Kulingana na Mathayo 12:1-50

  • Yesu ndiye “Bwana wa Sabato” (1-8)

  • Mtu mwenye mkono uliopooza aponywa (9-14)

  • Mtumishi mpendwa wa Mungu (15-21)

  • Atumia roho takatifu kuwafukuza roho waovu (22-30)

  • Dhambi isiyosamehewa (31, 32)

  • Mti hujulikana kwa matunda yake (33-37)

  • Ishara ya Yona (38-42)

  • Roho mwovu anaporudi (43-45)

  • Mama na ndugu za Yesu (46-50)

12  Wakati huo, Yesu alipitia katikati ya mashamba ya nafaka siku ya Sabato. Wanafunzi wake wakahisi njaa wakaanza kukata masuke ya nafaka na kula.+  Mafarisayo walipoona hilo, wakamwambia: “Tazama! Wanafunzi wako wanafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato.”+  Yesu akawaambia: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi wakati yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye walipohisi njaa?+  Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, nao wakala mikate ya toleo,*+ kitu ambacho hakikuwa halali kwake au kwa wale waliokuwa pamoja naye kula, ila makuhani tu?+  Au, je, hamjasoma katika Sheria kwamba siku ya Sabato makuhani huvunja Sabato na wanabaki bila hatia?+  Lakini ninawaambia, hapa pana mtu mkuu kuliko hekalu.+  Hata hivyo, kama mngeelewa maana ya maneno haya, ‘Ninataka rehema+ si dhabihu,’+ hamngewalaumu watu wasio na hatia.  Kwa maana Mwana wa binadamu ndiye Bwana wa Sabato.”+  Baada ya kutoka hapo, akaingia ndani ya sinagogi lao, 10  na tazama! kulikuwa na mtu aliyepooza mkono!+ Basi, ili wapate sababu ya kumshtaki wakamuuliza, “Je, ni halali kumponya mtu siku ya Sabato?”+ 11  Akawaambia: “Ukiwa na kondoo mmoja, naye kondoo huyo atumbukie shimoni siku ya Sabato, je, kuna yeyote kati yenu ambaye hatamshika na kumtoa humo?+ 12  Kwa kweli, mwanadamu ni mwenye thamani sana kuliko kondoo! Basi ni halali kutenda mema siku ya Sabato.” 13  Kisha akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukawa mzima kama ule mkono mwingine. 14  Lakini Mafarisayo wakaenda nje na kupanga njama ili wamuue. 15  Yesu alipojua jambo hilo, akaondoka hapo. Watu wengi wakamfuata,+ naye akawaponya wote, 16  lakini akawaagiza kwa kusisitiza wasimtangaze,+ 17  ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Isaya: 18  “Tazama! Mtumishi wangu+ niliyemchagua, mpendwa wangu, ambaye nimemkubali!*+ Nitaweka roho yangu juu yake,+ naye atayatangazia mataifa haki. 19  Hatagombana+ wala kupiga kelele, wala yeyote hatasikia sauti yake kwenye barabara kuu. 20  Hataponda tete lililovunjika, wala hatazima utambi unaofifia,+ hadi atakapofanikiwa kuleta haki. 21  Kwa kweli, mataifa yatalitumainia jina lake.”+ 22  Kisha wakamletea mwanamume kipofu aliyekuwa bubu kwa sababu alikuwa na roho mwovu, Yesu akamponya, na yule bubu akaanza kuongea na kuona. 23  Basi, umati wote ukashangaa na kusema: “Je, inawezekana kwamba huyu ndiye Mwana wa Daudi?” 24  Mafarisayo waliposikia jambo hilo wakasema: “Mtu huyu anawafukuza roho waovu kwa nguvu za Beelzebuli,* mtawala wa roho waovu.”+ 25  Akijua fikira zao, akawaambia: “Kila ufalme uliogawanyika dhidi yake wenyewe utaangamia, na kila jiji au nyumba iliyogawanyika dhidi yake yenyewe haitasimama. 26  Vivyo hivyo, ikiwa Shetani anamfukuza Shetani, amegawanyika dhidi yake mwenyewe; basi, ufalme wake utawezaje kusimama? 27  Zaidi ya hayo, ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia Beelzebuli, wana wenu wanawafukuza kupitia nani? Hiyo ndiyo sababu watakuwa waamuzi wenu. 28  Lakini ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia roho ya Mungu, kwa kweli Ufalme wa Mungu umewafikia ninyi ghafla.+ 29  Au yeyote anawezaje kuivamia nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuchukua mali zake isipokuwa kwanza amfunge mtu huyo? Hapo ndipo anaweza kuipora nyumba yake. 30  Yeyote asiye upande wangu ananipinga, na yeyote asiyekusanya pamoja nami anatawanya.+ 31  “Kwa hiyo mimi ninawaambia, watu watasamehewa kila aina ya dhambi na makufuru, lakini yeyote anayekufuru roho takatifu hatasamehewa.+ 32  Kwa mfano, yeyote anayesema neno baya dhidi ya Mwana wa binadamu, atasamehewa;+ lakini yeyote anayesema vibaya dhidi ya roho takatifu, hatasamehewa, hapana, si katika mfumo huu wa mambo* wala ule utakaokuja.+ 33  “Ufanyeni mti kuwa mzuri na matunda yake yawe mazuri, au muufanye mti uoze na matunda yake yaoze, kwa maana mti hujulikana kwa matunda yake.+ 34  Uzao wa nyoka,*+ mnawezaje kusema mambo mema, wakati ninyi ni waovu? Kwa maana kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni.+ 35  Mtu mwema hutoa mambo mema katika hazina yake njema, lakini mtu mwovu hutoa mambo mabaya katika hazina yake mbovu.+ 36  Ninawaambia kwamba katika Siku ya Hukumu watu watatoa hesabu+ kuhusu kila neno lisilofaa wanalosema; 37  kwa maneno yako utatangazwa kuwa mwadilifu, na kwa maneno yako utahukumiwa.” 38  Ndipo baadhi ya waandishi na Mafarisayo wakamjibu kwa kumwambia: “Mwalimu, tunataka kuona ishara kutoka kwako.”+ 39  Akawajibu: “Kizazi kiovu na chenye uzinzi* kinaendelea kutafuta ishara, lakini hakitapewa ishara yoyote isipokuwa ishara ya nabii Yona.+ 40  Kwa maana kama vile Yona alivyokuwa katika tumbo la samaki mkubwa kwa siku tatu mchana na usiku,+ ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa katika moyo wa ardhi siku tatu mchana na usiku.+ 41  Watu wa Ninawi watasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki nao watakihukumu, kwa sababu walitubu Yona alipowahubiria.+ Lakini tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Yona.+ 42  Malkia wa kusini atasimamishwa katika hukumu pamoja na kizazi hiki naye atakihukumu, kwa sababu alikuja kutoka miisho ya dunia ili asikie hekima ya Sulemani.+ Lakini tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Sulemani.+ 43  “Roho mwovu anapomtoka mtu, yeye hupitia maeneo yasiyo na maji akitafuta mahali pa kupumzika, lakini hapati.+ 44  Kisha anasema, ‘Nitarudi kwenye nyumba yangu niliyoihama’; naye anapofika, anakuta haijakaliwa lakini imefagiwa ikawa safi na kupambwa. 45  Naye huenda na kuwaleta roho wengine saba walio waovu kuliko yeye, na baada ya kuingia ndani, wao hukaa humo; na hali ya mwisho ya mtu huyo huwa mbaya zaidi kuliko ya kwanza.+ Hivyo ndivyo itakavyokuwa pia kwa kizazi hiki kiovu.” 46  Alipokuwa bado akizungumza na umati, mama yake na ndugu zake+ walikuwa wamesimama nje, wakitaka kuongea naye.+ 47  Basi mtu fulani akamwambia: “Tazama! Mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kuongea nawe.” 48  Yesu akamjibu mtu huyo: “Mama yangu ni nani, na ndugu zangu ni nani?” 49  Akinyoosha mkono wake kuelekea wanafunzi wake, akasema: “Tazama! Mama yangu na ndugu zangu!+ 50  Kwa maana yeyote anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu, dada yangu, na mama yangu.”+

Maelezo ya Chini

Au “mikate iliyowekwa mbele za Mungu.”
Au “nafsi yangu imemkubali.”
Jina lingine la Shetani.
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “nyoka-vipiri.”
Au “kisicho na uaminifu.”