Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 57

Yesu Anaponyesha Mutoto Mwanamuke na Mwanaume Mwenye Kuwa Kiziwi

Yesu Anaponyesha Mutoto Mwanamuke na Mwanaume Mwenye Kuwa Kiziwi

MATAYO 15:21-31 MARKO 7:24-37

  • YESU ANAPONYESHA BINTI YA MWANAMUKE FULANI MUFOINIKE

  • ANAPONYESHA MWANAUME FULANI KIZIWI NA MWENYE KUWA BUBU

Kisha kuonyesha waziwazi desturi za Wafarisayo zenye wametia kwa faida yao wenyewe, Yesu anaondoka pamoja na wanafunzi wake. Anaenda katika maeneo ya Tiro na Sidoni katika Foinike, kwenye kilometre nyingi upande wa kaskazini-mangaribi.

Yesu anapata nyumba mwenye anaweza kukaa lakini hapendi watu wajue kuwa iko katika eneo hilo. Hata hivyo, watu wanafikia kujua. Mwanamuke mumoja Mugiriki mwenye alizaliwa katika eneo hilo anamuona Yesu na kuanza kumuomba hivi: “Unisikilie huruma, Bwana, Mwana wa Daudi. Binti yangu anasumbuliwa sana na pepo muchafu.”—Matayo 15:22; Marko 7:26.

Kisha wakati fulani, wanafunzi wanamuomba Yesu hivi: “Muambie aende, kwa sababu anaendelea kufanya makelele nyuma yetu.” Yesu anaeleza sababu yenye inafanya asihangaikie mwanamuke huyo. Anasema hivi: “Nimetumwa tu kwa kondoo wenye kupotea wa nyumba ya Israeli.” Lakini mwanamuke huyo hachoke. Anakaribia na kuinama mbele ya Yesu, na kumuomba hivi: “Bwana, nisaidie!”—Matayo 15:23-25.

Pengine ili kujaribu imani ya mwanamuke huyo, Yesu anafikiria mawazo ya mubaya yenye Wayahudi wako nayo juu ya watu wa mataifa mengine na kusema hivi: “Haiko sawa kukamata mukate wa watoto na kuutupia imbwa wadogo.” (Matayo 15:26) Wakati anazungumuzia “imbwa wadogo,” Yesu anaonyesha kuwa iko na huruma nyingi juu ya watu wenye hawako Wayahudi. Pia, sura yake na maneno yake vinaonyesha kabisa sifa hiyo ya huruma.

Kuliko kukwazika na maneno ya Yesu, mwanamuke huyo anafikiria mawazo yenye ubaguzi ya Wayahudi na kusema hivi kwa unyenyekevu: “Ndiyo Bwana, lakini hata hao imbwa wadogo wanakula vipande vya chakula vyenye kuanguka kutoka kwenye meza ya mabwana wao.” Yesu anatambua kuwa mwanamuke huyo iko na moyo muzuri, na anasema hivi: “Ee mwanamuke, imani yako ni kubwa; na itendeke kwako kama vile unataka.” (Matayo 15:27, 28) Na inakuwa hivyo, hata kama mutoto wake mwanamuke haiko pale! Wakati mwanamuke huyo anarudia nyumbani kwake, anakuta mutoto wake mwanamuke kwenye kitanda, amepona kabisa; “ule pepo muchafu alikuwa ametoka”!—Marko 7:30.

Yesu na wanafunzi wake wanatoka katika eneo la Foinike na wanaenda upande wa Muto Yordani. Inawezekana wanavuka Yordani kupitia mahali fulani kwenye upande wa kaskazini mwa Bahari ya Galilaya na kuenda katika eneo la Dekapoli. Huko, wanaenda kwenye mulima fulani, lakini watu wanawaona. Watu hao wanamuletea Yesu viwete, vilema, vipofu, na mabubu. Wanaweka watu hao kwenye miguu ya Yesu, na anawaponyesha. Watu hao wanashangaa na wanatukuza Mungu wa Israeli.

Yesu anakazia uangalifu wake mwanaume mumoja mwenye ni kiziwi na ambaye iko na tatizo la kusema. Waza namna mutu huyo anapaswa kujisikia kati ya watu hao wengi sana. Pengine Yesu anaona namna mwanaume huyo anahangaika, ndiyo sababu anamukamata na kuenda naye pembeni, mbali na watu. Wakati wako peke yao, Yesu anaonyesha kile anakata kumufanyia mwanaume huyo. Anaweka vidole vyake katika masikio ya mwanaume huyo na, kisha kutema mate, anagusa ulimi wa mwanaume huyo. Kisha Yesu anaangalia mbinguni na kusema “Efata”, maneno yenye yanamaanisha “Funguka.” Kwa hiyo, mwanaume huyo anaanza kusikia na kusema kama kawaida. Yesu hapendi watu wajue jambo hilo, anapenda watu wamuamini kupitia mambo yenye wanaona na kusikia wao wenyewe.—Marko 7:32-36.

Uwezo wa Yesu wa kufanya miujiza kama hiyo unafanya watu wenye walikuwa wanaona ‘washangae sana.’ Wanasema hivi: “Amefanya mambo yote muzuri. Hata anafanya viziwi wasikie na mabubu waseme.”—Marko 7:37.