Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NJIA YA MAISHA INAYOLETA FURAHA

Kuridhika na Kuwa Mkarimu

Kuridhika na Kuwa Mkarimu

NI MARA NYINGI KADIRI GANI UMESIKIA WATU WAKIPIMA FURAHA NA MAFANIKIO KWA MSINGI WA MALI AU UTAJIRI? Kwa sababu ya mtazamo huo, mamilioni ya watu hufanya kazi kwa bidii na kwa saa nyingi ili wapate pesa zaidi. Lakini je, pesa na mali huleta furaha ya kudumu? Uthibitisho unafunua nini?

Kulingana na jarida moja (Journal of Happiness Studies), mahitaji yetu ya msingi yanapotimizwa, kuwa na pesa zaidi hakutatuongezea furaha wala kuboresha hali yetu ya moyoni. Pesa zenyewe si tatizo. “Kuzifuatia kupita kiasi ndiko hufanya mtu akose furaha,” inaeleza makala moja ya gazeti Monitor on Psychology. Maneno hayo yanafanana na ushauri wa Biblia uliotolewa miaka elfu mbili hivi iliyopita: “Kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo, wengine . . . [wamejichoma] kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Maumivu hayo yanatia ndani nini?

WASIWASI NA KUKOSA USINGIZI KWA SABABU MALI ZINAHITAJI KULINDWA. “Usingizi wa mtumishi ni mtamu, iwe anakula kidogo au kingi, lakini wingi alionao tajiri haumruhusu kulala usingizi.”—Mhubiri 5:12.

KUTAMAUKA TUNAPOKOSA FURAHA TULIYOITARAJIA. Kwa kiasi fulani, hali hiyo ya kutamauka inatokea kwa sababu tamaa ya pesa haiwezi kutoshelezwa. “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.” (Mhubiri 5:10) Vilevile, njaa ya utajiri inaweza kumsukuma mtu kudhabihu mambo muhimu sana yanayoleta furaha, kama vile wakati wa kuwa pamoja na familia na marafiki au kufanya mambo ya kiroho.

KUKATA TAMAA NA KUHUZUNIKA PESA NA MALI TULIZOWEKEZA ZINAPOSHUKA THAMANI AU ZINAPOTULETEA HASARA. “Usijichoshe kupata utajiri. Acha, na uonyeshe uelewaji. Ukiutupia jicho, haupo, kwa maana hakika utaota mabawa kama ya tai na kuruka mbali angani.”—Methali 23:4, 5.

SIFA ZINAZOLETA FURAHA

KURIDHIKA. “Hatukuleta chochote ulimwenguni, wala hatuwezi kuondoka na chochote. Basi, tukiwa na chakula na mavazi, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:7, 8) Watu walioridhika huwa hawalalamiki wala kunung’unika, na mtazamo wao unawasaidia wasiwe wenye wivu. Na kwa sababu wanaishi kulingana na kipato chao, hawawi na mahangaiko wala mkazo usio wa lazima.

UKARIMU. “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Watu wakarimu wana furaha kwa sababu wanapenda kufanya wengine wawe na furaha, hata ikiwa kitu pekee wanachoweza kutoa ni muda au nguvu zao. Mara nyingi, wao hupendwa na kuheshimiwa, na hupata marafiki wa kweli ambao ni wakarimu pia, mambo ambayo pesa haziwezi kununua!—Luka 6:38.

KUWATHAMINI WATU KULIKO VITU. “Ni afadhali kula mboga za majani mahali penye upendo kuliko kula ng’ombe dume aliyenoneshwa mahali penye chuki.” (Methali 15:17) Maana yake? Uhusiano mzuri na wengine ni wenye thamani kuliko utajiri wa kimwili. Na kama tutakavyoona baadaye, upendo unahitajika sana ili kuwa mwenye furaha.

Sabina, mwanamke anayeishi Amerika Kusini, alijifunza thamani ya kanuni za Biblia. Akiwa ametelekezwa na mume wake, Sabina alihangaika kupata mahitaji ya msingi kwa ajili yake na binti zake wawili. Alifanya kazi sehemu mbili tofauti na kila siku aliamka saa 10 usiku. Licha ya kwamba ratiba yake ilikuwa imebanana sana, Sabina aliamua kujifunza Biblia. Matokeo?

Hali yake ya kiuchumi haikubadilika sana. Lakini, mtazamo wake wa maisha ulibadilika kwa kiwango kikubwa! Kwa mfano, alipata furaha inayotokana na kutimiza uhitaji wa kiroho. (Mathayo 5:3) Alipata marafiki wa kweli miongoni mwa waabudu wenzake. Na alipata furaha inayotokana na kutoa kwa kuzungumza na wengine mambo aliyojifunza.

Biblia inasema: “Hekima hutetewa kwa matokeo yake.” (Mathayo 11:19; maelezo ya chini) Kwa msingi huo, kuridhika, kuwa mkarimu, na kuwathamini watu kuliko vitu, sikuzote kutathibitika kuwa jambo sahihi la kufanya.