Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutoa?

Jibu la Biblia

 Biblia inatutia moyo kutoa kwa hiari na kwa nia nzuri. Inaonyesha kwamba kutoa kwa njia hiyo kunamnufaisha anayepokea na anayetoa pia. (Methali 11:25; Luka 6:38) Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Matendo 20:35.

 Ni wakati gani ambapo Mungu anafurahi tunapotoa?

 Mungu anafurahi tunapotoa kwa hiari. Biblia inasema hivi: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si bila kutaka wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”​—2 Wakorintho 9:7, maelezo ya chini.

 Kutoa kwa hiari ni “namna ya dini” ambayo Mungu anakubali. (Yakobo 1:27, maelezo ya chini) Mtu anayewasaidia wengine kwa ukarimu anafanya kazi pamoja na Mungu, ambaye anaona ukarimu huo kuwa mkopo kwake. (Methali 19:17) Biblia inafundisha kwamba Mungu atamlipa yule anayetoa.​—Luka 14:12-​14.

 Ni wakati gani ambapo Mungu hafurahi tunapotoa?

 Tunapotoa kwa nia mbaya. Ifuatayo ni mifano kadhaa:

 Ikiwa zawadi yetu itatumiwa kuunga mkono utendaji na mitazamo ambayo Mungu anashutumu. Kwa mfano, lingekuwa kosa kumpa mtu pesa za kucheza kamari au kutumia kileo vibaya au dawa za kulevya. (1 Wakorintho 6:9, 10; 2 Wakorintho 7:1) Vivyo hivyo, si sawa kumpa mtu ambaye anaweza kujitegemeza lakini anakataa kufanya kazi.​—2 Wathesalonike 3:​10.

 Wakati ambapo kutoa kunaingilia majukumu tuliyopewa na Mungu. Biblia inafundisha kwamba vichwa vya familia wanapaswa kuandaa mahitaji ya familia zao. (1 Timotheo 5:8) Si jambo linalofaa kwa kichwa cha familia kuwapa wengine kupita kiasi hivi kwamba familia yake inateseka. Vivyo hivyo, Yesu aliwashutumu wale waliokataa kuwaandalia wazazi wao waliozeeka kwa kudai kwamba mali zao zote zilikuwa “zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu.”​—Marko 7:​9-​13.