Hamia kwenye habari

“Alfa na Omega” Ni Nani au Ni Nini?

“Alfa na Omega” Ni Nani au Ni Nini?

Jibu la Biblia

 “Alfa na Omega” ni Yehova Mungu, Mweza-Yote. Maneno hayo yanapatikana mara tatu katika Biblia.​—Ufunuo 1:8; 21:6; 22:13. a

Kwa nini Mungu anajiita “Alfa na Omega”?

 Alfa na omega ndiyo herufi ya kwanza na ya mwisho katika alfabeti ya Kigiriki, lugha iliyotumiwa kuandika sehemu ya Biblia ambayo kwa kawaida inaitwa Agano Jipya, inayotia ndani kitabu cha Ufunuo. Kwa kuwa herufi hizo zinapatikana mwanzo na mwisho wa alfabeti ya Kigiriki zinatumiwa kuonyesha kwamba Yehova peke yake ndiye mwanzo na mwisho. (Ufunuo 21:6) Alikuwa Mungu Mweza-Yote tangu zamani, naye ataendelea kuwa Mungu Mweza-Yote milele. Yeye peke yake ndiye aliyepo “tangu milele hadi milele.”​—Zaburi 90:2.

Ni nani aliye ‘wa kwanza na wa mwisho’?

 Biblia inatumia maneno hayo kumhusu Yehova Mungu na pia kumhusu Mwana wake, Yesu, lakini katika maana tofauti. Fikiria mifano miwili.

  •   Kwenye Isaya 44:6, Yehova anasema: “Mimi ndiye wa kwanza na mimi ndiye wa mwisho. Hakuna Mungu ila mimi.” Hapa Yehova anakazia kwamba yeye ndiye Mungu wa kweli wa milele; mbali naye, hakuna mwingine. (Kumbukumbu la Torati 4:​35, 39) Katika kisa hiki, maneno “wa kwanza na . . . wa mwisho” yana maana ileile kama “Alfa na Omega.”

  •   Isitoshe, maneno “wa Kwanza [pro’tos, si alfa] na wa Mwisho [e’skha·tos, si omega]” yanapatikana kwenye Ufunuo 1:​17, 18 na 2:8. Katika mistari hiyo, muktadha unaonyesha kwamba anayeelezewa alikufa kisha akarudi kuwa hai. Hivyo, mistari hiyo haiwezi kuwa inamrejelea Mungu kwa kuwa yeye hajawahi kufa. (Habakuki 1:​12) Hata hivyo, Yesu alikufa na kufufuliwa. (Matendo 3:​13-​15) Alikuwa mwanadamu wa kwanza kufufuliwa na kupewa uhai usioweza kufa mbinguni, ambako sasa anaishi “milele na milele.” (Ufunuo 1:​18; Wakolosai 1:​18) Baada ya hapo, Yesu ndiye anayeshughulikia ufufuo mwingine wote. (Yohana 6:​40, 44) Hivyo, alikuwa wa mwisho kufufuliwa moja kwa moja na Yehova. (Matendo 10:40) Katika maana hiyo, Yesu anastahili kuitwa “wa Kwanza na wa Mwisho.”

Je, Ufunuo 22:13 inathibitisha kwamba Yesu ndiye “Alfa na Omega”?

 Hapana. Msemaji wa Ufunuo 22:13 hatambulishwi moja kwa moja, na kuna wasemaji kadhaa katika sura hiyo. Akizungumza kuhusu sehemu hiyo ya Ufunuo, Profesa William Barclay aliandika hivi: “Mambo hayajaandikwa kwa mpangilio wowote; . . . na mara nyingi ni vigumu kujua msemaji mkuu ni nani.” (Ufunuo wa Yohana, Buku la 2, Toleo Lililorekebishwa, ukurasa wa 223) Hivyo, “Alfa na Omega” anayetajwa kwenye Ufunuo 22:13 anaweza kutambuliwa kuwa Mtu yuleyule aliyepewa jina hilo sehemu nyingine za Ufunuo​—Yehova Mungu.

a Maneno hayo yanaonekana mara ya nne katika Ufunuo 1:​11 kwenye Biblia ya King James Version. Hata hivyo, maneno hayo hayapatikani katika tafsiri nyingi za kisasa kwa sababu hayapatikani katika hati za Kigiriki za zamani zaidi lakini inaonekana yaliongezwa katika nakala za baadaye za Maandiko.