Hamia kwenye habari

Vita vya Har-Magedoni Ni Nini?

Vita vya Har-Magedoni Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Vita vya Har-Magedoni ni vita vya mwisho kati ya serikali za wanadamu na Mungu. Hata sasa, serikali hizo na watu wanaoziunga mkono wanampinga Mungu kwa kukataa kujitiisha chini ya utawala wake. (Zaburi 2:2) Vita vya Har-Magedoni vitakomesha utawala wa wanadamu.​—Danieli 2:​44.

 Neno “Har-Magedoni” linapatikana mara moja tu katika Biblia, kwenye Ufunuo 16:16. Kwa njia ya kinabii, kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” watakusanywa pamoja “mahali panapoitwa katika Kiebrania Har-Magedoni,” kwa ajili ya “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.”​—Ufunuo 16:14.

 Ni nani watakaopigana katika Har-Magedoni? Yesu Kristo ataliongoza jeshi la kimbingu kushinda maadui wa Mungu. (Ufunuo 19:11-​16, 19-​21) Maadui hao wanatia ndani watu wanaopinga mamlaka ya Mungu na wanaomtendea Mungu kwa dharau.​—Ezekieli 39:7.

 Je, vita vya Har-Magedoni vitapiganwa kihalisi huko Mashariki ya Kati? Hapana. Badala ya kupiganwa katika eneo fulani hususa, vita vya Har-Magedoni ni vita vya dunia nzima.​—Yeremia 25:32-​34; Ezekieli 39:17-​20.

 Neno Har–​Magedoni (Kiebrania Har Meghiddohnʹ), linamaanisha “Mlima wa Megido.” Megido lilikuwa jiji katika eneo la kale la Israeli. Historia inaonyesha kwamba vita vya kukata maneno vilipiganwa katika eneo hilo, kutia ndani vita fulani ambavyo vimerekodiwa katika Biblia. (Waamuzi 5:​19, 20; 2 Wafalme 9:​27; 23:29) Hata hivyo, Har-Magedoni hairejelei eneo fulani hususa karibu na jiji la kale la Megido. Hakuna mlima mkubwa hapo, na ile nchi tambarare ya chini ya Yezreeli haiwezi kuwatosha wote watakaopigana dhidi ya Mungu. Badala yake, Har-Magedoni ni hali ya ulimwenguni pote ambayo mataifa yote yatajikusanya ili kuupinga utawala wa Mungu kwa mara ya mwisho.

 Hali zitakuwaje wakati wa vita vya Har-Magedoni? Ingawa hatujui jinsi Mungu atakavyotumia nguvu zake, atatumia silaha sawa na zile alizotumia zamani, yaani, mvua ya mawe, matetemeko ya nchi, mvua ya mafuriko, moto na kiberiti, radi, na magonjwa. (Ayubu 38:22, 23; Ezekieli 38:19, 22; Habakuki 3:​10, 11; Zekaria 14:12) Kwa sababu ya kuvurugika, baadhi ya maadui wa Mungu watauana wenyewe kwa wenyewe, lakini mwishowe watatambua kwamba Mungu ndiye anayepigana nao.​—Ezekieli 38:21, 23; Zekaria 14:13.

 Je, Har-Magedoni ndio mwisho wa ulimwengu? Hautakuwa mwisho wa sayari yetu, kwa kuwa dunia ni makao ya milele ya wanadamu. (Zaburi 37:29; 96:10; Mhubiri 1:4) Kwa kweli, kusudi la vita vya Har-Magedoni ni kuiokoa jamii ya wanadamu, si kuiangamiza, kwa kuwa “umati mkubwa” wa watumishi wa Mungu wataokoka.​—Ufunuo 7:​9, 14; Zaburi 37:34.

 Ingawa neno “ulimwengu” hutumiwa kuirejelea dunia, nyakati nyingine Biblia hulitumia kurejelea jamii ya wanadamu waovu wanaompinga Mungu. (1 Yohana 2:​15-​17) Katika maana hiyo, vita vya Har-Magedoni vitaleta “mwisho wa ulimwengu.”​—Mathayo 24:3, King James Version.

 Vita vya Har-Magedoni vitapiganwa lini? Alipokuwa akizungumzia ile “dhiki kuu” itakayofikia upeo wake kwenye vita vya Har-Magedoni, Yesu alisema hivi: “Kuhusu siku ile na saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.” (Mathayo 24:21, 36) Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba vita vya Har-Magedoni vitaanza wakati wa kuwapo kwa Yesu kusikoonekana. Kipindi hicho kilianza mwaka wa 1914.​—Mathayo 24:37-​39.