Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Walijitoa kwa kujipendea—Katika Mexique

Walijitoa kwa kujipendea—Katika Mexique

NI JAMBO lenye kutia moyo kuona hesabu inayoongezeka ya Mashahidi vijana wanaorahisisha maisha yao ili wahubiri zaidi. (Mt. 6:22) Wanafanya mabadiliko gani? Ni matatizo gani wanayopambana nayo? Ili kujibu maulizo hayo, acheni tuzungumuzie ndugu na dada fulani wanaotumikia sasa huko Mexique.

“TULIPASWA KUFANYA MABADILIKO FULANI”

Dustin na Jassa

Dustin na Jassa wa États-Unis walifunga ndoa Mwezi wa 1, 2007. Kisha muda kidogo, walifanya jambo ambalo walitamani kufanya tangu zamani, ni kusema, kununua mashua na kuishi ndani kwa mwaka mumoja. Walisimamisha mashua yao karibu na Astoria, huko Oregon, États-Unis, muji wenye kupendeza unaozungukwa na milima midogo yenye misitu na milima mirefu yenye kufunikwa na teluji, karibu tu na Bahari ya Pasifike. Dustin anasema kwamba “eneo hilo lilikuwa lenye kupendeza upande wote!” Yeye na bibi yake walifikiri kwamba waliishi maisha mepesi, na kwamba walimutegemea Yehova. Kisha walianza kuwaza hivi: ‘Kwa kweli tunaishi katika mashua yenye urefu wa metre 8 hivi, hatutumike saa nyingi, tunakusanyika katika kutaniko linalozungumuza luga ya kigeni, na wakati fulani tunafanya upainia musaidizi.’ Lakini kisha muda mufupi, walitambua kama walikuwa wanajidanganya. Dustin anasema hivi: “Kuliko kutegemeza mipango ya kutaniko, tulipitisha wakati mwingi kutengeneza mashua yetu. Kwa hiyo, tulitambua kwamba ikiwa tulitaka kabisa kumutia Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu, tulipaswa kufanya mabadiliko fulani.”

Dada Jassa anaongezea hivi: “Mbele ya kuolewa niliishi Mexique, ambako nilikusanyika katika kutaniko la Kiingereza. Nilifurahia kutumikia huko, na nilikuwa na hamu ya kurudi huko.” Ili kutia nguvu tamaa yao ya kutumikia katika inchi nyingine, Dustin na Jassa walisoma, wakati wa ibada yao ya familia, masimulizi ya maisha ya ndugu na dada waliohamia katika maeneo ambamo mavuno yalikuwa tayari kukusanywa. (Yoh. 4:35) Dustin anasema hivi: “Tulitaka kuwa na furaha kama yao.” Marafiki wao wa Mexique walipowajulisha kwamba kulikuwa kikundi kipya kilichohitaji musaada, Dustin na Jassa waliamua kuenda huko ili kusaidia. Waliacha kazi zao, waliuzisha mashua yao, na walihamia Mexique.

“JAMBO NZURI SANA KATIKA MAISHA YETU”

Dustin na Jassa walienda kuishi katika muji wa Tecomán, karibu na Bahari ya Pasifike lakini umbali wa kilometre 4345 kusini mwa Astoria. Dustin anasema hivi: “Mahali hapo hapakuwa upepo na milima yenye kufurahisha, tuliishi sasa katika joto nyingi na miti ya ndimu ilikuwa mahali popote.” Mwanzoni, hawakupata kazi. Kwa kuwa hawakuwa na feza za kutosha, walikula wali na maharagi mara mbili kila siku. Jassa anasema hivi: “Lakini chakula hicho kilipoanza kutuchokesha, wanafunzi wetu wa Biblia walianza kutupatia mahembe, ndizi, papai, na vilevile vifuko vyenye kujaa ndimu!” Baadaye, Dustin na bibi yake walipata kazi katika masomo inayofundisha luga kwa njia ya Internete, masomo inayopatikana huko Taïwan. Feza wanazopata sasa katika kazi hiyo zinawasaidia kutosheleza mahitaji yao ya kila siku.

Dustin na Jassa wanaona maisha yao mapya namna gani? Wanasema hivi: “Kuhamia hapa ni jambo nzuri sana katika maisha yetu. Uhusiano wetu na Yehova na uhusiano kati yetu ni muzuri zaidi kuliko namna tulivyowazia. Kila siku tunafanya mambo mengi pamoja kama vile kuhubiri, kuzungumuzia namna tunavyoweza kusaidia wanafunzi wetu wa Biblia, kutayarisha mikutano. Pia, hatuna mahangaiko tuliyokuwa nayo zamani. Tunajua sasa kwamba zamani hatukuelewa kabisa ukweli wa ahadi inayopatikana katika Zaburi 34:8, ‘Onjeni muone ya kuwa Yehova ni mwema.’”

NI NINI ILIWACHOCHEA WAHUBIRI WENGI WAJITOLEE?

Ndugu na dada zaidi ya 2 900, bibi na bwana na wengine ambao hawajafunga ndoa, wengi wakiwa kati ya miaka 20 na 30 wamehamia katika maeneo ya Mexique ambayo ingali na lazima kubwa ya wahubiri wa Ufalme. Sababu gani Mashahidi hao wote wameazimia kufanya kazi hiyo? Wamoja kati yao walipoulizwa ulizo hilo, walitoa sababu kubwa tatu. Ni sababu gani hizo?

Leticia na Hermilo

Ili kuonyesha upendo kwa Yehova na kwa jirani. Leticia aliyekuwa na miaka 18 alipobatizwa, anasema hivi: “Nilipojitoa katika sala kwa Yehova, nilielewa kwamba hilo linamaanisha kumutumikia kwa moyo wangu wote na nafsi yangu yote. Kwa hiyo, ili kuonyesha kwamba ninamupenda kwa moyo wangu wote, niliona ni vizuri kutumia wakati na nguvu nyingi katika kazi yake.” (Mk. 12:30) Hermilo, ambaye sasa amemuoa Leticia, alikuwa na miaka 20 hivi alipohamia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri wa Ufalme. Anasema hivi: “Nilitambua kwamba kuwasaidia wengine watosheleze mahitaji yao ya kiroho ilikuwa njia nzuri sana ya kuonyesha upendo kwa jirani.” (Mk. 12:31) Kwa hiyo, aliacha muji wenye kuendelea wa Monterrey, ambako alitumika katika banke na alikuwa na maisha mazuri, na akahamia katika muji mudogo.

Essly

Ili Kupata furaha ya kweli na yenye kudumu. Muda mufupi tu kisha kubatizwa, Leticia alienda kuhubiri kwa mwezi mumoja na dada mumoja painia wa siku nyingi katika muji wa mbali. Leticia anakumbuka hivi: “Nilishangaa sana. Nilifurahi sana kuona namna watu walivyokubali ujumbe tuliowatolea. Mwezi huo ulipomalizika, nilijiambia hivi: ‘Hii ndiyo kazi ninayotaka kufanya katika maisha yangu!’” Vilevile, Essly, dada asiyeolewa aliye na miaka 20 hivi, alihamia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri kwa sababu ya furaha aliyojionea. Alipokuwa angali kwenye masomo ya segondere alikutana na Wakristo fulani wenye bidii ambao walitumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri. Anasema hivi: “Nilipoona furaha ya ndugu na dada hao, nilitaka kuwa kama wao.” Dada wengi walitenda kama dada Essly. Kwa hiyo, huko Mexique kuna zaidi ya dada 680 wasioolewa wanaotumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri. Dada hao wanatuwekea sisi wote mufano muzuri!

Ili kuishi maisha yenye kusudi la kweli na furaha. Kisha kumaliza masomo ya segondere, dada Essly alipewa nafasi ya kusoma bure masomo ya juu. Marafiki walimutia moyo asome na afuatie “maisha ya kawaida,” ni kusema, kupata diplome ya masomo ya juu, kazi nzuri, motokari, na kutembelea inchi za kigeni. Lakini, hakuwasikiliza. Dada Essly anasema hivi: “Wengi kati ya marafiki wangu Wakristo walifuatia mambo hayo, na nilitambua kwamba miradi ya kiroho haikuwa tena jambo la lazima katika maisha yao. Nilitambua pia kwamba mwishowe walipata matatizo walipojiingiza zaidi na zaidi katika mambo ya ulimwengu. Nilitaka kutumia ujana wangu ili kumutumikia Yehova kwa moyo wangu wote.”

Racquel na Phillip

Dada Essly alisoma masomo fulani ya muda mufupi ambayo yalimusaidia kupata kazi ili ajitegemeze katika kazi ya upainia, na kisha alihamia mahali ambapo kulikuwa lazima kubwa ya wahubiri wa Ufalme. Alijikaza pia kujifunza luga za kienyeji za Waatomi na Watlapaneko. Sasa, anapokumbuka miaka mitatu aliyopitisha katika maeneo ya mbali, anasema hivi: “Kutumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri kumeniletea furaha na maisha yangu yamekuwa na kusudi kabisa. Zaidi sana, kumetia nguvu uhusiano wangu na Yehova.” Phillip na bibi yake Racquel, wa États-Unis walio na miaka 30 hivi wanakubaliana na jambo hilo. “Ulimwengu unabadilika haraka na watu wanafikiri kwamba maisha yao yanabadilika​-badilika. Lakini kuhubiri mahali ambapo tunapata watu wengi wanaosikiliza ujumbe wa Biblia kunafanya tuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Maisha yanakuwa yenye kufurahisha sana!”

NAMNA YA KUPAMBANA NA MATATIZO

Verónica

Bila shaka, si rahisi kutumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri. Tatizo moja ni namna ya kupata feza ili kutosheleza mahitaji ya kimwili. Ili kupambana na tatizo hilo, unapaswa kuwa tayari kuzoea hali za eneo unamotumikia. Dada Verónica, painia wa miaka mingi, anaeleza hivi: “Nilipokuwa katika eneo moja, nilipika na kuuzisha vyakula vyepesi vya bei chini. Katika eneo lingine, niliuzisha nguo na kusuka nywele. Sasa, ninafanya kazi ya kusafisha nyumba na kufundisha wazazi wapya namna ya kuzungumuza na watoto wao.”

Inaweza kuwa vigumu kuzoea desturi na tabia za wenyeji wa eneo la mbali. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Phillip na Racquel walipotumikia katika eneo ambamo luga ya Nahuatl inazungumuzwa. Phillip anasema hivi: “Desturi zetu zilitofautiana sana.” Ni nini iliwasaidia kuzoea? Phillip anasema hivi: “Tulifikiria zaidi sana mambo mazuri tuliyojionea kwa watu hao wanaozungumuza luga ya Nahuatl, ni kusema, umoja wa familia zao, namna walivyotendeana vizuri, na sifa yao ya kutoa.” Racquel anaongeza hivi: “Maisha ya ndugu na dada wenyeji wa eneo hilo yalitufundisha mambo mengi.”

KUJITAYARISHA

Ikiwa unataka kutumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri, unaweza kujitayarisha namna gani? Ndugu na dada ambao wamefanya hivyo wanashauri hivi: Mbele ya kuhama, rahisisha kwanza maisha yako na ujifunze kutosheka na mambo ulio nayo. (Flp. 4:11, 12) Unaweza tena kufanya nini? Leticia anaeleza hivi: “Niliepuka kazi ambazo zilinifanya nibaki mahali pamoja kwa muda murefu. Nilitaka kuwa tayari kuenda wakati wowote na mahali popote ilipohitajika.” Ndugu Hermilo anasema: “Nilijifunza kupika chakula, kufua nguo, na kupiga nguo pasi.” Dada Verónica anaeleza hivi: “Nilipokuwa ningali nyumbani na wazazi na ndugu na dada zangu, nilisaidia kusafisha nyumba na nilijifunza kutayarisha chakula cha bei chini lakini chenye kujenga mwili. Nilijifunza pia kutumia feza vizuri.”

Amelia na Levi

Levi na Amelia wa États-Unis na ambao wamefunga ndoa miaka munane iliyopita wanaeleza namna ambayo kusali kuhusu tamaa yao ya kuenda kutumikia huko Mexique kulivyowasaidia kujitayarisha. Ndugu Levi anasema hivi: “Tulikadiria ni kiasi gani cha feza tunachoweza kutumia kwa mwaka mumoja katika inchi ya kigeni na tulimuomba Yehova atusaidie kupata kiasi hicho tu.” Kwa miezi fulani, walipata kiasi hicho cha feza ambacho walimuomba Yehova awasaidie kukipata, na walienda bila kukawia. Ndugu Levi anasema tena hivi: “Yehova alijibu ombi letu, kwa hiyo wakati huo tulipaswa kufanya mambo tuliyomuahidi.” Dada Amelia anaongezea hivi: “Tulifikiri kwamba tutapitisha hapa mwaka mumoja tu, lakini sasa tumepitisha miaka saba hapa, na hatutaki kuondoka! Tumejionea namna Yehova anavyotusaidia. Kila siku, tunajionea mambo yanayotusadikisha kwamba Yehova ni mwema.”

Adam na Jennifer

Sala iliwasaidia pia Adam na bibi yake Jennifer wa États-Unis, wanaotumikia katika eneo la Kiingereza huko Mexique. Wanashauri hivi: “Usingoje mupaka hali iwe nzuri kabisa. Sali kuhusu tamaa yako ya kutumikia mahali ambapo kuna lazima kubwa ya wahubiri na tenda kulingana na sala yako. Rahisisha maisha yako, julisha biro ya tawi ya inchi ambamo unataka kutumikia, na kisha kuhesabu garama, funga safari!” * Ukifanya hivyo, utapata baraka nyingi za kiroho.

^ Kwa kujua mengi zaidi, soma habari “Je, ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Mwezi wa 8, 2011.