mara nyingi nilikuwa mwenye kujaa damu na niliachwa karibu kufa kwenye barabara. Mama yangu alihuzunika sana wakati alinikuta katika hali hiyo na kunipeleka haraka kwenye hospitali.

Wakati nilikuwa na miaka 16, rafiki mumoja wa utoto mwenye kuitwa Jorge alitutembelea. Alituambia kwamba alikuwa Shahidi wa Yehova na kwamba alipenda kutuelezea ujumbe wa maana. Alianza kutufasiria mambo yenye aliamini, na alitumia Biblia ili kufanya hivyo. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kusikia mambo yenye alisoma, na nilifurahia kujifunza juu ya jina la Mungu na makusudi yake. Jorge alituonyesha kwamba iko tayari kujifunza Biblia pamoja na sisi. Tulikubali kujifunza.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Nilipata kitulizo wakati nilijua ukweli juu ya moto wa mateso. Nilielewa kwamba Biblia haifundishe hivyo. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5) Kisha kujua jambo hilo, sikuogopa tena Mungu kwa njia yenye haifae. Lakini, nilianza kumuona kuwa Baba mwenye upendo, mwenye anapenda watoto wake wakuwe na maisha mazuri.

Wakati niliendelea kufanya maendeleo katika funzo la Biblia, nilielewa kwamba nilipaswa kubadilisha tabia zangu. Nilipaswa kukomalisha sifa ya unyenyekevu na kuacha kuwa mwenye jeuri. Shauri lenye kupatikana katika 1 Wakorintho 15:33 lilinisaidia. Andiko hilo linasema hivi: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” Nilielewa kwamba kama nilipenda kubadilisha mwenendo wangu, nilipaswa kuacha kujiunga na watu wenye walinichochea kufanya mambo mabaya. Kwa hiyo, niliacha marafiki wangu wa zamani na kujiunga na ndugu na dada wa kutaniko la Kikristo, wenye walimaliza matatizo yao kwa kutumikisha kanuni za Biblia kuliko kumaliza matatizo yao kwa kupigana ao kutumia jeuri.

Andiko lingine la Biblia lenye lilinisaidia ni Waroma 12:17-19. Andiko hilo linasema hivi: ‘Musimulipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, mukuwe wenye kufanya amani na watu wote. . . . Musijilipizie kisasi, . . . kwa maana imeandikwa: Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’ Nilifikia kukubali kwamba Yehova atashugulikia ukosefu wa haki kwa njia na kwa wakati wenye kufaa. Polepole, niliachana na tabia yangu ya kuwa mwenye jeuri.

Sitasahau hata kidogo jambo lenye lilinifikia mangaribi moja wakati nilikuwa ninarudia nyumbani. Vijana wa kikundi chenye tulikuwa tunapigana nacho zamani walinishambulia, na kiongozi wao alinipiga kwenye mugongo na kusema kwa sauti, “Pigana tuone!” Wakati huo nilitoa sala fupi kwa Yehova. Nilimuomba anisaidie kuvumilia hali hiyo. Hata kama nilichochewa sana kuwarudishia, niliweza kuwakimbia kuliko kuwarudishia. Siku yenye kufuata, nilikutana kiongozi wa kikundi hicho peke yake. Nilikasirika sana na nilitaka kujilipizia kisasi, lakini tena niliomba Yehova katika moyo ili anisaidie kujizuia. Nilishangaa kuona kijana huyo anakuja kwenye niko na kusema: “Unihurumie kwa yote yenye ilitokea jana mangaribi. Kusema kweli, ninapenda kuwa kama wewe. Ninapenda kujifunza Biblia.” Nilifurahi kuona kwamba niliweza kuzuia hasira yangu! Kwa sababu nilifanya hivyo, yeye pia alianza kujifunza Biblia.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, watu wa familia yetu hawakuendelea kujifunza Biblia wakati huo. Lakini, nilishikamana na uamuzi wangu wa kuendelea kujifunza Biblia na sikuacha mutu yeyote ao jambo lolote linirudishe nyuma. Nilijua kwamba kuendelea kujiunga na watu wa Mungu kutaniponyesha maumivu yangu ya moyoni na kunipatia familia ya muzuri. Niliendelea kufanya maendeleo, na katika mwaka wa 1991, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

FAIDA YENYE NIMEPATA:

Nilikuwa mukali sana, mwenye kupenda kutawala wengine, na mwenye jeuri. Lakini Neno la Mungu limebadilisha kabisa maisha yangu. Sasa ninaelezea ujumbe wa Biblia wenye amani kila mutu mwenye iko tayari kusikiliza. Nimefanya miaka 23 katika pendeleo la kuwa mutumishi wa wakati wote.

Kwa muda fulani, nilifanya kazi ya kujitolea kwenye biro ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika inchi ya Meksiko. Wakati nilikuwa huko, tulijuana na dada Claudia, kijana mwanamuke Mukristo mwenye bidii, na tulioana katika mwaka wa 1999. Ninamushukuru sana Yehova kwa kunipatia mwanamuke huyo mwaminifu!

Tulitumika pamoja naye katika kutaniko la Luga ya Ishara ya Meksiko ili kusaidia watu wenye kuwa na magumu ya kusikia wamujue Yehova. Kisha, tuliombwa kuenda katika inchi ya Belize ili kufundisha watu Biblia. Hata kama tunaishi maisha mepesi, tuko na yote yenye tuko nayo lazima ili kuwa na furaha. Hatuwezi kubadilisha furaha hiyo na kitu chochote.

Kisha muda fulani, mama yangu alianza tena kujifunza Biblia na kufikia kubatizwa. Pia, ndugu yangu mukubwa, bibi yake, na watoto wake wako sasa Mashahidi wa Yehova. Wamoja kati ya marafiki wangu wa zamani wenye nilihubiria ujumbe wa Ufalme, wanamutumikia pia Yehova leo.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, watu fulani wa familia yetu walikufa kwa sababu hawakuacha tabia yao yenye jeuri. Kama niliendelea na tabia hiyo pia, pengine mimi pia singekuwa muzima leo. Ninamushukuru Yehova kwa kunivuta kwake na kwa watumishi wake, wenye walinifundisha kutumikisha kanuni za Biblia katika maisha yangu. Walifanya hivyo kwa uvumilivu na wema.