Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA

Jinsi ya Kuonyesha Upendo

Jinsi ya Kuonyesha Upendo

 Kadiri miaka inavyopita, baadhi ya wenzi wa ndoa hupunguza kadiri wanavyoonyeshana upendo. Je, unapaswa kuhangaika ikiwa hilo linatokea katika ndoa yako?

 Unachopaswa kujua

 Kuonyesha upendo ni muhimu ili kuwa na ndoa imara. Kama tu ilivyo muhimu sana kupata chakula na maji kwa ukawaida ili mwili wako uwe na nguvu na afya, ndivyo kuonyesha upendo kwa ukawaida kunavyoboresha na kuimarisha ndoa. Miaka mingi baada ya arusi, waume na wake wanahitaji kuhakikishiwa kwa ukawaida kwamba wenzi wao wanawapenda sana na kuwajali.

 Upendo wa kweli hauna ubinafsi. Upendo unajitahidi kumfurahisha yule mtu mwingine. Hivyo, badala ya kuonyesha upendo kwa kushtukiza tu, mwenzi mwenye ufikirio atazingatia kwamba mwenzi wake anahitaji kuonyeshwa upendo na atajitahidi kutosheleza uhitaji huo.

 Kwa ukawaida, wake wanahitaji kuonyeshwa upendo zaidi kuliko waume. Mume anaweza kuwa anampenda sana mke wake. Lakini akimwonyesha upendo huo asubuhi na usiku peke yake au kabla ya kufanya ngono tu, huenda mke asiwe na uhakika ikiwa kweli anamjali. Inafaa zaidi kumwonyesha upendo mara nyingi kila siku.

 Unachoweza kufanya

 Onyesha upendo kwa maneno. Maneno rahisi kama vile “Nakupenda” au “Wewe ni mtu muhimu sana kwangu” yanaweza kumfanya mwenzi wako ahisi anathaminiwa sana.

 Kanuni ya Biblia: “Kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni.”​—Mathayo 12:34.

 Dokezo: Usiseme tu maneno yanayoonyesha kwamba unampenda mwenzi wako. Mwandikie pia​—barua, barua-pepe, au ujumbe mfupi kupitia simu.

 Mwonyeshe upendo kwa matendo. Kumkumbatia, kumbusu, au kumshika mkono kunaweza kuonyesha kwamba unasema kweli unapomwambia, “Ninakupenda.” Kumgusa kwa wororo, kumtazama kwa upendo, au kumpa zawadi mara kwa mara kunaweza kuonyesha kwamba unamjali kikweli. Namna gani ikiwa pia utafanya mambo fulani kumsaidia mke wako​—labda kumbebea mifuko, kumfungulia mlango, kuosha vyombo, kufua nguo, au kupika? Kwa wengi, mambo hayo si msaada tu​—ni njia ya kuonyesha upendo!

 Kanuni ya Biblia: “Tunapaswa kupendana, si kwa neno au kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”​—1 Yohana 3:​18.

 Dokezo: Mtendee mwenzi wako kwa ufikirio kama ulivyofanya mlipokuwa mkichumbiana.

 Tenga wakati wa kuwa na mwenzi wako. Kutenga wakati wa kuwa peke yenu kunaimarisha ndoa yenu na kumhakikishia mwenzi wako kwamba unafurahia kuwa pamoja naye. Bila shaka, huenda ikawa vigumu kupanga kuwa peke yenu ikiwa mna watoto au ikiwa kuna shughuli nyingi za lazima za kuzungumzia kila siku. Labda mnaweza kupanga kufanya jambo fulani dogo kama kutembea kwa ukawaida​—mkiwa wawili tu.

 Kanuni ya Biblia: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”​—Wafilipi 1:​10.

 Dokezo: Wenzi fulani wa ndoa wenye shughuli nyingi hutenga usiku wa kwenda mkahawani kwa ukawaida au miisho juma ili kuwa pamoja.

 Mfahamu mwenzi wako. Kila mtu ana mahitaji yake binafsi ya kuonyeshwa upendo. Zungumzieni jinsi ambavyo mngependa kuonyeshwa upendo na ikiwa yeyote kati yenu anahisi angependa kuonyeshwa upendo zaidi. Kisha, jitahidi sana kutimiza uhitaji wa mwenzi wako. Kumbuka, ni muhimu kwa wenzi wa ndoa kuonyeshana upendo ili ndoa iwe imara.

 Kanuni ya Biblia: “Upendo . . . hautafuti faida zake wenyewe.”​—1 Wakorintho 13:4, 5.

 Dokezo: Badala ya kumlazimisha mwenzi wako akuonyeshe upendo, jiulize, ‘Ninaweza kufanya nini ili mwenzi wangu anionyeshe upendo zaidi?’